slider gif

slider gif

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

Wednesday, May 23, 2018

WAZIRI KIGWANGALLA AFANYA MAZUNGUMZO NA BALOZI WA ITALIA NCHINI, ROBERTO MENGONI

 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla akizungumza na Balozi wa Italia nchini, Roberto Mengoni ofisini kwake Jijini Dodoma leo ambapo wamekubaliana kuimarisha ushirikiano kwenye tafiti za binadamu wa kale katika eneo la Olduvai, kuboresha utoaji wa elimu hususan ya mapishi ya vyakula vya Kiitaliano katika Chuo cha Taifa cha Utalii na Utangazaji wa vivutio vya utalii nchini. 
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla akiwa kwenye picha ya pamoja na Balozi wa Italia nchini, Roberto Mengoni baada ya mazungumzo ofisini kwake Jijini Dodoma leo.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla akiagana na Balozi wa Italia nchini, Roberto Mengoni baada ya mazungumzo ofisini kwake Jijini Dodoma leo.

MAPORI MATANO YA AKIBA MKOANI KAGERA NA GEITA KUPANDISHWA HADHI YA KUWA HIFADHI ZA TAIFA (NATIONAL PARKS)

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt Hamisi Kigwangalla akizungumza bungeni alipokuwa akijibu hoja wa wabunge waliochangia mjadala wa bajeti wa kupitisha makadirio ya mapato na matumizi ya wizara yake kwa mwaka wa fedha 2018/2019, jijini Dodoma juzi.

............................................................

Wizara ya Maliasili na Utalii imetangaza kuanza mchakato wa kuyapandisha hadhi Mapori ya Akiba ya Burigi, Kimisi, Biharamulo, Ibanda na Rumanyika kuwa Hifadhi za Taifa.

Mchakato huo tayari umeungwa mkono na Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli.

Hayo yameelezwa juzi bungeni Jijini Dodoma na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla wakati akihitimisha mjadala wa bajeti wa makadirio ya mapato na matumizi ya wizara yake kwa mwaka wa fedha 2018/2019.

“Mheshimiwa Spika, ninaomba kulitaarifu Bunge lako tukufu kuwa  Mhe. Rais ameridhia ombi letu la kupandisha hadhi Mapori ya Akiba ya Burigi, Kimisi, Biharamulo, Ibanda na Chief Rumanyika kuwa Hifadhi za Taifa, kipekee namshukuru sana Mhe. Rais kwa kuridhia ombi letu hilo” amesema Dkt. Kigwangalla.

Amesema kufuatia hatua hiyo, wizara yake inaanzisha mchakato rasmi wa kukamilisha taratibu  za kupandisha hadhi mapori hayo ili kupanua wigo wa vivutio vya utalii katika kanda ya Kaskazini Magharibi na hivyo kufikia azma ya Serikali kuongeza idadi ya watalii kufikia milioni 8 na mapato ya dola za kimarekani bilioni 16 katika kipindi cha miaka 7 ijayo.

Inaelezwa kuwa mchakato huo utapitia hatua mbalimbali ikiwemo kuwashirikisha wadau husika kupata maoni yao, mapendekezo kuwasilishwa baraza la mawaziri kabla ya kujadiliwa bungeni na hatimaye kuwasilishwa kwa Mhe. Rais kwa ajili ya kuidhinishwa kuwa Sheria kamili ya kupandisha hadhi mapori hayo.

Akizungumzia mikakati mingine mipya ya kuboresha sekta ya maliasili na utalii itakayotekelezwa, Dkt. Kigwangalla amesema ni pamoja na kuanzisha mamlaka ya usimamizi na uendelezaji wa utalii wa fukwe nchini, kuhuisha maeneo ya vivutio vya Mambo ya Kale na kuviunganisha katika 'package' moja ya utalii na vivutio vya wanyamapori.

Mikakati mingine ni kuunda mfumo mmoja funganishi wa TEHAMA uitwao "MNRT Portal" kwa ajili ya kutoa leseni na vibali, ukusanyaji wa takwimu na mapato kutoka vyanzo mbalimbali vya sekta ya maliasili na utalii, ambapo utaunganishwa na mifumo mingine ya Serikali iliwemo GePG, NIDA, TIRA, BRELA, TRA na NBS.

Amesema mikakati mingine ni kuanzisha Jeshi Usu, Utambulisho wa Utalii wa Tanzania Kimataifa ujulikanao kama "Tanzania, Unforgettable", kufungua utalii wa kanda ya kusini, kuanzisha mwezi wa maadhimisho ya Urithi wa Mtanzania "Urithi Festival"  (Septemba), kuhuisha sheria za TANAPA, TAWA na TFS, pamoja na kuunda kanuni mpya za kusimamia vizuri sekta hizo.

Pori la Akiba Burigi lina ukubwa wa kilomita za mraba 2,941 katika wilaya za Karagwe, Muleba na Ngara mkoani Kagera, wakati Pori la Kimisi likiwa na ukubwa wa kilomita za mraba 1,030 katika wilaya za Ngara na Karagwe mkoani humo.

Pori la Akiba Biharamulo lina ukubwa wa kilomita za mraba 731 katika wilaya ya Muleba mkoani Kagera na wilaya ya Chato mkoani Geita, huku Pori la Akiba Ibanda likiwa na ukubwa wa kilomita za mraba 200 na Pori la Akiba Rumanyika kilomita za mraba 800 katika wilaya ya Kyerwa mkoani Kagera.

Mapori haya yapo katika ukanda muhimu wa kuunganisha watalii kutoka ikolojia za Magharibi na Mashariki ambapo uwanja wa ndege wa Chato utakuwa muhimu katika kutoa mawasiliano.

Mapori hayo ambayo yanasimamiwa na Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania - TAWA sasa yatakuwa chini ya Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania - TANAPA punde baada ya mchakato wa kuyapandisha hadhi kukamilika. 

Bunge limeidhinisha Sh. bilioni 115.794 kwa ajili ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa mwaka wa fedha 2018/2019 ambapo Sh. bilioni 85.816 ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na Sh. bilioni 29,978 ni kwa ajili ya miradi ya maendeleo. 
  Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga akizungumza bungeni alipokuwa akijibu hoja wa wabunge waliochangia mjadala wa bajeti wa kupitisha makadirio ya mapato na matumizi ya wizara yake kwa mwaka wa fedha 2018/2019, jijini Dodoma juzi.
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt Hamisi Kigwangalla na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga wakipongezwa na wabunge mbalimbali baada ya bajeti ya wizara yao kupitishwa na Bunge juzi jioni.
Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Maj. Gen. Gaudence Milanzi (kushoto), Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Shirika la Hifadhi za Taifa - TANAPA na Mkuu wa Majeshi Mstaafu, Jenerali George Waitara (katikati) na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Mamlaka ya Hifadhi ya Wanyamapori Tanzania - TAWA, Meja  Jenerali (Mstaafu) Hamis Rajabu SEMFUKO wakiwa kwenye picha ya pamoja nje ya ukumbi wa Bunge muda mfupi baada ya bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii kupitishwa na Bunge.
 Picha ya pamoja ya Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt Hamisi Kigwangalla, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga, Katibu Mkuu, Maj. Gen. Gaudence Milanzi, Naibu Katibu Mkuu, Dkt. Aloyce Nzuki, Wakuu wa Idara, Vitengo na Taasisi pamoja na wafanyakazi wa wizara hiyo baada ya bajeti ya wizara yao kupitishwa na Bunge juzi jioni. 

Sunday, May 13, 2018

MADHIMISHO YA KIMONDO CHA MBOZI KUFANYIKA KWA MARA YA KWANZA MWEZI JUNI, 2018

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga akiangalia Kimondo cha Mbozi alipotembelea kijiji cha Ndolezi, wilaya ya Mbozi mkoani Songwe jana kwa ajili ya kuangalia maandalizi ya maadhimisho ya siku ya kimondo duniani yatakayofanyika Juni 28 hadi 30 mwaka huu. Kimondo cha Mbozi ni cha pili kwa ukubwa barani Afrika na kinakadiriwa kuwa na tani 12 na mchanganyiko wa madini ya Chuma 90%, Nickel 8.69%, Copper 0.66%, Sulphur 0.01% na Phosphorus 0.11.

Na Hamza Temba-WMU-Songwe
..........................................................................
Mkoa wa Songwe kwa kushirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii na wadau wengine wa uhifadhi na maendeleo utafanya maadhimisho ya siku ya Kimondo cha Mbozi kwa mara ya kwanza katika historia kwenye Kijiji cha Ndolezi Kata ya Mlangali, wilayani Mbozi kuanzia Juni 28 hadi 30 mwaka huu .

Maadhimisho hayo yataenda sambamba na maadhimisho ya siku ya Vimondo duniani ambayo yaliazimiwa kufanyika Juni 30 kila mwaka na kikao cha Umoja wa Mataifa cha tarehe 6 Desemba, 2016.

Pamoja na mambo mengine, kikao hicho pia kiliazimia tarehe hiyo kuwa siku ya kuelimisha umma kuhusu elimu ya anga na mafanikio ya tafiti mbalimbali yaliyopatikana kuhusu elimu hiyo, kutambua juhudi zilizofanyika, kuweka sheria za kimataifa na kutoa tahadhari juu ya athari zinazoweza kutokea endapo dunia itafanya uharibifu juu ya anga.

Taarifa hiyo imetolewa jana katika Kijiji cha Ndolezi wilayani Mbozi na Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Songwe, Herman Tesha wakati akiwasilisha taarifa ya maandalizi ya maadhimisho hayo kwa Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga ambaye alitembelea kituo hicho kwa ajili ya kukagua shughuli za maandalizi.

Amesema lengo la maadhimisho hayo ni kutangaza Kimondo kama kivutio muhimu cha utalii mkoani Songwe pamoja na vivutio vingine vya mkoa huo kwa ujumla ili kutoa fursa ya uwekezaji kwenye sekta ya utalii mkoani humo. 

Amesema maadhimisho hayo yataenda sambamba na kongamano la uwekezaji na sayansi ya vimondo, maonesho ya malikale, maonesho ya kiutamaduni, mashindano ya riadha (Kimondo Marathon), mashindano ya netiboli na mpira wa miguu (Kimondo Ligi).

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga amesema Serikali kupitia Wizara yake itashiriki kikamilifu katika maadhimisho hayo kwa kushirikiana na mkoa wa Songwe na wadau wengine ili kuhakikisha kivutio hicho cha Kimondo kinajulikana zaidi ndani na nje ya nchi na hatimaye kiongeze idadi ya watalii na mapato.

Amesema wizara yake ina mkakati maalum wa kuimarisha kituo hicho cha utalii ambapo hivi sasa imeshajenga kituo maalum cha taarifa ambacho kimegharimu zaidi ya Shilingi milioni 400 za Kitanzania. 

Aidha, amesema kupitia mkakati mpya wa wizara wa kuimarisha na kuvijengea uwezo vituo vya malikale nchini kwa kuzishirikisha taasisi za uhifadhi wa wanyamapori na misitu, Shirika la Hifadhi za Taifa Tanapa litashirikiana na kituo hicho kwa kuimarisha miundombinu pamoja na utangazaji. 

Nao wananchi wa kijiji cha Ndolezi wakizungumza kwa nyakati tofauti hawakusita kuonyesha furaha zao kuhusu maendeleo ya eneo hilo na kuahidi kutoa ushirikiano kwa Serikali katika mipango na miradi mbalimbali itakayoanzishwa katika eneo hilo kwa faida ya pande zote mbili.

Katika hatua nyingine, baada ya kuhitimishwa kwa ratiba za Mwenge wa Uhuru wilayani Mbozi, wakimbiza Mwenge Kitaifa walilazimika kutumia fursa ya uwepo wao wilayani humo kwenda kutalii kwenye kivutio cha Kimondo wakati wa usiku wakiongozwa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga. 

Kimondo cha Mbozi kilianguka mwaka 1840 kutoka kwenye obiti yake huko angani huku kikikadiriwa kuwa na tani 12 na mchanganyiko wa madini ya Chuma 90%, Nickel 8.69%, Copper 0.66%, Sulphur 0.01% na Phosphorus 0.11. Kimomdo hicho ni cha pili kwa ukubwa barani Afrika na cha nane duniani kati ya vimondo 600 vilivyodondoka maeneo mbalimbali ulimwenguni, sifa yake kubwa ni kuwa na ubaridi wakati wote hata mchana wa jua kali.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga akikagua mpaka wa eneo la kituo cha kimondo na vijiji jirani alipotembelea kituo hicho cha utalii  katika kijiji cha Ndolezi, wilaya ya Mbozi mkoani Songwe jana kwa ajili ya kuangalia maandalizi ya maadhimisho ya siku ya kimondo duniani yatakayofanyika Juni 28 hadi 30 mwaka huu. Kimondo cha Mbozi ni cha pili kwa ukubwa barani Afrika na kinakadiriwa kuwa na tani 12 na mchanganyiko wa madini ya Chuma 90%, Nickel 8.69%, Copper 0.66%, Sulphur 0.01% na Phosphorus 0.11.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga akikagua kituo cha taarifa cha Kimondo cha Mbozi alipotembelea kituo hicho cha utalii  katika kijiji cha Ndolezi, wilaya ya Mbozi mkoani Songwe jana kwa ajili ya kuangalia maandalizi ya maadhimisho ya siku ya kimondo duniani yatakayofanyika Juni 28 hadi 30 mwaka huu. Kimondo cha Mbozi ni cha pili kwa ukubwa barani Afrika na kinakadiriwa kuwa na tani 12 na mchanganyiko wa madini ya Chuma 90%, Nickel 8.69%, Copper 0.66%, Sulphur 0.01% na Phosphorus 0.11.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga akizungumza na baadhi ya watalii wa ndani waliotembelea kituo cha utalii cha kimondo katika kijiji cha Ndolezi, wilaya ya Mbozi mkoani Songwe jana. Nyuma yao ni jengo jipya la kituo cha taarifa ambalo ujenzi wake umekamilika.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya watalii wa ndani waliotembelea kituo cha utalii cha kimondo katika kijiji cha Ndolezi, wilaya ya Mbozi mkoani Songwe jana. Nyuma yao ni jengo jipya la kituo cha taarifa ambalo ujenzi wake umekamilika. Kimondo cha Mbozi ni cha pili kwa ukubwa barani Afrika na kinakadiriwa kuwa na tani 12 na mchanganyiko wa madini ya Chuma 90%, Nickel 8.69%, Copper 0.66%, Sulphur 0.01% na Phosphorus 0.11.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga (nyuma kulia) akiwa kwenye picha ya pamoja na Wakimbiza Mwenge kitaifa, Mkuu wa Wilaya ya Mbozi, Ernest Palingo (kushoto) na waratibu wa Mwenge mkoa wa Songwe mbele ya Kimondo cha Mbozi katika kijiji cha Ndolezi, wilaya ya Mbozi mkoani Songwe jana usiku baada ya shughuli za Mwenge. Kimondo hicho ni cha pili kwa ukubwa barani Afrika na kinakadiriwa kuwa na tani 12 na mchanganyiko wa madini ya Chuma 90%, Nickel 8.69%, Copper 0.66%, Sulphur 0.01% na Phosphorus 0.11.

Saturday, May 12, 2018

WAZIRI KIGWANGALLA AMTEUA MISS JOURNALISM TANZANIA 2018 KUWA BALOZI WA UTALII WA PORI LA AKIBA SELOUS

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akizungumza na Miss Journalism Tanzania, 2018, Witness Teddy Kavumo (21) ambaye pia ni mshindi wa mwaka jana wa mataji manne ya Uanamitindo nchini Afrika ya Kusini, alipomtembelea ofisini kwake Jijini Dodoma mwishoni mwa wiki kwa ajili ya kuomba ufadhili wa kushiriki mashindano ya Dunia ya Miss Journalism yatakayofanyika Jijini Arusha mwezi Oktoba mwaka huu. Aidha, amemteua mwanamitindo huyo kuwa balozi wa utalii wa Pori la Akiba Selous. 

Na Hamza Temba-WMU-Dodoma
.............................................................................
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla amemteua mshindi wa taji la Miss Journalism Tanzania, 2018, Witness Teddy Kavumo (21) kuwa balozi wa utalii wa Pori la Akiba Selous.

Amefanya uteuzi huo mwishoni mwa wiki Jijini Dodoma baada ya mazungumzo na mwanamitindo huyo aliyemtembelea ofisini kwake kwa ajili ya kuomba ufadhili wa kuandaa  mradi wa kijamii ambao ni sehemu ya shindano atakaloshiriki la taji la Dunia la Miss Journalism 2018 litakalofanyika Oktoba 27 Jijini Arusha.

Kufuatia uteuzi huo, Dk. Kigwangalla amemuagiza Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Utalii Tanzania, Devotha Mdachi kuandika barua ya uteuzi kwa balozi huyo mpya sambamba na kumkabidhi hati ya uteuzi ili pamoja na mambo mengine aweze kunadi vivutio vya utalii vya pori hilo.

Wakati huo huo, Dk. Kigwangalla amemuagiza Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania TAWA, Dk. James Wakibara kuandaa safari maalum ya balozi huyo mteule aweze kutembelea Pori la Akiba Selous kwa ajili ya kuona na kujifunza mambo mbalimbali yanayohusu hifadhi hiyo kwa ajili ya utangazaji.

Sambamba na pori hilo atatembelea pia mapori mengine ikiwemo BBK (Burigi, Biharamulo na Kimisi) mkoani Kagera na Mpanga Kipengele mkoani Njombe ambapo  atatumia fursa hiyo kufanya mahojiano na wasichana wa vijiji jirani na hifadhi hizo kwa ajili ya mradi wa kijamii wa kuwainua ikiwa ni sehemu yenye alama muhimu kwenye shindano hilo la Dunia la Miss Journalism 2018.

Awali akiwasilisha ombi lake kwa Waziri Kigwangalla la ufadhili wa safari yake ya ushiriki wa mashindano hayo, Witness pia aliomba kupewa fursa ya kuwa balozi wa Tanzania kwenye moja ya sekta ikiwemo Misitu, Nyuki au Utalii.

Mbali na kushikilia taji la Miss Journalism Tanzania 2018, Witness amesema amewahi kushinda mataji mengine manne makubwa ya kimataifa ya ulimbwende nchini Afrika ya Kusini anakosomea urubani kwa sasa.

Anasema, "Miongoni mwa mataji hayo ni Miss Garden Route 2017, ambalo ni taji la kitaifa la kuhamasisha na kukuza sekta ya Maliasili na Utalii nchini humo, licha ya kuwa ugenini nilitumia fursa hiyo kunadi vivutio vya utalii vya Tanzania. 

"Mashindano haya yalihusisha washiriki 600 na wote walikuwa na asili ya kizungu, mimi peke yangu nilikuwa na asili ya kiafrika na niliibuka mshindi". 

Aliyataja mataji mengine kuwa ni Miss Bees Cape Town 2017 kwa ajili kuhamasisha uhifadhi wa sekta ya nyuki na mataji mawili ya kimkoa ambayo ni Miss Asla Capetown 2017 na Miss Carnival Mosselbay 2017.

Mataji mengine ya kitaifa aliyowahi kushinda Witness hapa nchini ni pamoja na Miss Arusha Higher Learning 2014 na Miss Northern Zone 2014.

Mashindano hayo ya Dunia ya Miss Journalism 2018 yanahusisha pia uhamasishaji wa maendeleo ya utalii, utamaduni wa amani, uandishi wa habari na kupiga vita ugonjwa wa ukimwi na Malaria.

Pori la akiba Selous ndio hifadhi kubwa kuliko zote nchini ikiwa na ukubwa wa kilomita za mraba takriban 50,000 katika mikoa ya Pwani, Morogoro, Lindi, Mtwara na Ruvuma. Mwaka 1982, Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (Uneso) lilitangaza eneo hilo kuwa moja ya eneo la Urithi wa Dunia na kuanza kuhifadhiwa.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akionyeshwa taji la urembo la "Miss Garden Route South Africa 2017" ambalo ni maalum kwa ajili ya kuhamasisha utalii nchini Afrika ya Kusini na Miss Journalism Tanzania 2018, Witness Teddy Kavumo (21) aliyeshinda taji hilo na mataji mengine matatu nchini humo mwaka jana, alipomtembelea ofisini kwake mwishoni mwa wiki kwa ajili ya kuomba ufadhili wa kushiriki kwenye mashindano ya Dunia ya Miss Journalism yatakayofanyika Jijini Arusha mwezi Oktoba mwaka huu. Aidha, amemteua mwanamitindo huyo kuwa balozi wa vivutio vya utalii vya Pori la Akiba Selous. 
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akiwa kwenye picha ya pamoja na Miss Journalism Tanzania, 2018, Witness Teddy Kavumo (21) ambaye pia ni mshindi wa mwaka jana wa mataji manne ya Uanamitindo nchini Afrika ya Kusini, alipomtembelea ofisini kwake Jijini Dodoma mwishoni mwa wiki kwa ajili ya kuomba ufadhili wa kushiriki mashindano ya Dunia Miss Journalism yatakayofanyika Jinini Arusha mwezi Oktoba mwaka huu. Aidha, amemteua mwanamitindo huyo kuwa balozi wa vivutio vya utalii vya Pori la Akiba Selous.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akiagana na Miss Journalism Tanzania, 2018, Witness Teddy Kavumo (21) ambaye pia ni mshindi wa mwaka jana wa mataji manne ya Uanamitindo nchini Afrika ya Kusini, baada ya mazungumzo ofisini kwake Jijini Dodoma alipomtembelea mwishoni mwa wiki kwa ajili ya kuomba ufadhili wa kushiriki mashindano ya Dunia ya Miss Journalism yatakayofanyika Jinini Arusha mwezi Oktoba mwaka huu. Aidha, amemteua mwanamitindo huyo kuwa balozi wa wa utalii wa Pori la Akiba Selous. 

Friday, May 11, 2018

DK. KIGWANGALLA AFUNGUA WARSHA YA KITAIFA YA MAPITIO YA RASIMU YA SERA YA TAIFA YA UTALII YA MWAKA 2018 JIJINI DODOMA

Waziri wa Maliasili na Utalii Dk. Hamisi Kigwangalla akifungua Warsha ya Kitaifa ya Mapitio ya Rasimu ya Sera ya Taifa ya Utalii ya mwaka 2018 Jijini Dodoma leo.
............................................

WAZIRI wa Maliasili na Utalii,Dk.Hamisi Kigwangalla amesema  Serikali itaendelea kutekeleza sera ya Taifa ya Utalii  kwa ushirikiano na wadau katika usimamizi, uhifadhi na matumizi endelevu ya rasilimali za maliasili na utalii nchini.

Dk. Kigwangalla ametoa kauli hiyo Jijini Dodoma leo wakati akifungua warsha ya kitaifa ya mapitio ya rasimu ya Sera ya Taifa ya Utalii ya mwaka 2018.

Amesema mafanikio ya sekta ya utalii yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na uwepo wa Sera ya Taifa ya Utalii ya mwaka 1999 na juhudi za Serikali katika kutekeleza sera hiyo kwa ushirikiano na Wadau katika usimamizi, uhifadhi na matumizi endelevu ya rasilimali za utalii, utangazaji katika masoko mbalimbali ya utalii duniani na mazingira bora ya uwekezaji.

“Wote tunaelewa ya kuwa Utalii ni moja ya sekta zinazokua kwa kasi na hivyo kuchangia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa uchumi wa nchi na kupunguza umasikini wa kipato”.

Amesema ukuaji wa sekta hiyo, umedhihirika pale ambapo katika miaka ya hivi karibuni mapato yatokanayo na utalii yaliongezeka kutoka Dola za Marekani bilioni 1.7 mwaka 2012 hadi kufikia Dola za Marekani bilioni 2.2 mwaka 2017.

Amesema ongezeko la mapato hayo ni kutokana na ongezeko la idadi ya watalii kutoka 1,077,058 mwaka 2012 hadi kufikia watalii 1,327,143 mwaka 2017.

Waziri Kigwangalla amesema sekta ya utalii inachangia takriban asilimia 25 ya mapato yote ya fedha za kigeni (foreign exchange earnings).

Akizungumzia mambo yaliyowekewa mkazo katika rasimu hiyo amesema ni pamoja na Serikali kuendelea kushirikiana na wadau wote wa utalii katika kuhifadhi rasilimali za utalii.

“Kuendeleza rasilimali watu, kuimairisha ushirikiano wa kikanda na kimataifa, kuimarisha mnyororo wa thamani katika mazao ya utalii, kuongeza wigo wa mzao ya utalii kama vile kuendeleza utalii wa fukwe na utalii wa mikutano, kuweka mkazo katika kutangaza Tanzania kama kituo bora cha utalii kimataifa.

“Napenda kusisitiza kuwa, Sera hii itakuwa na nyenzo nyingine muhimu za kuitekeleza ambazo ni Mkakati wa utekelezaji wa Sera na Progamu ya Maendeleo ya Utalii nchini.

“Tayari Wizara imeanza maandalizi ya awali ya kukamilisha nyenzo hizo na mtashirikishwa kikamilifu katika kuziandaa na utekelezaji wake,”amesema.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Meja Jenerali Gaudence Milanzi amesema sera ya Taifa ya Utalii iliyopo hivi sasa ilifanyiwa mapitio kwa mara ya mwisho mwaka 1999 ambapo ni takribani miaka 18 iliyopita.

Amesema kwa kutambua hilo, Wizara iliona kuna umuhimu mkubwa kupitia upya Sera hiyo ili kuhakikisha ukuaji wa Sekta ya Utalii nchini unaenda sambamba na mabadiliko mbalimbali yanayotokea duniani ikiwamo mabadiliko ya teknolojia, kijamii, kiuchumi, kisiasa na kimazingira.

Alisema kwa kuzingatia kuwa msingi mkuu wa kuandaa Sera yeyote ni kuwashirikisha wadau ambao ndio watekelezaji wa Sera hiyo, mapitio ya Sera hii, yameshirikisha wadau wote muhimu tangu hatua za awali.

“Kazi hii ilipangwa kufanyika kwa awamu tano (5) ambazo ni kukusanya maoni ya wadau katika kanda saba za Tanzania Bara na Zanzibar, uchambuzi wa maoni na kuandaa rasimu ya Sera, kuwasilisha rasimu ya Sera kwenye warsha ya kitaifa ambayo inafanyika leo na hatimaye kuandaa rasimu ya mwisho ya Sera na Mkakati wa Utekelezaji,” alisema.

Warsha hiyo imejumuisha wadau mbalimbali wa sekta ya umma na binafsi wanaohusika maendeleo ya sekta ya utalii nchini.
Waziri wa Maliasili na Utalii Dk. Hamisi Kigwangalla akifungua Warsha ya Kitaifa ya Mapitio ya Rasimu ya Sera ya Taifa ya Utalii ya mwaka 2018 Jijini Dodoma leo.
Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Meja Jenerali Gaudence Milanzi akizungumza katika warsha hiyo.
Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Meja Jenerali Gaudence Milanzi akizungumza katika warsha hiyo.
Mkurugenzi wa Idara ya Utalii, Wizara ya Maliasili na Utalii Deogracious Mdam akizungumza katika warsha hiyo.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa ESRF, Deodatus Sagamiko akizumza katika warsha hiyo. ESRF ni moja ya wadau wakuu waliofadhili zoezi hilo la kuhuisha sera ya taifa ya utalii.
 Baadhi ya wadau katika wa warsha hiyo.
 Baadhi ya washiriki wa warsha hiyo.
 Meza kuu.
 Wadau. 
  
 Picha ya pamoja.
 Picha ya pamoja.
 Picha ya pamoja.
Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Meja Jenerali Gaudence Milanzi (katikati) akifurahia jambo na Naibu Katibu wa Wizara hiyo, Dk. Aloyce Nzuki (kulia) na Mkurugenzi wa Idara ya Utalii, Deogracious Mdam wakati Warsha ya Kitaifa ya Mapitio ya Rasimu ya Sera ya Taifa ya Utalii ya mwaka 2018 Jijini Dodoma leo.
 Waziri wa Maliasili na Utalii Dk. Hamisi Kigwangalla akiteta jambo na mdau wa utalii, Dk. Leaky Abdallah wakati wa Warsha ya Kitaifa ya Mapitio ya Rasimu ya Sera ya Taifa ya Utalii ya mwaka 2018 Jijini Dodoma leo.
Baadhi ya wadau wa utalii kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii.

Sunday, May 6, 2018

TANZANIA YATAJWA KUWA BUSTANI YA EDEN NA CHIMBUKO LA MWANADAMU WA KALE DUNIANI


Hatimaye utata uliokuwa ukiendelea duniani kwa watafiti wa mambo ya kale kuhusiana na mahali mwanadamu wa kwanza alipotokea umemalizika baada ya jopo la wataalam liloundwa na Wizara ya Maliasili na Utalii kufuatia ushahidi wa vinasaba kubaini kuwa binadamu huyo alitokea barani Afrika huku ikidaiwa kuwa ni Tanzania eneo la Olduvai Gorge.

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Japhet Hasunga wakati wa mkutano wa wadau wa sekta ya ufugaji nyuki aloiutisha kujadili maendeleo ya sekta hiyo Jijini Dodoma mwishoni mwa wiki.

Amesema  utafiti huo umeshirikisha wataalamu kutoka mataifa mbalimbali duniani na kuwa kumalizika kwake kutaiwezesha sekta ya utalii nchini kukua kwa kasi sambamba na kuongeza pato la taifa.

Saturday, May 5, 2018

SERIKALI YAELEZA FURSA ILIYOPO KATIKA UFUGAJI WA NYUKI

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga (katikati) akizungumza na wadau wa sekta ya ufugaji nyuki nchini katika kikao alichokiitisha kujadili maendeleo ya sekta hiyo ikiwemo marekebisho ya kanuni za ufugaji nyuki za mwaka 2017 katika ukumbi wa Hazina Jijini Dodoma leo. Kushoto ni MKuu wa Kitengo cha Masoko, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania, Mwanahamisi Mapolu na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Misitu na Nyuki wa Wizara hiyo, Deosdedit Bwoyo.

Dodoma
.............................................................

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga ametoa wito kwa wananchi kutumia fursa kubwa iliyopo hapa nchini ya ufugaji nyuki na uwepo wa masoko ya ndani na nje ya nchi kwa kuongeza uzalishaji wa mazao yake na kuyaongezea thamani ili kuinua uchumi wao na taifa kwa ujumla.

Ametoa wito huo leo mbele ya wadau wa sekta ya ufugaji nyuki kutoka mikoa yote nchini katika mkutano aliouitisha kujadili maendeleo ya sekta hiyo ikiwemo marekebisho ya kanuni za ufugaji nyuki za mwaka 2017 katika ukumbi wa Hazina Jijini Dodoma.

Amesema kwa sasa mchango wa sekta ya nyuki katika pato la taifa bado ni mdogo ukilinganisha na fursa zilizopo za ufugaji nyuki hapa nchini ambazo zikitumiwa ipasavyo zitasaidia kuinua pato la wananchi na taifa kwa ujumla.

Amesema mbali na kuongeza uzalishaji, mazao hayo pia yanatakiwa kuongezewa thamani na kuwekewa ngazi za ubora ili yaweze kuhimili masoko ya ndani na nje ya nchi.

Ameongeza kuwa, ili kuimarisha sekta hiyo Serikali itashirikiana na wadau kutatua changamoto zilizopo ikiwemo kutafuta masoko, kuimarisha uwekezaji na kuanzisha viwanda vidogo vya kuchakata mazao ya nyuki ikiwemo asali na nta ambayo ina soko kubwa nje ya nchi.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Misitu na Nyuki wa wizara hiyo, Deosdedit Bwoyo amesema Tanzania ni moja kati ya nchi 50 duniani zenye utajiri mkubwa wa rasilimali za misitu ambazo zinatoa fursa pana ya ufugaji nyuki nchini.

Amesema eneo la misitu ni takriban hekta milioni 48.1 ambalo ni asilimia 54 ya ukubwa ardhi yote ya Tanzania ambayo ikitumiwa ipasavyo na wananchi itawawawezesha kujiajiri na kuongeza uzalisahaji wa mazao ya nyuki na mapato.

Amesema ili kulinda mazalia ya nyuki na kuongeza uzalishaji wa mazao ya nyuki nchini, Serikali kupitia Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania TFS, imeanzisha hifadhi za nyuki 11 huku Serikali za vijiji zikianzisha hifadhi za nyuki 14.

Wadau walioshiriki mkutano huo ambao ni wazalishaji, wachakataji na wasafirishaji wameishukuru Serikali kwa kuandaa mkutano huo na kuiomba kusaidia katika tafiti, elimu kwa wananachi wanaojihusisha na ufugaji nyuki hususan maeneo ya vijijini na utafutaji wa masoko ya uhakika.Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga (kushoto) akizungumza na wadau wa sekta ya ufugaji nyuki nchini katika kikao alichokiitisha kujadili maendeleo ya sekta hiyo ikiwemo marekebisho ya kanuni za ufugaji nyuki za mwaka 2017 katika ukumbi wa Hazina Jijini Dodoma leo.Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Misitu na Nyuki wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Deosdedit Bwoyo akiwasilisha hotuba yake kwa wadau hao.Mkurugenzi Msaidi wa Uendelezaji Nyuki wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Allen Richard akitambulisha meza kuu katika mkutano huo.Wadau wa Misitu na Nyuki wakisikiliza hotuba ya mgeni rasmi ambaye ni Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga (hayupo pichani). Katikati ni Magdalena Muya wa Wizara ya Maliasili na Utalii na Stephen Msemo kutoka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (kulia).Baadhi ya wadau walioshiriki mkutano huo.Mmoja ya wadau wa sekta ya ufugaji nyuki nchini akitoa maoni yake.Mmoja ya wadau wa sekta ya ufugaji nyuki nchini akitoa maoni yake.Picha ya pamoja ya Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga na wadau wa sekta ya ufugaji nyuki nchini wakati wa kikao alichokiitisha kujadili maendeleo ya sekta hiyo ikiwemo marekebisho ya kanuni za ufugaji nyuki za mwaka 2017 katika ukumbi wa Hazina Jijini Dodoma leo.Picha ya pamoja ya Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga na wadau wa sekta ya ufugaji nyuki nchini wakati wa kikao alichokiitisha kujadili maendeleo ya sekta hiyo ikiwemo marekebisho ya kanuni za ufugaji nyuki za mwaka 2017 katika ukumbi wa Hazina Jijini Dodoma leo.