slider gif

slider gif

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

Tuesday, January 1, 2019


NAIBU WAZIRI MHE,KANYASU AWAFUNDA WATUMISHI WA  TFS PAMOJA NA WANANCHI


Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Constantine Kanyasu amewaonya wananchi  wanaofanya shughuli za kibinadamu ndani ya Hifadhi za Misitu nchini kuacha tabia ya kuwashambulia Watumishi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) wanapokuwa wanatekeleza majukumu yao.

Onyo hili linakuja ikiwa zaidi ya watumishi watano wa TFS  katika mikoa ya Pwani, Tabora ,Kigoma pamoja Kilimanjaro wakiwa wamepoteza maisha yao kwa kushambuliwa na wananchi wakati wakiwa wanatekeleza majukumu yao.

Aidha, Mhe.Kanyasu amewapiga marufuku watumishi wa TFS kujichukulia sheria mkononi kwa kuwapiga wananchi wanapobainika kutenda makosa.

"Watumishi wa TFS hamruhusiwi   kumpiga Mwananchi mnapomkamata ndani ya Hifadhi au akiwa anasafirisha mazao ya Misitu kinyume na sheria, atakayebainika sheria itachukua mkondo wake.

Ametoa  onyo hilo wakati akizungumza na wananchi  kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika  katika kata ya Mgusu  wilayani  Geita mkoani Geita ikiwa ni ziara yake ya kutatua migogoro ya mipaka kwenye msitu wa Hifadhi Geita iliyopo baina ya Vijiji ambapo jumla ya hekta 4,462.95 zimefutwa kwa tangazo la Serikali.


Amesema shughuli za uhifadhi ni lazima zifanyike kwa ushirikishwaji kati ya wananchi na watumishi wa TFS.

" Uhasama unaozidi kujengeka kati yenu  hauna tija katika uhifadhi shirikianeni" amesisitiza Mhe.Kanyasu.

Aidha,  Mhe . Kanyasu amewataka wananchi kuheshimu na kuzifuata sheria za uhifadhi ya Misitu nchini huku akiwataka  watumishi kujiepusha na migongano kati yao na wananchi.

Katika hatua nyingine, Mhe.Kanyasu amewataka wananchi wafuate sheria kwa kulipia vibali kwa TFS pale wanapokuwa na mahitaji ya mazao ya Misitu badala ya kusubilia mpaka wakamatwe.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Geita, Mhe.Josephat Maganga amemueleza Naibu Waziri huyo kuwa hali ya Misitu katika wilaya hiyo ni mbaya kufuatia shughuli za kibinadamu zinazoendelea kufanyika Misitu hiyo.

Hata hivyo, Mkuu huyo wa Wilaya  hiyo Mhe.Maganga alisema kufuatia hali hiyo tayari  Kamati ya Ulinzi na Usalama kwa kushirikiana TFS wameshaanza kufanya  doria ya kuwaondoa wafugaji na wakulima waliovamia  Hifadhi.

Katika hatua nyingine, Diwani ya Kata ya Mgusu, Pastory Lugusa amemuomba  Naibu Waziri huyo kumegewa eneo la Hifadhi  kwa vile idadi ya wakazi wa kata hiyo imeongezeka hali inayopelea kukosa maeneo kwa ajili  ya malisho na Kilimo.

Kwa upande wake Meneja wa Misitu  wa  wilaya wa TFS, Fedy Ndandika amemuhakikishia Naibu Waziri kuwa  watashirikiana na wananchi hata hivyo tayari wameanza kutoa elimu ya umuhimu wa uhifadhi kwa jamii zinazozunguka Hifadhi


Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe.Constantine Kanyasu  akiwa na kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya ya Geita mkoani Geita akipewa maelezo na Meneja wa Misitu  wa  wilaya wa Wakala wa Huduma ya Misitu Tanzania (TFS) Fedy Ndandika wakati alipotembelea eneo la Manga lililokuwa limevamiwa na wakulima ambayo ni moja ya eneo la Msitu wa Hifadhi  Geita
 
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe.Constantine Kanyasu akizungumza na wananchi  kwenye mkutano wa hadhara katika kata ya Mgusu, Halmashauri ya wilaya ya  Geita mkoani Geita akiwasisitiza wananchi umuhimu wakufuata  sheria na kuacha tabia ya kuvamia Hifadhi za Misitu
 Baadhi ya wananchi wakimsikiliza Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe.Constantine Kanyasu wakati wa mkutano huo wa hadhara.

 Mkazi wa kata ya Mgusu, Anaeli Mbokile akizungumza mbele ya Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe.Constantine Kanyasu akiwasilisha ombi  la kumegewa eneo la Hifadhi ya Msitu Geita ili liweze kutumika kwa ajili ya malisho na makazi baada ya wakazi wa kata ya Mgusu idadi ya kuongezeka.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe.Constantine Kanyasu akiteta jamabo na baadhi ya wanachama wa CCM  wakati alipomaliza mkutano wa hadhara katika  kata ya Mgusu mkoani Geita.