slider gif

slider gif

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

Wednesday, March 21, 2018

ATUMIA MIEZI SABA KUSAFIRI KWA PIKIPIKI KUTOKA OMAN HADI TANZANIA, ATEMBELEA WIZARA YA MALIASILI NA UTALII MJINI DODOMA


 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga akiteta jambo na Maher Al Barwani kutoka nchi ya Oman mwenye asili ya Tanzania ambaye amesafiri kwa muda wa miezi saba kupitia mataifa mbalimbali hadi kufika Tanzania kwa pikipiki kwa lengo la kuimarisha uhusiano uliopo baina ya nchi hizo mbili pamoja na kutangaza utalii wa Tanzania nchini humo, alipotembelea ofisi za Wizara hiyo mjini Dodoma. 
 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga akiteta jambo na Maher Al Barwani kutoka Oman mwenye asili ya Tanzania ambaye amesafiri kwa muda wa miezi saba kupitia mataifa mbalimbali hadi kufika Tanzania kwa pikipiki kwa lengo la kuimarisha uhusiano uliopo baina ya nchi hizo mbili pamoja na kutangaza utalii wa Tanzania nchini humo alipotembelea ofisi za Wizara hiyo mjini Dodoma jana. Kulia ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dk. Aloyce Nzuki na Mkurugenzi wa Idara ya Utawala, Tutubi Mangazeni. 
 Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Dk. Aloyce Nzuki akiteta jambo na Maher Al Barwani kutoka Oman mwenye asili ya Tanzania ambaye amesafiri kwa muda wa miezi saba kupitia mataifa mbalimbali hadi kufika Tanzania kwa pikipiki kwa lengo la kuimarisha uhusiano uliopo baina ya nchi hizo mbili pamoja na kutangaza utalii wa Tanzania nchini humo alipotembelea ofisi za Wizara hiyo mjini Dodoma jana. Kulia ni Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga. 
 Picha ya pamoja ya Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Japhet Hasunga (kulia) na Maher Al Barwani, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dk. Aloyce Nzuki na Mkurugenzi wa Idara ya Utawala, Tutubi Mangazeni.
 Maher al Barwani akimuelezea Ndugu David ambeye ni Afisa Usafirishaji wa Wizara ya Maliasili na Utalii jinsi alivyoweza kutumia usafiri huo wa pikipiki kutoka nchini Oman hadi Tanzania.
 Maher al Barwani anapatikana kupitia Mawasiliano hayo.
 Kwa muda wa miezi saba Maher al Barwani ameweza kusafiri umbali wa kilomita 18,035.6 kutoka Oman hadi ofisi za Makao Makuu ya Wizara ya Maliasili na Utalii mjini Dodoma.
 Pikipiki anayotumia aina ya BMW ina uwezo wa kukimbia kwa spidi 240.
Maher al Barwani akiondoka baada ya kusalimiana na viongozi wa viwaza mjini Dodoma. 
(PICHA NA HAMZA TEMBA-WMU-DODOMA)

Tuesday, March 20, 2018

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI, MHE. JAPHET HASUNGA AZINDUA MABASI MAWILI MAPYA YA WIZARA HIYO MJINI DODOMA

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe, Japhet Hasunga akiendesha moja ya basi hilo kama ishara ya uzinduzi.

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe, Japhet Hasunga amezindua rasmi mabasi mawili aina ya TATA kwa ajili kutoa huduma za usafiri wa kwenda na kurudi kazini kwa Watumishi wa Wizara hiyo walioko mjini Dodoma.
Akizungumza baada ya uzinduzi huo, Naibu Waziri Hasunga amesema mabasi hayo yatasadia kukabiliana na changamoto ya usafiri iliyokuwepo hususan kwa wale watumishi wa Wizara wanaotumia ofisi zilizopo Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM).
Aidha, ametoa wito kwa madereva na watumishi watakaotumia mabasi hayo kuyatunza ili yaweze kudumu kwa muda mrefu.
Mabasi hayo ya uwezo wa kuchukua abiria 91 wakiwa wamekaa ambapo basi moja kubwa lina uwezo wa kuchukua abiria 51 na lingine dogo abiria 40.
Naye Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Rasilimali Watu wa Wizara hiyo, Tutubi Mangazeni amesema mabasi hayo yatatumika pia kwa ajili ya shughuli nyingine za Kiserikali ikiwemo kuwasafirisha Watumishi wa Umma watakaohitaji kutembelea maeneo ya Hifadhi na kushirikia kwenye michezo mbalimbali hapa nchini.
Mabasi hayo yamegharimu jumla ya Shilingi Milioni 232 za Kitanzania.


Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe, Japhet Hasunga (kulia), Naibu Katibu Mkuu, Dk. Aloyce Nzuki (kushoto) na Mkurugenzi wa Idara ya Utawala, Tutubi Mangazeni wakiwa wameketi kwenye viti vya moja ya basi hilo baada ya uzinduzi.

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga (nyuma) akiongozwa na Naibu Katibu Mkuu, Dk. Aloyce Nzuki kukagua moja ya basi hilo.

Monday, March 12, 2018

TANZANIA NA UJERUMANI ZAKUBALIANA KUENDELEZA TAFITI ZA MASALIA YA MIJUSI KATIKA ENEO LA TENDAGURU MKOANI LINDI

Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii Maj. Gen. Gaudence S. Milanzi (kushoto) akipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa Makumbusho ya Historia Asilia ya Berlin Ujerumani (Berlin Museum of Natural History), Prof. Johannes Vogel kuhusu masalia ya mjusi wa Tanzania yaliyofadhiwa katika makumbusho hiyo.

.....................................................

Ujerumani na Tanzania zimekubaliana kuendeleza tafiti za masalia ya mijusi katika eneo la Tendaguru mkoani Lindi.

Makubaliano hayo yamefikiwa baada ya Katibu Mkuu, Wizara ya Maliasili na Utalii, Maj. Gen. Gaudence Milanzi kutembelea Makumbusho ya Historia Asilia ya Berlin (Berlin Museum of Natural History) nchini Ujerumani yanapohifadhiwa pia masalia ya mijusi waliopatikana eneo la Mlima Tendaguru mkoani Lindi.

Maj. Gen. Milanzi aliongoza msafara wa Tanzania ulioshiriki maonesho ya Kimataifa ya utalii ya ITB Berlin 2018 yaliyohitimishwa jana nchini Ujerumani. Maonesho hayo yaliyoanza tarehe 7 mwezi huu yalihusisha taasisi 5 za Serikali na Makampuni binafsi 60 kutoka Tanzania.

Mkurugenzi Mkuu wa Makumbusho hiyo, Prof. Johannes Vogel alimueleza Maj. Gen. Milanzi kuwa shughuli kubwa inayofanywa na makumbusho hiyo ni utafiti kwa ajili ya maendeleo ya sayansi, elimu na ufahamu wa mambo mbalimbali kuhusu Dunia, viumbe pamoja na mazingira ili maarifa na ufahamu huo usaidie binadamu kutawala maisha yake na mazingira yanayomzunguka.

Akizungumzia fursa zilizopo za kushirikiana kutafiti maeneo yalikopatikana masalia ya mijusi hao na viumbe wengine Prof. Johannes alisema, Makumbusho yake ipo tayari kushirikiana na Wanasayansi wa Tanzania ili kujenga uwezo wa kufanya utafiti na kupata matokeo yatakayochangia katika hazina ya maarifa na sayansi ya viumbe na mazingira.

“Ili kuwa na utafiti endelevu, ni vema kwa nchi ikawekeza kwa wataalamu wake ili kuendeleza utafiti na maendeleo ya sayansi.  Hivyo tupo tayari kushirikiana ili kujenga uwezo kwa wasomi wa Tanzania kuweza hatimaye kufanya utafiti na kuleta maendeleo kwa nchi yao” alisema.

Akizungumzia kuhusu masalia ya mijusi waliopatikana Tendaguru na ambayo yanahifadhiwa katika makumbusho hiyo, alisema badala ya kuwarudisha nchini Tanzania, ni vema wakachukuliwa kuwa elimu, utafiti na maendeleo ya sayansi yanayopatikana kutokana na kuwafanyia utafiti ni kwa maendeleo na ustawi wa dunia nzima.

“Ichukuliwe kuwa huu ni urithi wa dunia nzima na hivyo ni wajibu wetu kuhakikisha kuwa urithi huu hauachi ukapotea.  Hivyo, ni vema tukaimarisha utafiti katika eneo walikopatikana ili kupata masalia mengi zaidi na kuitangaza Tanzania katika Nyanja za utafiti.

“Makumbusho yangu ipo tayari kufanya ziara ya kuimarisha mazungumzo na mamlaka za Tanzania mapema iwezekanavyo ili utafiti katika eneo la Tendaguru uendelee kwa manufaa ya Tanzania na Dunia nzima”. alisema Prof. Johannes. 

Kwa upande wake Katibu Mkuu Milanzi aliahidi kuwapa ushirikiano ili kuwezesha tafiti hizo kufanyika kwa ajili ya ustawi wa sayansi na uchumi wa nchi zote mbili.  Alimkaribisha Prof. Johannes na timu yake kuja Tanzania mapema iwezekanavyo ili kujadili na kukamilisha makubaliano ya kuendeleza tafiti hizo.

Awali, Maj. Gen. Milanzi alipata fursa ya kuonana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Tanzania nchini Ujerumani, Dk. Abdalla Possi. Miongoni mwa mambo waliyozungumza ni pamoja na masalia hayo ya mjusi wa Tanzania anayehifadhiwa katika moja ya makumbusho nchini humo.

Balozi Possi alisema kuwa kwa maoni yake haoni kuwa wazo la kuhamisha masalia hayo kurudishwa Tanzania kuwa litakuwa na tija kwa maendeleo ya utalii na utafiti wa sayansi kwa nchi yetu. 

Alitoa baadhi ya sababu kuwa sio kweli kuwa masalia hayo ndiyo kivutio kikubwa pekee kinachofanya wanasayansi na watalii wengi kutembelea makumbusho hiyo na hivyo kuipa mapato makumbusho hiyo. 

“Makumbusho inapata ruzuku kutoka serikalini na kiingilio ni sehemu ndogo sana ya mapato ya makumbusho hiyo.  Fedha nyingi za kufanyia shughuli za Makumbusho ya Berlin zinatokana na fedha zinazolipwa kwa ajili ya kufanya utafiti na si viingilio katika makumbusho” alisema Dk. Possi.

Alisema makumbusho hiyo ina mikusanyo mingi ya viumbe mbalimbali zaidi ya milioni 30 ikiwemo ya mijusi kutoka nchi nyingine duniani.  Mkusanyiko huo kwa pamoja unatoa mvuto kwa watafiti na watalii kutembelea na kufanya shughuli zao chini ya makumbusho hiyo. 

Dk. Possi alisema kuendelea kuwepo masalia hayo katika makumbusho hiyo kuna manufaa zaidi ya kuitangaza Tanzania kiutalii na utafiti wa kisayansi kuliko masalia hayo yatakapoondolewa katika makumbusho hiyo na kurejeshwa nchini Tanzania. 

Alisema kuwepo masalia hayo katika makumbusho hiyo ni kama Balozi wa utalii na utafiti wa kisayansi anayeitangaza Tanzania sehemu mbalimbali duniani. 

Akizungumzia mchakato unaoendelea hivi sasa hapa nchini wa kuandaa Utambulisho mpya wa Tanzania (National Branding), Balozi Possi alishauri kuwa ni vema mabadiliko yatakayopelekea kuondokana na utambulisho unaotumika hivi sasa ukaangaliwa kwa umakini kwa kuwa kuna hatari ya kupoteza msisitizo uliopo katika vivutio maarufu vya utalii nchini na kutoa fursa kwa washindani kutangaza utalii wao kupitia vivutio hivyo.

Alisema endapo hakuna athari kwa kutumia utambulisho wa sasa ambao ni maarufu (Tanzania the Land of Kilimanjaro, Serengeti and Zanzibar), ni vema zikaangaliwa pia athari zitakazopatikana kwa kuachana na “brand” inayotumika hivi sasa.

Alisema kuwa baadhi ya vitu vinavyotumika kwenye utambulisho wa sasa tayari ni “brand”.  Alitoa mfano kuwa Mlima Kilimanjaro ni Brand maarufu na inayojiuza, hali kadhalika kwa Serengeti na Zanzibar.

Saturday, March 10, 2018

TANZANIA YASHIRIKI MAONESHO YA KIMATAIFA YA UTALII YA ITB BERLIN 2018 NCHINI UJERUMANI

Picha ya pamoja ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii Maj. Gen. Gaudence S. Milanzi (wa tano kushoto) na baadhi ya washiriki wa maonesho ya Kimataifa ya Utalii ya ITB 2018 yanayoendelea Jijini Berlin nchini Ujerumani

Na Mwandishi Wetu - Berlin, Ujerumani
.................................................................................
Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii Maj. Gen. Gaudence S. Milanzi ameongoza msafara wa Tanzania unaoshiriki katika Maonesho ya Kimataifa ya Utalii ya ITB 2018 yanayoendelea Jijini Berlin nchini Ujerumani.

Lengo la Maonesho hayo ni kutangaza fursa za utalii zilizopo nchini Tanzania katika masoko mbalimbali ya utalii barani Ulaya na duniani kote.


Sekta ya utalii inachangia wastani wa asilimia 25 ya fedha zote za kigeni zinazoingia nchini Tanzania huku ikichangia asilimia 17.5 ya pato la Taifa.


Maonesho hayo yalianza tarehe 7 mwezi huu na yanatarajiwa kufikia tamati keshokutwa tarehe 11 Machi, 2018. Ushiriki wa Tanzania katika maonesho hayo umehusisha Sekta ya Umma na Sekta Binafsi.

Washiriki kutoka sekta ya umma ni pamoja na Idara ya Utalii – Wizara ya Maliasili na Utalii, Bodi ya Utalii Tanzania, Shirika la Hifadhi za Taifa, Mamlaka ya Hifadhi Ngorongoro na Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania.

Kwa upande wa Sekta Binafsi jumla ya kampuni 60 zimeshiriki maonyesho hayo ikiwemo Kampuni moja inayoshughulika na uratibu wa matukio (Events and Exhibitions management), Kampuni tatu zinazoshughulika na usafiri wa anga, Kampuni ishirini na saba zinazoshughulika na huduma za malazi (hoteli, loji na kambi za utalii), na Kampuni ishirini na tisa za Wakala wa biashara ya kusafirisha watalii.

Pamoja na shughuli za maonyesho hayo, Katibu Mkuu Milanzi amefanya pia mikutano kadhaa na wadau wa utalii na washirika wa maendeleo waliopo nchini Ujerumani.
 Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Maj. Gen. Gaudence Milanzi (wa pili kulia) akijadili jambo na wadau walioshiriki maonesho hayo kutoka Tanzania. Kulia ni Mkurugenzi wa Idara ya Utalii TANAPA, Ibrahim Mussa.

Friday, March 2, 2018

TUTAENDELEZA UTALII WA PICHA KATIKA PORI LA AKIBA BURIGI - DK. KIGWANGALLA, WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII


Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akiangalia Twiga katika fukwe za ziwa Burigi ndani ya Pori la Akiba Burigi mkoani Kagera.
Baadhi ya Twiga wanaopatikana katika Pori la Akiba Burigi. 
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akipata maelezo kutoka kwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Malmlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania, David Kanyata kuhusu mipango mbalimbali ya mamlaka hiyo kuendeleza utalii katika Pori la Akiba Burigi alipotembelea pori hilo jana mkoani Kagera.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akiangalia mandhari fukwe ya ziwa Burigi kwa kutumia darubuni alipotembelea Pori la Akiba Burigi mkoani Kagera jana. Utalii wa fukwe ni moja ya kivutio muhimu cha utalii katika pori hilo ambapo watalii hupata fursa ya kuona wanyamapori mbalimbali wakiwemo viboko, simba, tembo, pundamilia na ndege aina mbalimbali.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akishuka ngazi kwa ajili ya kukagua fukwe za ziwa Burigi.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akishiriki kusukuma boti iingie kwenye maji kwa ajili ya kunza ziara ya kukagua fukwe za ziwa Burigi alipotembelea Pori la Akiba Burigi mkoani Kagera jana. Utalii wa fukwe ni moja ya kivutio muhimu cha utalii katika pori hilo ambapo watalii hupata fursa ya kuona wanyamapori mbalimbali wakiwemo viboko, simba, tembo, pundamilia na ndege aina mbalimbali.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akipiga kasia tayari  kwa kwa kuanza Safari ya boti kwa ajili ya kukagua fukwe ya ziwa Burigi alipotembelea Pori la Akiba Burigi mkoani Kagera jana. 
Ndege aina mbalimbali pia ni kivutio katika pori hilo.
Viboko nao wanapatikana katika pori hilo ndani ya ziwa Burigi.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akishuka kwenye boti baada ya kukagua fukwe ya ziwa Burigi alipotembelea Pori la Akiba Burigi mkoani Kagera jana kwa ajili ya kukagua shughuli za uhifadhi. Utalii wa fukwe ni moja ya kivutio muhimu cha utalii katika pori hilo ambapo watalii hupata fursa ya kuona wanyamapori mbalimbali wakiwemo viboko, simba, tembo, pundamilia na ndege aina mbalimbali.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akishuka kwenye boti baada ya kukagua fukwe ya ziwa Burigi alipotembelea Pori la Akiba Burigi mkoani Kagera jana kwa ajili ya kukagua shughuli za uhifadhi.
Picha ya pamoja kati ya Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla na watumishi wa Pori la Akiba Burigi.
Picha ya pamoja. (Imeandaliwa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Malisili na Utalii)

Wednesday, February 28, 2018

SERIKALI YAAGIZA OPERESHENI YA KUONDOA WAVAMIZI WA KIGENI KATIKA KISIWA CHA IZINGA MKOANI KAGERA


.........................................................................................
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla ametoa siku 7 kwa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania TAWA  kwa kushirikiana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Karagwe kufanya Operesheni ya kuwaondoa wavamizi wa nchi jirani wanaodaiwa kulima na kufiga ndani kisiwa cha Izinga kilichopo ndani ya Pori la Akiba la Kimisi mkoani Kagera.

Ametoa agizo hilo jana wakati wa ziara yake wilayani Karagwe mkoa wa Kagera muda mfupi baada ya kupokea taarifa na malalamiko ya kukamatwa kwa mifugo ya Watanzania ndani ya kisiwa cha Mubali huku kukiwepo mazao yanayodaiwa kulimwa na wananchi wa Rwanda katika kisiwa kingine cha Izinga.

“Ndani ya siku saba hicho kisiwa cha Zinga msafishe kila kitu, Mkuu wa Wilaya msaidie mtengeneze kikosi kiende kule kitoe takataka zote zilizoko kule, inakua ngumu kuadministrate (kutawala) wengine wa kwetu tunawatoa alafu wa nchi nyingine wamekaa, unatawalaje?”. Aliuliza kwa mshangao Dk. Kigwangalla.

Alisema watanzania wakienda upande wa Rwanda kuvua samaki ziwa Ihema wanauawa mara moja bila mjadala, wakati kwa upande wa Tanzani raia wa nchi hiyo wapo wengi na wengine wamepewa Uraia wa Kuasili (Citizenship by Naturalisation, CN) na huwa hawafanyiwi vitendo vya unyanyasaji wala mauaji  jambo ambalo alisema  ipo haja kama nchi kuchukua hatua ili kukomesha vitendo hivyo.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania, David Kenyata alisema atatekeleza agizo hilo la Waziri Kigwangalla kwa haraka ndani ya muda uliotolewa ili kumaliza mgogoro huo.

Katika hatua nyingine Waziri Kigwangalla alikataa ombi la Mbunge wa Jimbo la Karagwe, Innocent Bashugwa la kuiomba Serikali iwamegee wananchi wa vijiji jirani sehemu ya eneo katika Pori la Akiba Kimisi kwa ajili ya shughuli za kilimo na ufugaji.

“Ardhi mimi sitatoa, sjui mlima sjui nini, siwezi kwenda kupeleka hilo ombi kwa Mhe. Rais, kabisa, hicho ni kitu ambacho hatuwezi kufanya kwa sasa’,” Alisisitiza Dk. Kigwangalla.

Mbunge huyo pia aliiomba Serikali kuweka uzio wa waya kwa ajili ya kutenganisha mpaka wa hifadhi hiyo na vijiji kwa madai ya kuepuka ukamataji wa mifugo ya wananchi unaofanywa na askari wa wanyamapori kwenye ardhi za vijiji na kuingizwa hifadhini na kutozwa faini, hoja iliyopigwa vikali na Mkuu wa Wilaya ya Karagwe, Godfrey Mheluka.

Hata hivyo, Dk. Kigwangalla alikataa ombi hilo na kusema kuwa mipaka ya hifadhi hiyo ni mikubwa kuwezesha utekelezaji wa ombi hilo. Alisema Serikali itatengeneza mtandao wa barabara zinazounganisha hifadhi hiyo na vijiji kwa ajili ya kuimarisha doria na shughuli za utalii pamoja na kujenga ofisi ndogo za pori hilo katika kila wilaya inayohusika na pori hilo.

Mkuu wa Wilaya ya Karagwe, Godfrey Mheluka aliwataka wananchi wanaofanya vitendo vya kuingiza mifugo kwenye pori hilo wakati wa usiku kuacha mara moja kwa kuwa wakimatwa watachukuliwa hatua kali za kisheria.

Alisema malalamiko ya wananchi hao kuwa askari wa wanyamapori wanakamata mifugo yao kwenye maeneo ya vijiji na kuiingiza hifadhini kwa lengo la kuwatoza faini kuwa sio ya kweli na kwamba malalamiko yanakuja kwakuwa hukamatwa asubuhi wakiwa wameshatoka kulisha mifugo hifadhini.

Kisiwa hicho cha Izinga ambacho kipo katika wilaya ya Karagwe mkoani Kagera kina ukubwa wa Kilomita za Mraba 12 na kinapakana na nchi Rwanda.
Pori la Akiba Kimisi liliqnzishwa mwaka 2003 kwa Tangazo la Serikali na 116 na lina ukubwa wa kilomita za mraba 1,030. Pori hilo lina wanyamapori mbalimbali wakiwemo Tembo, Twiga, Simba na Chui. 
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akiongozana na Mbunge wa Jimbo la Karagwe, Innocent Bashugwa kukagua Pori la Akiba Kimisi wakati wa ziara yake ya kutatua migogoro ya ardhi kwenye maeneo ya hifadhi katika Wilaya ya Karagwe mkoani Kagera jana. 
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akizungumza na baadhi ya viongozi wa kijiji cha Mwisheni alipofika kukagua Pori la Akiba Kimisi wakati wa ziara yake ya kutatua migogoro ya ardhi kwenye maeneo ya hifadhi katika Wilaya hiyo mkoani Kagera jana.
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akiongozana na Mbunge wa Jimbo la Karagwe, Innocent Bashugwa kukagua Pori la Akiba Kimisi wakati wa ziara yake ya kutatua migogoro ya ardhi kwenye maeneo ya hifadhi katika Wilaya ya Karagwe mkoani Kagera jana. 
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akiteta jambo na Mkuu wa Wilaya ya Karagwe, Godfrey Mheluka wakati akikagua Pori la Akiba Kimisi akiwa kwenye ziara yake ya kutatua migogoro ya ardhi kwenye maeneo ya hifadhi katika Wilaya hiyo mkoani Kagera jana.
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akionyesha mpaka wa Pori la Akiba Kimisi wakati wa ziara yake ya kutatua migogoro ya ardhi kwenye maeneo ya hifadhi katika Wilaya hiyo mkoani Kagera jana. Kulia ni Mkuu wa Karagwe, Godfrey Mheluka na Mbunge wa Karagwe, Innocent Bashungwa (kulia kwake).
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akizungumza na Mkuu wa Wilaya ya Ngara, Lut. Col. Michael Mutenjele (kushoto) wakati wakivuka kivuko cha Ruvuvu wakati wa ziara yake ya kutembelea na kutatua migogoro ya ardhi kwenye maeneo ya hifadhi katika Wilaya hiyo mkoani Kagera jana. 
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akiangalia baadhi ya mifugo iliyokamatwa ndani ya Pori la Akiba Kimisi wakati wa ziara yake ya kutatua migogoro ya ardhi kwenye maeneo ya hifadhi katika Wilaya Ngara mkoani Kagera jana. (Picha na Wizara ya Maliasili na Utalii).