slider gif

slider gif

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

Monday, April 9, 2018

JENGO LA MAMLAKA YA HIFADHI YA NGORONGORO KUWA KIVUTIO CHA KIHISTORIA CHA UTOAJI WA HUDUMA ZA UTALII JIJINI ARUSHA



Na Hamza Temba - WMU
........................................................
JENGO la kitega uchumi la Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro jijini Arusha ambalo ujenzi wake unatarajiwa kukamilika mwezi juni mwaka huu litakuwa kivutio cha kihistoria cha utoaji wa huduma za utalii hapa nchini.

Hayo yameelezwa jana na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla muda mfupi baada ya kukagua jengo hilo ambalo linasemekana kuwa refu kuliko majengo yote jijini Arusha likiwa na jumla ya ghorofa 18.

Alisema jengo hilo ambalo linatizamana na Round About ya AICC katikati ya jiji hilo, limekusudiwa kuwa Kituo Kimoja (One Stop Centre) cha shughuli zote za utoaji wa huduma za utalii jijini humo kuanzia uwekezaji, utangazaji na menejimenti kwa ujumla.

Alisema jengo hilo litatoa fursa kwa wadau mbalimbali wanaotoa huduma za utalii kuweka ofisi zao ikiwemo mabenki, watoa huduma za usafiri, mashirika ya ndege, mawakala wa safari za utalii na huduma, maduka ya bidhaa za utalii na mahoteli.

"Tutapamba pia jengo hili na" live screen" (Mabango ya Video Mubashara) za vivutio, hivyo wanyama wakiwa wanapita huko porini watakuwa wanaonekana "LIVE" (Mubashara) kwenye jengo hili kupitia LED Screen ambazo zitakuwa zimezunguka jengo hili" alisema Dk. Kigwangalla.

Alisema huduma nyingine zitakazotolewa katika Jengo hilo ni pamoja na zile za kuangalia jiji la Arusha kupitia darubini, huduma za burudani ikiwemo kumbi za starehe na migahawa.

Kwa upande wake Mkandarasi wa jengo hilo, Mhandisi Bismas Meela wa Kampuni ya Inter-Consult limited alisema ujenzi wa jengo hilo ambalo ulianza mwezi Novemba, 2013 unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi juni mwaka huu.

Alisema jengo hilo ambalo lina uwezo wa kupaki magari 67 kwa wakati mmoja katika ghorofa za chini linagharimu shilingi za Kitanzania bilioni 45.

Katika ziara hiyo ya siku moja ya ukaguzi wa jengo hilo, Dk. Kigwangalla aliongozwa na Mhifadhi Mkuu wa Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro, Dk. Fredy Manongi na Naibu Mhifadhi wa Huduma za Uendeshaji wa Mamlaka hiyo, Asangye Bangu. 
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla (wa pili kushoto) akipata maelezo kutoka kwa Naibu Mhifadhi wa Huduma za Uendeshaji wa Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro, Asangye Bangu kuhusu jengo la kitega uchumi la mamlaka hiyo lililopo katikati ya Jiji la Arusha ambalo limekusudiwa kuwa Kituo Kimoja cha shughuli zote za utoaji wa huduma za utalii jijini humo kuanzia uwekezaji, utangazaji na menejimenti kwa ujumla. Kulia ni Mhifadhi Mkuu wa Mamlaka hiyo, Dk. Fredy Manongi.
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akiangalia mandhari ya Jiji la Arusha akiwa juu ya Jengo la kitega uchumi la Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro. Kutoka kulia ni Naibu Mhifadhi wa Huduma za Uendeshaji wa Mamlaka hiyo, Asangye Bangu na  Mhifadhi Mkuu wa Mamlaka hiyo, Dk. Fredy Manongi. 
Dk. Kigwangalla akiendelea kupata maelezo kuhusu jengo hilo kutoka kwa Naibu Mhifadhi wa Huduma za Uendeshaji wa mamlaka hiyo, Asangye Bangu. 

 Dk. Kigwangalla na msafara wake wakiangalia umbo la uso wa simba uliotengengenezwa katika moja lango la kuingilia kwenye lift ndani ya jengo hilo. Milango yote ya kuingilia kwenye lift ndani ya jengo hilo itapambwa kwa taswira mbalimbali za wanyamapori.
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akishuka kwenye ngazi maalum zinazotumia nishati ya umeme ndani ya Jengo hilo. Kulia ni Naibu Mhifadhi wa Huduma za Uendeshaji wa Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro, Asangye Bangu na nyuma yake ni Mhifadhi Mkuu wa Mamlaka hiyo, Dk. Fredy Manongi. \
Waziri Kigwangalla akikagua kabati la kuhifadhia vitu katika moja ya Hotel Aprtment ndani ya jengo hilo. Kulia ni Naibu Mhifadhi wa Huduma za Uendeshaji wa Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro, Asangye Bangu.
Muonekano wa jengo hilo kutokea barabara ya Makongoro Jijini Arusha.

Friday, April 6, 2018

AGIZO ALILOTOA WAZIRI KIGWANGALLA WILAYANI KISHAPU WAKATI WA KILELE CHA MAADHIMISHO YA UPANDAJI MITI KITAIFA



WAZIRI KIGWANGALLA AAGIZA KILA KIJIJI KUTENGA ENEO LA UHIFADHI WA MISITU, ATOA SIKU 7 KWA TFS KUWASILISHA MPANGO WA UVUNAJI

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga,Zainab Telack na Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri wakipanda mti wa kumbukumbu wakati wa kilele cha kuadhimisha siku ya upandaji miti kitaifa iliyofanyika jana katika kijiji cha Mhunze wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga.

Na Hamza Temba, WMU, Kishapu, Shinyanga
.......................................................................................
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla amewaagiza Wakuu wa Mikoa nchini kuhakikisha Halmashauri zote nchini zinatenga maeneo katika kila kijiji kwa ajili ya uhifadhi wa misitu ikiwa ni pamoja na vijiji hivyo kuunda kanuni na taratibu zao wenyewe za kusimamia maeneo hayo. 

Ametoa agizo hilo jana katika kijiji cha Mhunze wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga wakati wa kuhitimisha kilele cha Maadhimisho ya Upandaji Miti Kitaifa yaliyofanyika mkoani humo kuanzia Aprili 03 mwaka huu.

Katika kufanikisha zoezi hilo ameuagiza uongozi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kuchagua mikoa 10 ya kuanza utekelezaji wa agizo hilo ikiwemo mikoa ya Shinyanga na Tabora ambayo inakabiliwa na changamoto kubwa ya uharibifu wa misitu.

Ameugiza pia we uongozi huo wa TFS kuweka mpango wa uhifadhi wa misitu ya asili katika maeneo hayo kwa kushirikiana na vijiji kupanga maeneo yanayostahili kuhifadhiwa sambamba na kuwapa elimu ya umuhimu wa uhifadhi wa maeneo hayo.

Wakati huo huo Dk. Kigwangalla ametoa siku saba kwa uongozi huo wa Wakala wa Huduma za Misitu kuwasilisha kwake mpango wa tathmini ya uvunaji wa mazao ya misitu wa nchi nzima kwa kuzingatia kiasi cha rasilimali misitu kilichopo na kiwango halisi kitakachotakiwa kuvunwa ambacho hakitazidi robo ya rasilimali iliyopo.

"Hatuwezi kuendelea tu kutoa vibali vya kuvuna misitu hatujui tunavuna wapi, tuna rasilimali kiasi gani, wavune kiasi gani, hapana, mnitengenezee mpango laa sivyo nitasitisha uvunaji, nikisema nasitisha uvunaji nitapeleka waraka kwa Wakuu wa Mikoa, na nina uhakika kwa nguvu walinayo hawashindwi kuzuia uvunaji. 

"Kwahiyo TFS nawapa siku saba mniletee mpango wa tathmini ya namna ambavyo tuna rasilimali kwenye kila mkoa, tujue mkoa flani una miti cubic mita kadhaa ya mbao kadhaa, ya kuni kadhaa, ya mkaa kadhaa na kwa mwaka huu tutaruhusu wavune kwenye msitu fulani  kiasi kadhaa, twende kisayansi, sio Meneja wa TFS anakaa Wilayani anatoa vibali watu wanaenda kuvuna,".

Dk. Kigwangalla amesema  takwimu za uharibifu wa misitu hapa nchini zinatisha jambo ambalo likiachwa liendelee bila kuchukua hatua nchi itageuka kuwa jangwa.

"Kwa mwaka tunakata miti kwa mahitaji mbalimbali kati ya ekari 800,000 na 1,200,000.
Ili kurejesha walau nusu ya miti tunayokata kwa mwaka tunahitaji kupanda miti 3,000,000 kwa mwaka mfululizo kwa miaka 17 ili kufidia kiasi cha uharibifu tunachofanya kwa nusu mwaka" alisema Dk. Kigwangalla.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Misitu na Nyuki wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dk. Ezekiel Mwakalukwa ambaye alimuwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara hiyo alisema kumekuwepo na jitihada za kuandaa programu kubwa za kitaifa za uhifadhi wa mazingira katika maeneo mahususi yaliyoonekana kuzidiwa na tatizo la uharibifu wa mazingira. 

Alitaja Programu hizo kuwa ni Hifadhi Ardhi Dodoma (HADO), Hifadhi Ardhi Shinyanga (HASHI), na Hifadhi Mazingira Iringa (HIMA).

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack alisema mkoa wake kwa kushirikiana na uongozi wa mkoa wa Tabora umeanza kuchukua hatua za kurejesha uoto wa asili katika maeneo yao ikiwemo kuanzisha utaratibu wa kugawa miche ya miti kwa kila kaya pamoja na kuimarisha kamati za uhifadhi wa mazingira.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Taboba, Aggrey Mwanri alisema ushirikiano huo ni muhimu kwani utawezesha kukabiliana na changamoto zilizopo katika mikoa hiyo kwa kuweka mikakati ya pamoja wa kudhibiti vitendo vya uharibifu wa mazingira kwa kuzingatia sheria, taratibu na miongozo iliyopo.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga,Zainab Telack na Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri wakipanda mti wa kumbukumbu wakati wa kilele cha kuadhimisha siku ya upandaji miti kitaifa iliyofanyika jana katika kijiji cha Mhunze wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akiwahutubia wananchi wakati wa kuhitimisha kilele cha Maadhimisho ya Upandaji Miti Kitaifa yaliyofanyika kijiji cha Mhunze wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga jana.
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga,Zainab Telack na Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri wakiteta jambo wakati wa kilele cha kuadhimisha siku ya upandaji miti kitaifa iliyofanyika jana katika kijiji cha Mhunze wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga.
 Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga,Zainab Telack akiwahutubia wananchi wakati wa maadhimisho hayo.
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga,Zainab Telack na Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri wakiwasalimu wananchi wakati wa kilele cha kuadhimisha siku ya upandaji miti kitaifa iliyofanyika jana katika kijiji cha Mhunze wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga.
  Mkurugenzi wa Idara ya Misitu na Nyuki wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dk. Ezekiel Mwakalukwa ambaye alimuwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara hiyo akitoa maelezo kuhusu maadhimisho hayo.
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack na Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri wakielekea eneo la tukio la kupanda miti wakati wa kilele cha kuadhimisha siku ya upandaji miti kitaifa iliyofanyika jana katika kijiji cha Mhunze wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akishiriki kucheza ngoma wakati wa maadhimisho hayo.

Friday, March 30, 2018

WATALII WENGI WAZIDI KUTEMBELEA TANZANIA - WAZIRI KIGWANGALLA

Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dkt. Hamisi Kigwangalla (kushoto) akipokelwa na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Maj. Gen. Gaudensi Milanzi mjini Dodoma jana ambapo alikuwa mgeni rasmi katika Mkutano wa 25 wa Baraza la wafanyakazi wa Wizara hiyo.
.............................................................................
Tanzania imefanikiwa kuongeza idadi ya watalii kutoka 1,284,279 mwaka 2016 hadi kufikia 1,327,143  mwaka 2017 hali iliyopelekea  kuongezeka kwa mapato ya Serikali.

Akizungumza wakati wa Mkutano wa 25 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Maliasili na Utalii uliofanyika mjini Dodoma, Waziri wa Wizara hiyo, Dkt. Hamisi Kigwangalla amesema Wizara yake itaendelea kuvutia watalii wengi zaidi ili kukuza utalii na kuongeza pato la Taifa.

“Mapato yanayotokana na utalii yameongezeka kutoka Dola za Kimarekani Bilioni 2.1 mwaka 2016 hadi Dola za Kimarekani Bilioni 2.2 mwaka 2017” alisema Dk. Kigwangalla.

Akifafanua Dkt. Kigwangala amesema lengo la Serikali ni kuona mafanikio haya yanazidi kuimarika, hivyo kila mtumishi katika Wizara hiyo lazima atimize wajibu wake  ipasavyo katika kutimiza lengo la Wizara hiyo ambalo ni kuhifadhi na kusimamia maliasili, malikale na kuendeleza utalii.

Aliongeza kuwa ili kufanikisha majukumu ya Wizara hiyo ipasavyo ni muhimu kuwa na bajeti ambayo itawezesha kushughulikia changamoto za migogoro ya mipaka katika maeneo ya hifadhi, kufanya mapitio ya Sera, Sheria na Kanuni mbalimbali, upungufu wa watumishi, uhaba wa vitendea kazi, kutoa elimu ya maadili na kusimamia watumishi.

Alisema Wizara yake itaendelea na  mapambano dhidi ya ujangili, biashara haramu ya nyara, magogo na kuwachukulia hatua kali  za kinidhamu na kisheria kwa watumishi wote watakaogundulika kukiuka maadili ya utumishi wa umma kwa kushiriki katika vitendo hivyo.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Meja Jenerali Gaudensi Milanzi amesema kuwa Wizara hiyo itazingatia ushauri utakaotolewa na Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo ili kuongeza tija katika kutatua changamoto zinazojitokeza.

“Wizara itaendelea kupambana dhidi ya ujangili, biashara haramu ya nyara na magogo na kuwachukulia hatua kali watumishi wote watakaogundulika kukiuka maadili ya utumishi wa umma kwa kushiriki katika vitendo hivyo “ Alisisitiza Meja Jenerali Milanzi.

Wizara kwa mwaka wa fedha 2017/2018 iliendelea na utaratibu wa kuendeleza watumishi katika mafunzo ya aina mbalimbali kama ifuatavyo:-Jumla ya watumishi wanne (4) wanahudhuria mafunzo ya muda mrefu nje na ndani. Aidha, mtumishi mmoja(1) yupo nje ya nchi.

Watumishi wengine  kumi na moja (11) walihudhuria mafunzo ya muda mfupi. Mafunzo haya yalihusu watumishi wa kada mbalimbali.

Jumla ya watumishi saba (7) wamehudhuria mafunzo ya ujasiliamali unaohusiana na maandalizi ya kustaafu. Aidha, Wizara bado inaendelea na utaratibu wa kuwaandaa watumishi wote wanaokaribia kustaafu kuhakikisha wanapata mafunzo hayo. 

Akifunga mkutano huo wa siku moja Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Mhe. Japhet Hasunga aliwataka watumishi wa Wizara hiyo kufanya kazi kwa bidii, juhudi na maarifa ili kufikia lengo lililokusudiwa la uhifadhi wa maliasili, malikale na kuendeleza Utalii.
 Waziri wa Mali  Asili na Utalii Mhe. Dkt. Hamisi Kigwangalla akihutubia Wafanyakazi wa Wizara hiyo wakati wa Mkutano wa 25 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo uliofanyika mjini Dodoma jana.
 Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii Maj. Gen. Gaudensi Milanzi  akizungumza na Wafanyakazi wa Wizara hiyo wakati wa mkutano huo.
Baadhi ya wajumbe wa mkutano huo wa baraza wakisikiliza hotuba ya mgeni rasmi, Mhe. Dk. Hamisi Kigwangalla.
Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dkt. HamisI KigwangalLa  (katikati) akiimba wimbo wa mshikamano pamoja na Katibu Mkuu  Wizara hiyo, Maj. Gen. Gaudensi Milanzi pamoja na viongozi wengine wa Shirikisho la Wafanyakazi.
Baadhi ya ya Wakurugenzi na Wakuu wa Taasisi wa Wizara ya Maliasili na Utalii Wakiimba wimbo wa mshikamano wa wafanyakazi wakati wa mkutano huo uliofanyika mjini Dodoma.
Naibu Waziri wa Malisili na Utalii, Mhe. Japhet Hasunga (kushoto) akisalimiana na Katibu Mteule wa Tughe Tawi la Wizara ya Maliasili na Utalii, William Mwita muda alipowasili kufunga mkutano huo wa baraza. Katikati anayemtambulisha kwake ni Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Maj. Gen. Gaudence Milanzi.
 Naibu Waziri wa Malisili na Utalii, Mhe. Japhet Hasunga (kulia) akiteta jambo na Katibu Mkuu Wizara wizara hiyo, Utalii, Maj. Gen. Gaudence Milanzi muda mfupi kabla ya kufunga mkutano huo wa baraza la wafanyakazi wa wizara hiyo.
Naibu Waziri wa Malisili na Utalii, Mhe. Japhet Hasunga (kulia) akizungumza na watumishi wa wizara hiyo wakatika akifunga mkutano huo wa baraza la wafanyakazi wa wizara hiyo.
 Baadhi ya Wakurugenzi na Wakuu wa Vitengo wa Wizara hiyo walioshiriki baraza hilo.
 Baadhi ya watumishi wa Wizara na wajumbe wa baraza hilo.

Wednesday, March 28, 2018

DK. KIGWANGALLA APOKEA WAWEKEZAJI KUTOKA CHINA WANAOTAKA KUWEKEZA KATIKA SEKTA YA UTALII

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akiwa kwenye picha ya pamoja na wawekezaji wa Kampuni ya Kimataifa ya Tibet Dexin Financia Leasing kutoka nchini China ofisini kwake mjini Dodoma jana wakati kampuni hiyo ilipowasilisha mpango wake wa kuwekeza apa nchini katika ujenzi wa  mahoteli na huduma za utalii zenye ladha na mandhari ya kichina.

Na Hamza Temba - WMU-Dodoma
...........................................................................
Kufuatia jitihada mbalimbali zinazofanywa na Serikali kutafuta wawekezaji wa Kimataifa kwa ajili ya kuwekeza katika sekta utalii hapa nchini, Kampuni ya Kimataifa ya Tibet Dexin Financia Leasing kutoka nchini China imejitokeza kwa lengo la kuwekeza katika utoaji wa huduma za kitalii zenye ladha na mandhari ya Kichina.

Mwenyekiti wa Kampuni hiyo aliyejitambulisha kwa jina moja la Tony, amesema kampuni hiyo imepanga kujenga hoteli za kitalii za kichina katika mji wa Karatu jijini Arusha na Serengeti mkoani Mara.

Akizungumza na Waziri wa Maliasil na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla ofisini kwake mjini hapa jana kwa ajili ya kutambulisha mradi huo, Tony alisema mradi huo ni mahsusi kwa ajili ya kutoa huduma kwa watalii wa China wanaotembelea Tanzania.

Alisema kupitia mradi huo jumla ya magari 500 ya safari  za utalii yatanunuliwa (Safari Cars) kwa ajili ya kutoa huduma kwa watalii hao wakati wa kutembelea maeneo ya vivutio hapa nchini.

Pamoja na magari hayo alisema kampuni hiyo pia imepanga kuanzisha safari za moja kwa moja za ndege kutoka China hadi Tanzania ili kupunguza muda wa usafiri na gharama.

"Kupitia mradi huu, tunategemea kuhudumia watalii 200,000 kwa mwaka kutoka nchini China na kutengeneza ajira zaidi ya 200 kwa Watanzania" alisema Tony.

Alisema kwa sasa ni watalii 35,000 tu kutoka China wanaotembelea Tanzania kwa mwaka, na kwamba kupitia mradi huo idadi hiyo inatarajiwa kuongezeka.

Naye Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla alisema mradi huo umekuja wakati muafaka  wakati huu Serikali kupitia Wizara yake imeshaweka mikakati mahususi ya kupanua wigo wa soko la utalii nchini China.

Alisema miongoni mwa mikakati hiyo inayolenga kuvutia watalii zaidi ya 200,000 kwa mwaka katika kipindi cha muda mfupi wa miaka mitatu, ni kuwakaribisha wachina wenyewe kuja kuwekeza kwenye mahoteli na huduma zenye ladha na mandhari ya kikwao. Mataifa mengine ni Israel, Urusi na Oman.

Alisema kwa sasa ni idadi ndogo tu ya watalii wa China wanaotembelea Tanzania ukilinganisha na ukubwa wa soko la nchi hiyo.

Aliahidi kuwapa ushirikiano wawekezaji hao ikiwa ni pamoja na kuwapa maeneo kwa ajili ujenzi wa hoteli hizo za kitalii ndani ya maeneo ya hifadhi ili kuwezesha ongezeko la watalii kutoka nchini humo.

"Kwa yale maeneo mtakayohitaji ambayo yapo nje na maeneo yetu ya hifadhi tunayoyasimamia, tutawasiliana na mamlaka husika ili muweze kuapatiwa maeneo ya kuanzisha uwekezaji huo muhimu kwa taifa" alisema Dk. Kigwangalla.

Aliwataka pia wawekezaji hao kupitia taratibu zote za kuwekeza hapa nchini ikiwa ni pamoja na kujisajili katika Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), Kusajili kampuni ya utalii hapa nchini na kuwasilisha andiko la mradi na namna ya utekelezaji wake.
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akizungumza na wawekezaji wa Kampuni ya Kimataifa ya Tibet Dexin Financia Leasing kutoka nchini China ofisini kwake mjini Dodoma jana wakati kampuni hiyo ilipowasilisha mpango wake wa kuwekeza apa nchini katika ujenzi wa  mahoteli na huduma za utalii zenye ladha na mandhari ya kichina.
 Wawekezaji wa Kampuni ya Kimataifa ya Tibet Dexin Financia Leasing kutoka nchini China wakiwa kwenye mazungumzo na Waziri Kigwangalla ofisini kwake mjini Dodoma.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akimkabidhi flash yenye picha za wanyamapori wa Tanzania Mwenyekiti wa Kampuni ya Kimataifa ya Tibet Dexin Financia Leasing, aliyefahamika kwa jina moja la Tony kutoka nchini China ofisini kwake mjini Dodoma jana wakati kampuni hiyo ilipowasilisha mpango wake wa kuwekeza hapa nchini katika ujenzi wa  mahoteli na huduma za utalii zenye ladha na mandhari ya kichina.
 Waziri Kigwangalla akiendelea na mazungumzo na wakezaji hao.
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akizungumza na wawekezaji wa Kampuni ya Kimataifa ya Tibet Dexin Financia Leasing kutoka nchini China ofisini kwake mjini Dodoma jana wakati kampuni hiyo ilipowasilisha mpango wake wa kuwekeza apa nchini katika ujenzi wa  mahoteli na huduma za utalii zenye ladha na mandhari ya kichina.
   Mazungumzo yakiwa yanaendelea.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akiagana na wawekezaji wa Kampuni ya Kimataifa ya Tibet Dexin Financia Leasing kutoka nchini China ofisini kwake mjini Dodoma jana baada ya kampuni hiyo kuwasilisha mpango wake wa kuwekeza apa nchini katika ujenzi wa  mahoteli na huduma za utalii zenye ladha na mandhari ya kichina.