slider gif

slider gif

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

Wednesday, April 18, 2018

UJANGILI NCHINI WAPUNGUA KWA ZAIDI YA ASILIMIA 50 - DK. KIGWANGALLA

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akizungumza na balozi wa Uingereza hapa nchini, Sarah Cooke ofisini kwake mjini Dodoma jana ambapo walijadili mambo mbalimbali ya kuimarisha ushirikiano katika sekta ya uhifadhi na maendeleo ya utalii.

Na Hamza Temba-Dodoma
..................................................................
Serikali imefanikiwa kudhibiti vitendo vya ujangili hapa nchini kwa zaidi ya asilimia 50.

Hayo yameelezwa jana na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla wakati akizungumza na Balozi wa Uingereza hapa nchini, Sarah Cooke ofisini kwake mjini Dodoma.

Mazungumzo hayo yalilenga kujadili mambo mbalimbali ikiwemo kuimarisha ushirikiano baina ya nchi hizo mbili katika sekta ya uhifadhi na maendeleo ya utalii.

Dk. Kigwangalla alisema katika kipindi cha miezi sita iliyopita hakuna mauaji mapya ya wanyamapori yaliyoripotiwa na kwamba nyara zinazokamatwa hivi sasa ikiwemo meno ya tembo na ngozi za wanyamapori ni masalia ya zamani.

Amesema mafanikio hayo yametokana na juhudi mbalimbali zinazofanywa na Serikali kudhibiti vitendo vya ujangili ikiwemo doria za mara kwa mara za kiitelijensia ambazo zimekuwa zikishirikisha vyombo mbalimbali vya ulinzi na usalama pamoja na raia wema. 

Alisema Serikali itaendelea kudhibiti vitendo hivyo kwa kuimarisha ulinzi katika maeneo ya hifadhi nchini ikiwa ni pamoja na kuanzisha jeshi maalum la usimamizi wa Misitu na Wanyamapori, Sheria ya wanyamapori na za taasisi za uhifadhi zimeanza kufanyiwa marekebisho kuwezesha mabadiliko hayo.

Katika hatua nyingine Dk. Kigwangalla amemueleza balozi Cooke kuwa, Serikali kupitia Wizara yake inaendelea kuimarisha  vivutio vya utalii hapa nchini kwa kupanua jeografia ya maeneo ya utalii sambamba na kuongeza vivutio ili kuongeza idadi ya watalii na mapato.

Amesema Serikali itajenga makumbusho ya Marais Wastaafu wa Tanzania mjini Dodoma pamoja kuanzisha makumbusho ya meno ya tembo katika miji ya Dar es Salaam, Arusha, Iringa na Dodoma.

Sambamba na hayo amesema Serikali itaanzisha mwezi maalum wa maadhimisho ya urithi wa Mtanzania ambao utafanyika mwezi Septemba kila mwaka pamoja na kuendeleza utalii wa mikutano.

Amesema Serikali pia itaanzisha Mamlaka ya Usimamizi na Uendelezaji wa Fukwe nchini ili kuimarisha utalii wa fukwe pamoja na kutambua barabara iliyokuwa ikitumika katika biashara ya utumwa wakati wa ukoloni ili iweze kutumika kiutalii.

Akizungumzia migogoro ya mipaka iliyopo baina ya wananchi na maeneo ya hifadhi, Dk. Kigwangalla alisema Serikali itatatua migogoro hiyo kwa kushirikisha wananchi sambamba na kuwasaidia kutatua changamoto za msingi ambazo ni kuimarisha maeneo ya malisho ya mifugo, upatikanaji wa maji kwa ajili ya wananchi na mifugo, mpango bora wa matumizi ya ardhi na uendelezaji wa kilimo na ufugaji.

Kwa upande wake balozi Cooke alisema nchi yake itaendelea kuimarisha ushirikiano inaoutoa kwa Serikali ya Tanzania katika kudhibiti mtandao wa uhalifu wa madawa ya kulevya, rushwa na ujangili.

Alisema kwa sasa watalii zaidi ya 75,000 wa Uingereza hutembelea Tanzania kila mwaka na wengine wamewekeza katika sekta utalii hapa nchini, hivyo akaiomba Serikali kurekebisha baadhi ya changamoto chache zilizopo katika sekta hiyo kwenye mtiririko wa kodi. 
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akizungumza na balozi wa Uingereza hapa nchini, Sarah Cooke ofisini kwake mjini Dodoma jana ambapo walijadili mambo mbalimbali ya kuimarisha ushirikiano katika sekta ya uhifadhi na maendeleo ya utalii.
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla.
 Balozi wa Uingereza hapa nchini, Sarah Cooke.
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akiaga na balozi wa Uingereza hapa nchini, Sarah Cooke ofisini kwake mjini Dodoma jana baada ya mazungumzo yaliyolenga walijadili mambo mbalimbali ya kuimarisha ushirikiano katika sekta ya uhifadhi na maendeleo ya utalii.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akiagana na msafara wa balozi wa Uingereza hapa nchini, Sarah Cooke ofisini kwake mjini Dodoma jana ambapo walijadili mambo mbalimbali ya kuimarisha ushirikiano katika sekta ya uhifadhi na maendeleo ya utalii.

Monday, April 16, 2018

MAAFISA WANYAMAPORI WATAKIWA KUTOA ELIMU KWA WANANCHI WANAOZUNGUKA MAENEO YA HIFADHI - NAIBU WAZIRI HASUNGA

 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe.Japhet Ngailonga Hasunga (wa pili kulia) akimsikiliza Kaimu Mkurugenzi – Usimamizi wa Rasilimali za Wanyamapori wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) Bw. David Kanyata alipokuwa akitoa maelekezo kwa Maafisa Hifadhi wa wanyamapori wa pori la la akiba la Mkungunero alipofanya ziara katika pori hilo jana Wilayani Kondoa.
 Maafisa hifadhi wa wanyamapori wa pori la akiba la Mkungunero wakimsikiliza Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe.Japhet Ngailonga Hasunga (hayupo pichani) wakati akitoa maelekezo ya namna bora ya usimamizi wa hifadhi za wanyamapori alipofanya ziara katika pori hilo jana Wilayani Kondoa.
 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe.Japhet Ngailonga Hasunga (wa pili kulia) akimsikiliza Kaimu Mkurugenzi – Usimamizi wa Rasilimali za Wanyamapori wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) Bw. David Kanyata alipokuwa akimfafanulia jambo wakati wa kikao na  Maafisa Hifadhi wa wanyamapori wa pori la akiba la Mkungunero alipofanya ziara ya kutatua migogoro kati ya wafugaji na mamlaka ya hifadhi ya pori hilo jana Wilayani Kondoa. Wakwanza kulia kwake ni Meneja wa pori la akiba la Mkungunero Bw. Emmanuel M. Birasso na Meneja wa pori la akiba la Swaga Swaga Bw. Alfred Choya.
 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe.Japhet Ngailonga Hasunga (kushoto) akitoa maelekezo kwa  Kaimu Mkurugenzi  – Usimamizi wa Rasilimali za Wanyamapori wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) Bw. David Kanyata wakati wa kikao na  Maafisa Hifadhi wa wanyamapori wa pori la akiba la Mkungunero alipofanya ziara ya kutatua migogoro kati ya wafugaji na mamlaka ya hifadhi ya pori hilo jana Wilayani Kondoa.
 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe.Japhet Ngailonga Hasunga (katikati) akitizama sehemu ya ng’ombe waliokamatwa na Maafisa wa wanyamapori wa pori la akiba la Mkungunero kwa kuingia katika hifadhi hiyo wakati  alipofanya ziara ya kutatua migogoro kati ya wafugaji na mamlaka ya hifadhi ya pori la Mkungunero jana Wilayani Kondoa, ambapo zaidi ya ng’ombe 250 wanashikiliwa. Kulia kwake ni Kaimu Mkurugenzi – Usimamiziwa Rasilimali za Wanyamapori wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) Bw. David Kanyata na kulia kwake ni Kaimu Kamanda wa Polisi Wilaya ya Kondoa Bw. Juma Solomon Nyamwakirya.
 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe.Japhet Ngailonga Hasunga (katikati) akimsikiliza Diwani wa Kata ya Bumbuta Bw. Bashiru Mtoro (kulia) alipofanya ziara katika hifadhi ya pori la Mkungunero lililoko Wilayani Kondoa jana. Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Kondoa Bi. Sezaria Makota.
 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe.Japhet Ngailonga Hasunga (kulia) akimsikiliza Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Kondoa Bi. Hija Suru (kushoto) alipofanya ziara katika hifadhi ya pori la Mkungunero lililoko Wilayani Kondoa jana. Kulia kwake  ni Mkuu wa Wilaya ya Kondoa Bi. Sezaria Makota.
 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe.Japhet Ngailonga Hasunga (kulia) akimsikiliza Meneja wa pori la akiba la Mkungunero Bw. Emmanuel M. Birasso (kushoto) alipofanya ziara katika hifadhi ya pori la Mkungunero lililoko Wilayani Kondoa jana.
 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe.Japhet Ngailonga Hasunga (kushoto) akimsikiliza Bw. Yohana Bilo ambaye ng’ombe wake wanashikiliwa na Maafisa Hifadhi wa pori la Mkungunero kwa kuingia katika pori hilo alipofanya ziara ya kutatua migogoro kati ya wafugaji na hifadhi ya pori hilo jana Wilayani Kondoa.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe.Japhet Ngailonga Hasunga (kushoto) akitoa maelekezo kwa wafugaji wa vijiji vinavyozunguka pori la akiba la Mkungunero alipofanya ziara ya kutatua migogoro kati ya wafugaji na hifadhi ya pori hilo jana Wilayani Kondoa.

Na Mwandishi Maalum-Kondoa, Dodoma
......................................................
Serikali imewataka Maafisa Wanyamapori nchini kujikita zaidi katika utoaji wa elimu kwa wananchi hususani wakulima na wafugaji wanaozunguka maeneo mbalimbali ya hifadhi nchini ili kuepusha migogoro kati ya wananchi na mamlaka za hifadhi zinazosimamia maeneo hayo.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Japhet Hasunga alipotembelea Pori la Akiba la Mkungunero katika wilaya ya Kondoa mkoani Dodoma kwa ajili ya kutatua mgogoro baina ya wafugaji wa vijiji vinavyozunguka pori hilo na uongozi wa pori hilo, ambapo zaidi ya ngombe mia mbili hamsini wanashikiliwa kwa uvamizi.

“Wekezeni nguvu kubwa katika kutoa elimu kwa wananchi wanaozunguka pori hili ili wafahamu umuhimu na manufaa ya kutunza hifadhi badala ya kusubiri ng’ombe waingie kwenye hifadhi ili muwakamate, kazi ya Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori siyo kuwafilisi wananchi” amesema Naibu Waziri Hasunga

Ameeleza kuwa jukumu kubwa la maafisa hifadhi ni kuwaelimisha wananchi ili waweze kuzijua taratibu na sheria zinazosimamia hifadhi za wanyama pori hapa nchini jambo litakalo punguza kwa kiasi kikubwa migogoro.

Aidha amewataka wafanyakazi wa Pori la Akiba la Mkungunero kufanya kazi kwa bidii, ubunifu, kuzingatia maadili ya utumishi na kujiepusha na vitendo vya rushwa na unyanyasaji wa wananchi  kwani vitendo hivyo vinaichafua taswira ya Mamlaka  hiyo na kujenga sifa mbaya kwa askari wake.

“Serikali haitosita kumchukila hatua kali za kinidhamu Afisa yoyote atakaye jihusisha na vitendo vya rushwa na unyanyasaji, hivyo hakikisheni mnafanya kazi kwa weledi mkizingatia Sera, Sheria, Kanuni, Taratibu na Miongozo iliyopo ili kuongeza ufanisi wa Mamlaka hii” aliongeza Hasunga.

Hasunga aliwaeleza wananchi ambao mifugo yao imekamatwa ndani ya pori hilo kukutana mahakamani ili sheria ichukue mkondo wake. Alisema sheria za uhifadhi haziruhusu kuingiza na kulisha mifugo kwenye maeneo yaliyohifadhiwa.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Kondoa Bi. Sezaria Makota ameishukuru Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kusimamia kwa karibu Mamlaka ya Usimamizi wa Pori la akiba la Mkungunero.

“Ninapenda kuishukuru Wizara kwa juhudi zake za dhati za kufuatilia na kusimamia kwa karibu shughuli za pori hili, tunaomba muendelee na juhudi hizi za kutoa elimu kwa maafisa hifadhi wa wanyamapori na kutatua migogoro ya pori hili”  alisisitiza Bi. Sezaria

Akitoa maelekezo kwa maafisa hifadhi wa pori la akiba la Mkungunero, Kaimu Mkurugenzi – Usimamizi wa Rasilimali za Wanyamapori wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) Bw. David Kanyata amesema wamepokea maelekezo yote ya Naibu Waziri na watahakikisha wanayafanyia kazi kwa wakati muafaka.

“Tunaahidi kuyatekeleza kwa haraka maagizo yote ya Mhe. Naibu Waziri ili kwenda na kasi ya awamu ya tano” alifafanua Bw. Kanyata.

Meneja wa pori la akiba la Mkungunero Bw. Emmanuel M. Birasso ameeleza kuwa pori hilo lina faida kubwa kiuchumi na kijeolojia ikiwa ni pamoja na kuwa sehemu muhimu ya mazalia ya wanyamapori ambao wako hatarini kutoweka kama tembo, chui na duma.

Aliongeza kuwa, pamoja na umuhimu wa pori hilo bado kuna changamoto mbalimbali zinazoikabili mamlaka ya pori hilo kama ujangili, uvamizi wa hifadhi kwa ajili ya kilimo, ufugaji na uchimbaji madini na  migogoro ya mipaka kati ya hifadhi na vijiji vinavyozunguka hifadhi hiyo.

“Kumekuwa na changamoto kubwa ya uvamizi wa hifadhi kwa ajili ya shughuli za ufugaji ambapo mifugo 1320 na watuhumiwa 12 wamekamatwa hadi sasa  kwa makosa ya uvamizi” aliongeza Bw. Birasso.

Pori la akiba la Mkungunero lililopo Wilaya ya Kondoa mkoani Dodoma, linazungukwa na vijiji vipatavyo 11 na lina ukubwa wa kilomita za mraba 743.95.

Thursday, April 12, 2018

WAZIRI KIGWANGALLA AFUNGUA MKUTANO WA SITA WA BARAZA LA WAFANYAKAZI WA WAKALA WA HUDUMA ZA MISITU TANZANIA MJINI DODOMA LEO

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla (wa pili kulia) akishiriki kuimba wimbo wa mshikamano wa wafanyakazi wakati wa mkutano wa sita wa Baraza la Wafanyakazi wa Wakala wa Huduma za Misitu TFS uliofanyika leo mjini Dodoma. Kulia ni Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Dk. Aloyce Nzuki na Mtendaji Mkuu wa Wakala hiyo, Prof. Dos Santos Silayo (wa tatu kulia).
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akihutubia baraza la wafanyakazi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania mjini Dodoma leo.
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania, Prof. Dos Santos Silayo akihutubia baraza hilo.
Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Maliasili na Utalii, Dk. Aloyce Nzuki akihutubia baraza hilo.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla (wa pili kulia) akiwa kwenye picha ya pamoja na wafanyakazi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania waliohitimu mafunzo ya Jeshi Usu hivi karibuni wakati wa mkutano wa sita wa Baraza la Wafanyakazi wa Wakala huyo uliofanyika leo mjini Dodoma. 
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla (wa pili kulia) akiteta jambo na Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Dk. Aloyce Nzuki muda mfupi baada ya kufungua baraza la wafanyakazi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania mjini Dodoma leo. 

Wednesday, April 11, 2018

DK. KIGWANGALLA AITAKA KAMATI INAYOCHUNGUZA TUHUMA ZA MAUAJI YA TEMBO KATIKA IKOLOJIA YA RUAHA-RUNGWA KUTENDA HAKI

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk.Hamisi Kigwangalla akisalimiana na Kamanda wa Polisi Mstaafu wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova ambaye ni Mwenyekiti wa kamati inayochunguza tuhuma za mauaji ya tembo katika Ikolojia ya Rugwa-Ruaha ambazo zilitolewa hivi karibuni na kituo cha habari cha ITV LONDON cha nchini Uingereza, alipokutana na kamati hiyo leo ofisini kwake mjini Dodoma. Wengine pichani ni wajumbe wa kamati hiyo.

Na Hamza Temba-Dodoma
........................................................................
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla ameitaka kamati inayochunguza tuhuma za mauaji ya tembo katika Ikolojia ya Ruaha-Rungwa ambazo zilitolewa mwishoni mwa mwaka jana na kituo cha habari cha ITV London cha Uingereza kufanya kazi hiyo kwa uaminifu na uadilifu mkubwa bila kumuonea mtu ili ukweli ubainike na Serikali iweze kuchukua hatua stahiki.

Dkt. Kigwangalla ametoa rai hiyo leo mjini Dodoma alipokutana na wajumbe wa kamati hiyo ambayo imewasilisha taarifa za awali za kazi ilizoanza kuzifanya za kupitia taarifa mbalimbali kuhusu tuhuma hizo kabla ya kwenda kuzifanyia uchunguzi maeneo husika.

Amewataka wajumbe hao kuchunguza ukweli wa tuhuma hizo ili kubaini kama kweli kuna watumishi wa Wizara waliohusika katika mauaji hayo pamoja na tuhuma kuwa mauaji ya tembo yalikuwa ni makubwa kama ilivyoripotiwa na chombo hicho cha habari.

Dkt. Kigwangalla pia ameitaka kamati hiyo kuchunguza ukweli wa tuhuma kuwa fedha za ufadhili wa mradi wa SPANEST zilizotolewa na Shirika la Maendeleo ya Umoja wa Mataifa (UNDP) zilitumika vibaya kufadhili mauaji hayo kama ilivyoripotiwa na chombo hicho cha habari.

“Msimtafute mtu, wala msimuonee mtu, fanyeni kazi hii kwa uadilifu na uaminifu mkubwa ukweli ujulikane ili sisi kama Serikali tuweze kuchukua uamuzi unaostahili” alisema Dkt. Kigwangalla.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati hiyo ambaye ni Kamanda wa Polisi Mstaafu wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova amesema kamati yake itafanya kazi kwa uaminifu na weledi wa hali ya juu na kuleta taarifa za ukweli na mapendekezo yatakayoisaidia Serikali kufanya maamuzi sahihi kuhusu tuhuma hizo.

Mapema mwezi Januari mwaka huu, Waziri Kigwangalla na Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), Natalie Boucly wakiwa katika ofisi ndogo ya wizara hiyo jijini Dar es Salaam walikubaliana kuunda kamati ya pamoja kuchunguza tuhuma hizo.

Kamati hiyo iliyoundwa mapema mwezi januari mwaka huu inajumuisha wajumbe sita wakiwemo wawili kutoka Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) na wengine wanne kutoka Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk.Hamisi Kigwangalla akisalimiana na Ndugu Robert Mande ambaye ni mjumbe wa Kamati hiyo kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii.Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk.Hamisi Kigwangalla akisalimiana na Bi. Getrude Lyatuu ambaye ni mjumbe wa Kamati hiyo kutoka Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP).Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk.Hamisi Kigwangalla akisalimiana na wajumbe wa kamati inayochunguza tuhuma za mauaji ya tembo katika Ikolojia ya Ruaha-Rungwa ambazo zilitolewa hivi karibuni na kituo cha habari cha ITV LONDON cha nchini Uingereza, alipokutana na kamati hiyo leo ofisini kwake mjini Dodoma.

Monday, April 9, 2018

JENGO LA MAMLAKA YA HIFADHI YA NGORONGORO KUWA KIVUTIO CHA KIHISTORIA CHA UTOAJI WA HUDUMA ZA UTALII JIJINI ARUSHA



Na Hamza Temba - WMU
........................................................
JENGO la kitega uchumi la Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro jijini Arusha ambalo ujenzi wake unatarajiwa kukamilika mwezi juni mwaka huu litakuwa kivutio cha kihistoria cha utoaji wa huduma za utalii hapa nchini.

Hayo yameelezwa jana na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla muda mfupi baada ya kukagua jengo hilo ambalo linasemekana kuwa refu kuliko majengo yote jijini Arusha likiwa na jumla ya ghorofa 18.

Alisema jengo hilo ambalo linatizamana na Round About ya AICC katikati ya jiji hilo, limekusudiwa kuwa Kituo Kimoja (One Stop Centre) cha shughuli zote za utoaji wa huduma za utalii jijini humo kuanzia uwekezaji, utangazaji na menejimenti kwa ujumla.

Alisema jengo hilo litatoa fursa kwa wadau mbalimbali wanaotoa huduma za utalii kuweka ofisi zao ikiwemo mabenki, watoa huduma za usafiri, mashirika ya ndege, mawakala wa safari za utalii na huduma, maduka ya bidhaa za utalii na mahoteli.

"Tutapamba pia jengo hili na" live screen" (Mabango ya Video Mubashara) za vivutio, hivyo wanyama wakiwa wanapita huko porini watakuwa wanaonekana "LIVE" (Mubashara) kwenye jengo hili kupitia LED Screen ambazo zitakuwa zimezunguka jengo hili" alisema Dk. Kigwangalla.

Alisema huduma nyingine zitakazotolewa katika Jengo hilo ni pamoja na zile za kuangalia jiji la Arusha kupitia darubini, huduma za burudani ikiwemo kumbi za starehe na migahawa.

Kwa upande wake Mkandarasi wa jengo hilo, Mhandisi Bismas Meela wa Kampuni ya Inter-Consult limited alisema ujenzi wa jengo hilo ambalo ulianza mwezi Novemba, 2013 unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi juni mwaka huu.

Alisema jengo hilo ambalo lina uwezo wa kupaki magari 67 kwa wakati mmoja katika ghorofa za chini linagharimu shilingi za Kitanzania bilioni 45.

Katika ziara hiyo ya siku moja ya ukaguzi wa jengo hilo, Dk. Kigwangalla aliongozwa na Mhifadhi Mkuu wa Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro, Dk. Fredy Manongi na Naibu Mhifadhi wa Huduma za Uendeshaji wa Mamlaka hiyo, Asangye Bangu. 
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla (wa pili kushoto) akipata maelezo kutoka kwa Naibu Mhifadhi wa Huduma za Uendeshaji wa Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro, Asangye Bangu kuhusu jengo la kitega uchumi la mamlaka hiyo lililopo katikati ya Jiji la Arusha ambalo limekusudiwa kuwa Kituo Kimoja cha shughuli zote za utoaji wa huduma za utalii jijini humo kuanzia uwekezaji, utangazaji na menejimenti kwa ujumla. Kulia ni Mhifadhi Mkuu wa Mamlaka hiyo, Dk. Fredy Manongi.
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akiangalia mandhari ya Jiji la Arusha akiwa juu ya Jengo la kitega uchumi la Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro. Kutoka kulia ni Naibu Mhifadhi wa Huduma za Uendeshaji wa Mamlaka hiyo, Asangye Bangu na  Mhifadhi Mkuu wa Mamlaka hiyo, Dk. Fredy Manongi. 
Dk. Kigwangalla akiendelea kupata maelezo kuhusu jengo hilo kutoka kwa Naibu Mhifadhi wa Huduma za Uendeshaji wa mamlaka hiyo, Asangye Bangu. 

 Dk. Kigwangalla na msafara wake wakiangalia umbo la uso wa simba uliotengengenezwa katika moja lango la kuingilia kwenye lift ndani ya jengo hilo. Milango yote ya kuingilia kwenye lift ndani ya jengo hilo itapambwa kwa taswira mbalimbali za wanyamapori.
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akishuka kwenye ngazi maalum zinazotumia nishati ya umeme ndani ya Jengo hilo. Kulia ni Naibu Mhifadhi wa Huduma za Uendeshaji wa Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro, Asangye Bangu na nyuma yake ni Mhifadhi Mkuu wa Mamlaka hiyo, Dk. Fredy Manongi. \
Waziri Kigwangalla akikagua kabati la kuhifadhia vitu katika moja ya Hotel Aprtment ndani ya jengo hilo. Kulia ni Naibu Mhifadhi wa Huduma za Uendeshaji wa Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro, Asangye Bangu.
Muonekano wa jengo hilo kutokea barabara ya Makongoro Jijini Arusha.

Friday, April 6, 2018

AGIZO ALILOTOA WAZIRI KIGWANGALLA WILAYANI KISHAPU WAKATI WA KILELE CHA MAADHIMISHO YA UPANDAJI MITI KITAIFA



WAZIRI KIGWANGALLA AAGIZA KILA KIJIJI KUTENGA ENEO LA UHIFADHI WA MISITU, ATOA SIKU 7 KWA TFS KUWASILISHA MPANGO WA UVUNAJI

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga,Zainab Telack na Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri wakipanda mti wa kumbukumbu wakati wa kilele cha kuadhimisha siku ya upandaji miti kitaifa iliyofanyika jana katika kijiji cha Mhunze wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga.

Na Hamza Temba, WMU, Kishapu, Shinyanga
.......................................................................................
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla amewaagiza Wakuu wa Mikoa nchini kuhakikisha Halmashauri zote nchini zinatenga maeneo katika kila kijiji kwa ajili ya uhifadhi wa misitu ikiwa ni pamoja na vijiji hivyo kuunda kanuni na taratibu zao wenyewe za kusimamia maeneo hayo. 

Ametoa agizo hilo jana katika kijiji cha Mhunze wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga wakati wa kuhitimisha kilele cha Maadhimisho ya Upandaji Miti Kitaifa yaliyofanyika mkoani humo kuanzia Aprili 03 mwaka huu.

Katika kufanikisha zoezi hilo ameuagiza uongozi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kuchagua mikoa 10 ya kuanza utekelezaji wa agizo hilo ikiwemo mikoa ya Shinyanga na Tabora ambayo inakabiliwa na changamoto kubwa ya uharibifu wa misitu.

Ameugiza pia we uongozi huo wa TFS kuweka mpango wa uhifadhi wa misitu ya asili katika maeneo hayo kwa kushirikiana na vijiji kupanga maeneo yanayostahili kuhifadhiwa sambamba na kuwapa elimu ya umuhimu wa uhifadhi wa maeneo hayo.

Wakati huo huo Dk. Kigwangalla ametoa siku saba kwa uongozi huo wa Wakala wa Huduma za Misitu kuwasilisha kwake mpango wa tathmini ya uvunaji wa mazao ya misitu wa nchi nzima kwa kuzingatia kiasi cha rasilimali misitu kilichopo na kiwango halisi kitakachotakiwa kuvunwa ambacho hakitazidi robo ya rasilimali iliyopo.

"Hatuwezi kuendelea tu kutoa vibali vya kuvuna misitu hatujui tunavuna wapi, tuna rasilimali kiasi gani, wavune kiasi gani, hapana, mnitengenezee mpango laa sivyo nitasitisha uvunaji, nikisema nasitisha uvunaji nitapeleka waraka kwa Wakuu wa Mikoa, na nina uhakika kwa nguvu walinayo hawashindwi kuzuia uvunaji. 

"Kwahiyo TFS nawapa siku saba mniletee mpango wa tathmini ya namna ambavyo tuna rasilimali kwenye kila mkoa, tujue mkoa flani una miti cubic mita kadhaa ya mbao kadhaa, ya kuni kadhaa, ya mkaa kadhaa na kwa mwaka huu tutaruhusu wavune kwenye msitu fulani  kiasi kadhaa, twende kisayansi, sio Meneja wa TFS anakaa Wilayani anatoa vibali watu wanaenda kuvuna,".

Dk. Kigwangalla amesema  takwimu za uharibifu wa misitu hapa nchini zinatisha jambo ambalo likiachwa liendelee bila kuchukua hatua nchi itageuka kuwa jangwa.

"Kwa mwaka tunakata miti kwa mahitaji mbalimbali kati ya ekari 800,000 na 1,200,000.
Ili kurejesha walau nusu ya miti tunayokata kwa mwaka tunahitaji kupanda miti 3,000,000 kwa mwaka mfululizo kwa miaka 17 ili kufidia kiasi cha uharibifu tunachofanya kwa nusu mwaka" alisema Dk. Kigwangalla.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Misitu na Nyuki wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dk. Ezekiel Mwakalukwa ambaye alimuwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara hiyo alisema kumekuwepo na jitihada za kuandaa programu kubwa za kitaifa za uhifadhi wa mazingira katika maeneo mahususi yaliyoonekana kuzidiwa na tatizo la uharibifu wa mazingira. 

Alitaja Programu hizo kuwa ni Hifadhi Ardhi Dodoma (HADO), Hifadhi Ardhi Shinyanga (HASHI), na Hifadhi Mazingira Iringa (HIMA).

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack alisema mkoa wake kwa kushirikiana na uongozi wa mkoa wa Tabora umeanza kuchukua hatua za kurejesha uoto wa asili katika maeneo yao ikiwemo kuanzisha utaratibu wa kugawa miche ya miti kwa kila kaya pamoja na kuimarisha kamati za uhifadhi wa mazingira.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Taboba, Aggrey Mwanri alisema ushirikiano huo ni muhimu kwani utawezesha kukabiliana na changamoto zilizopo katika mikoa hiyo kwa kuweka mikakati ya pamoja wa kudhibiti vitendo vya uharibifu wa mazingira kwa kuzingatia sheria, taratibu na miongozo iliyopo.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga,Zainab Telack na Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri wakipanda mti wa kumbukumbu wakati wa kilele cha kuadhimisha siku ya upandaji miti kitaifa iliyofanyika jana katika kijiji cha Mhunze wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akiwahutubia wananchi wakati wa kuhitimisha kilele cha Maadhimisho ya Upandaji Miti Kitaifa yaliyofanyika kijiji cha Mhunze wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga jana.
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga,Zainab Telack na Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri wakiteta jambo wakati wa kilele cha kuadhimisha siku ya upandaji miti kitaifa iliyofanyika jana katika kijiji cha Mhunze wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga.
 Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga,Zainab Telack akiwahutubia wananchi wakati wa maadhimisho hayo.
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga,Zainab Telack na Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri wakiwasalimu wananchi wakati wa kilele cha kuadhimisha siku ya upandaji miti kitaifa iliyofanyika jana katika kijiji cha Mhunze wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga.
  Mkurugenzi wa Idara ya Misitu na Nyuki wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dk. Ezekiel Mwakalukwa ambaye alimuwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara hiyo akitoa maelezo kuhusu maadhimisho hayo.
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack na Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri wakielekea eneo la tukio la kupanda miti wakati wa kilele cha kuadhimisha siku ya upandaji miti kitaifa iliyofanyika jana katika kijiji cha Mhunze wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akishiriki kucheza ngoma wakati wa maadhimisho hayo.