slider gif

slider gif

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

Wednesday, December 21, 2016

SERIKALI YATOA UFAFANUZI WA KUFUNGIA BIASHARA YA USAFIRISHAJI WANYAMAHAI NJE YA NCHI.



NA HAMZA TEMBA - WMU
........................................................................

Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii imetoa ufafanuzi wa uamuzi wake wa kuzuia biashara ya usafirishaji wa wanyamahai nje ya nchi kwa kipindi cha miaka mitatu mfululizo na kusema kuwa uamuzi huo ulitolewa kwa lengo la kupanga vizuri biashara hiyo kwa faida ya serikali na wafanyabiashara wenyewe.

Ufafanuzi huo umetolewa jana na Waziri wa Wizara hiyo, Prof. Jumanne Maghembe katika kikao alichokiitisha wizarani hapo na wafanyabiashara wa wanyamahai wa makundi ya wadudu, vyura, mijusi, ndege, nyani na tumbili ambao walitaka kupata ufafanuzi wa hatima ya biashara yao kutoka serikalini.

Katika risala iliyosomwa na kiongozi wa wafanyabiashara hao, Adam Rashid Warioba kwa Waziri Maghembe, aliiomba Serikali kutoa ufafanuzi wa hatma ya biashara yao iliyofungiwa ambayo imekuwa tegemeo pekee katika kuendesha maisha yao huku wakitaka kujua hatma ya wanyamahai waliohifadhiwa na gharama zao walizolipia Serikalini.

Akitoa ufafanuzi wa uamuzi wa Serikali kufungia biashara hiyo kwa wafanyabiashara hao, Prof. Maghembe amesema wanyamahai wengi kutoka nchini Tanzania wamekuwa wakisafirishwa nje ya nchi bila ya kufuata utaratibu maalum ikiwemo vibali vya kukamata na kuwasafirisha wanyama hao jambo ambalo limekuwa likiikosesha serikali mapato mengi.

“Wapo kati yenu ambao walikuwa wanasafirisha wanyamahai kinyume cha sheria, bila vibali vyovyote, na wanyama wa Tanzania walikuwa wakimatwa kwenye bandari na viwanja vya ndege, ambao wanasafirishwa kinyume cha sheria, wengi tu, na ndio maana Serikali ikasema hii biashara tusimamae kwanza tuwekwe utaratibu ambao kila mtu ataufuata, na ambao hautaweza kututia aibu huko nje”, alisema.

Alisema sababu nyingine iliyopelekea serikali kufunga biashara hiyo kwa muda ni bei ndogo inayouzwa wanyama hao nje ya nchi ambayo haiwanufaishi wafanyabiashara na Serikali ukilinganisha na thamani yake kwa kile wanachoenda kufanyiwa, alitolea mfano tumbili ambao hufanyiwa utafiti wa madawa mbali mbali na baadae kuuzwa mabilioni ya fedha huku tumbili huyo akiuzwa kwa dola 25 tu.

“Nimefurahi yule bwana aliyesema tumbili mmoja ni dola 25, lakini akasema hao ndio wanafanya medical research (utafiti wa madawa) yote duniani, sasa sisi tunapata dola 25 na wenzetu wanafanya research (utafiti) wanatuuzia madawa yote billions of dollars (mabilioni ya dola za kimarekani), tuweke utaratibu na ninyi mtakapokuwa mnafanya hii biashara mpate sio lazima serikali ndio lazma ipate, mpate kilicho sawa na thamani ya wanyama mnaowauza”, alisema Prof. Maghembe.

Aliwahakikishia wafanyabiashara hao kuwa Serikali ya awamu ya tano ni sikivu hivyo kuahidi kushuulikia changamoto walizoziwasilisha hadi kufikia Januari 10, mwakani (2017), aliwaeleza kuwa hatma ya wanyamahai ambao wamewahifadhi pamoja gharama za vibali walizowalipia serikalini zitashuulikiwa.

“Ambacho ninaweza kuwaambia hapa leo, kwamba tumepata hii taarifa, tunayo ile idadi ambayo imepitiwa na wataalamu huko kwenye mazizi, tunazo zile permit (vibali) za serikali ambazo mmepewa na leseni, vyote vile mlivyonavyo na sisi tunavyo, tutavipitia vyooote kabisa, alafu tutaona ni namna gani tutawainua kwa kuwafuta jasho”, alisema.

Aliongeza kuwa “Tutaangalia kila mfanyabiashara ameilipa nini serikali, kwa wanyama hawa ambao wapo, ambao katazo lilipofanywa walikuwa nao kwenye mazizi yao na wanyama hao tunawafanyia tathmini tukishakamilisha tutaamua sasa wanyama hao wanapelekwa wapi, na maeneo yenyewe ni machache tu, ama kwenye mazoo, ili waweze kutunzwa na kuendelezwa kwa vile ni vigumu kuwarudisha tena maporini.

 “Na kutokana na vibali na risiti mbalimbali ambazo wameilipa serikali katika kuwapata hao wanyama basi tutaviangalia na kuangalia utaratibu wa kuwarudishia wale wafanyabiashara hela zao”.

Akizungumzia lalamiko la wafanyabiashara hao kuwa wao wamezuiliwa kufanya biashara hiyo huku mfanyabiashara mmoja kutoka nje akiruhusiwa kufanya biashara hiyo kwa tangazo la serikali, Prof. Maghembe anasema “Na hilo tangazo mnalosema lina mtu amebebwa hamna ruhusa ya mtu kubebwa hapa, na mtu atayempa huyo mtu kibali mnafahamu kitakachotokea, hakuna ruhusu, ndivyo serikali ilivyosema”.

Mei 26, mwaka huu, akifanya majumuisho ya hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya wizara yake kwa mwaka 2016/17, Waziri wa Maliasili na Utalii, Prof. Jumanne Maghembe, alitangaza kuwa ni marufuku kusafirisha wanyamahai wote nje ya nchi kwa miaka mitatu mfululizo.


“Kuanzia sasa (saa moja na dakika tano usiku) kwa miaka mitatu serikali imepiga marufuku usafirishaji wa wanyamahai wote kwenda nje ya nchi, hata chawa wa Tanzania hawataruhusiwa kusafirishwa nje, Na katika kipindi hiki cha miaka mitatu, idara ya wanyamapori itafanya kazi ya kuishauri serikali namna gani biashara hiyo itakavyoendeshwa”, alisema Prof. Maghembe.

No comments:

Post a Comment