slider gif

slider gif

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

Friday, January 12, 2018

LAZIMA TUTAFUTE NAMNA MPYA YA KUJITAMBULISHA NDANI YA NCHI NA NJE YA NCHI-DK. HAMISI KIGWANGALLA




Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Khamis Kigwangalla (wa pili kushoto) akifuatilia mkutano wa uzinduzi wa Kamati ya Kitaifa ya kuandaa Utambulisho wa Utalii wa Tanzania katika hafla iliyofanyika kwenye ukumbi wa Chuo cha Taifa cha Utalii Jijini Dar es Salaam tarehe 11/01/2018, Kutoka kushoto ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt. Aloyce Nzuki, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Bibi. Devotha Mdachi na Mwenyekiti Mwenza wa kamati hiyo Richard Rugimbana.
Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Khamis Kigwangalla akisisistiza jambo wakati wa hafla ya uzinduzi wa Kamati ya Kitaifa ya Kuandaa Utambulisho wa Utalii wa Tanzania katika hafla iliyofanyika kwenye ukumbi wa Chuo cha Taifa cha Utalii Jijini Dar es Salaam. Kamati hiyo yenye wajumbe 21 imeundwa na Mhe. Waziri kwa lengo la kupitia na kubuni mkakati mbadala wa namna ya kutangaza utalii wa Tanzania ndani na nje ya nchi.
 Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Utambulisho wa Utalii wa Tanzania Bibi. Devotha Mdachi akielezea jambo mbele ya wajumbe wa kamati hiyo (hawapo pichani) mara baada ya kuzinduliwa rasmi kwa Kamati hiyo leo Jijini Dar es Salaam. 
Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Khamis Kigwangalla (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Kamati ya Kitaifa ya Utambulisho wa Utalii wa Tanzania lmara baada ya uzinduzi wa kamati hiyo leo Jijini Dar es Salaam. Kamati hiyo yenye wajumbe 21 imeundwa na Mhe. Waziri kwa lengo la kupitia na kubuni mkakati mbadala wa namna ya kutangaza utalii wa Tanzania ndani na nje ya nchi.
BR3
Baadhi ya wajumbe wa Kamati ya Kitaifa ya Utambulisho wa Utalii wa Tanzania wakifuatilia hotuba ya Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Khamis Kigwangalla.

Na Mwandishi Wetu
...................................................
WAZIRI wa Maliasili na Utalii Dkt.Hamis Kigwangala amesema ipo haja ya kuwa na kauli mbiu ambayo itatumika kutangaza vivutio vyote vya utalii wa Tanzania katika mataifa mbalimbali duniani.

Amesema Tanzania imejaaliwa kuwa na maeneo mengi ya utalii lakini hayajafahamika kutokana na nguvu ndogo ya kuyatangaza kwake, hivyo kusababisha watalii wengi kufanya utalii katika maeneo machache ya utalii ukiwamo Mlima Kilimanjaro.

Dk.Kigwangala ametoa kauli hiyo jijini  Dar es Salaam jana wakati anazindua Kamati ya Kuandaa Utambulisho wa Utalii Tanzania na kusema kuwa kuna vivutio vingi ambavyo sasa ipo haja kubwa ya kuendelea kuvitangaza kwa nguvu zote.

Amesema wajumbe wa kamati watakuwa na jukumu la kuweka mikakati sahihi ya kuhakikisha utalii wa Tanzania unaendelea kutangazwa kwa lengo la kuongeza watalii wa ndani na nje ya nchi.

“Tunayo maeneo mengi ya utalii lakini yanayofahamika ni machache, kuna watalii wanakuja kwa ajili ya kwenda Mlima Klimanjaro na wengine Mbuga ya Serengeti wakati yapo maeneo mengi ya utalii. Lazima tutafute namna mpya ya kujitambulisha nadni ya nchi na nje ya nchi, tutangaze utalii wetu na hii kamati itatusaidia kutuongoza,”amesema Dk.Kigwangala.

Amewataka wajumbe wa kamati hiyo kutafuta kauli mbiu ambayo itautangaza utalii wa Tanzania katika nchi mbalimbali duniani.

“Iwe kauli mbiu ambayo itatutofautisha Tanzania na nchi nyingine kwenye mambo ya utalii na lazima tuwe na kauli mbiu ya kipekee katika kuutangaza utalii wetu na vivutio vyake vyote”amesema Dk.Kigwangala.

Amefafanua kuna Hifadhi za Taifa 16 lakini zinazotambulika ni chache tu, hivyo juhudi zinahitaji zaidi kutangaza vivuto vya utalii vilivyopo.

Mwenyekiti Mwenza wa Kamati ya Kitaifa ya Utambulisho wa Utalii Tanzania Richard Lugimbana amemhakikishia Dk.Kigwangala kuwa wanatambua jukumu ambalo wamepewa na hivyo ni wajibu wao kuweka mikakati ambayo itasaidia kuutambulisha utalii wetu. 

Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Utalii Devotha Mdachi amefafanua kamati hiyo ina jumla ya wajumbe 21 ambao wengi wao ni  watalaamu wa masoko.

Ameongeza utambulisho mpya kwa ajili ya kutangaza utalii wa Tanzania utaifanya nchi kuwa katika ramani nzuri ya kutambulika kwa vivutio vyake vya utalii.

Thursday, January 11, 2018

WIZARA YA MALIASILI NA UTALII YATANGAZA RASMI VIWANGO VIPYA VYA ADA KWA MAWAKALA WA KUSAFIRISHA WATALII NCHINI

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla (kulia) na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Maj. Gen. Gaudence Milanzi (kushoto).

Na Hamza Temba-WMU-Dar es Salaam
.......................................................................

Wizara ya Maliasili na Utalii imetangaza rasmi viwango vipya vya malipo ya ada kwa Mawakala wa kusafirisha watalii nchini baada ya kukamilika kwa marekebisho ya kanuni ya ada na tozo za biashara ya utalii yaliyofanyika mwezi Desemba mwaka jana, 2017.

Taarifa iliyotolewa leo na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Maj. Gen. Gaudence Milanzi, imeeleza kuwa baada ya kukamilika kwa marekebisho hayo ya kanuni, Tangazo la Serikali namba 506 la tarehe 29 Desemba, 2017, limeweka viwango vipya vya ada kwa mawakala wa kusafirisha watalii (Tour Operators na Safari Outfitters).

Taarifa hiyo imeeleza viwango hivyo kuwa ni shilingi sawa na dola za Kimarekani 500 kwa kampuni za wazawa zenye umiliki mkubwa wa raia wa Tanzania na zinazomiliki gari 1 hadi 3.

"Shilingi sawa na dola za Kimarekani 2,000 kwa kampuni zenye gari 4 hadi 10, shilingi sawa na dola za Kimarekani 3,000 kwa kampuni zenye gari 11 hadi 50 na shilingi sawa na dola za Kimarekani 5,000 kwa kampuni zenye kumiliki gari 51 na kuendelea", imeeleza taarifa hiyo.

Kwa upande wa kampuni za kigeni zenye umiliki mkubwa wa raia wa kigeni na zinazomiliki gari 10 hadi 30 zitalipa ada ya shilingi sawa na dola za Kimarekani 5,000, kampuni zenye gari 31 hadi 50 zitalipa shilingi sawa na dola za kimarekani 7,500 na na kampuni zenye gari 51 na kuendelea zitalipa shilingi sawa na dola  za Kimarekani 10,000.

Kufuatia marekebisho hayo, muda wa kutumika kwa leseni za mwaka 2017 za Wakala wa kusafirisha watalii (Tour Operators na Safari Outfitters) umesogezwa mbele hadi tarehe 31 Januari, 2018 ili kuwezesha maandalizi ya kuingia kwenye mabadiliko ya viwango hivyo vipya.

Aidha, taarifa hiyo imeeleza kuwa  maombi ya usajili na leseni za biashara ya utalii na leseni za waongoza watalii kwa mwaka 2018  kwa wafanyabiashara wapya na wanaoendelea na biashara yanaendelea kupokelewa.

Waombaji wote wametakiwa kufuata masharti ya uombaji wa leseni hizo ikiwemo kuwasilisha nakala za hati za usajili wa magari zilizothibitishwa kisheria kwa Wakala wa kusafirisha watalii (wapya na wanaoendelea na biashara) na kivuli cha leseni ya mwaka 2017 kwa wafanyabiasbara wote. 

"Ni kosa kisheria kuwasilisha taarifa za uongo na adhabu yake ni pamoja na kufutiwa leseni", imeeleza sehemu ya taarifa hiyo.

Desemba 10 na 11 mwaka 2017, Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla alikutana na wadau wa sekta ya utalii jijini Arusha kwa lengo la kuwashirikisha katika mapendekezo ya viwango vipya vya ada kwa Wakala wa kusafirisha watalii ambavyo vilivyotolewa na Wizara yake.  Mapendekezo ya viwango hivyo yalilenga kuongeza mapato na kuwawezesha wafanyabiashara wadogo wenye gari kuanzia moja kuingia katika biashara hiyo.

Wednesday, January 10, 2018

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla azindua Kamati ya Kitaifa ya Kuandaa Mwezi Maalum wa Maadhimisho ya Urithi wa Tanzania

Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Hamisi Kigwangala akizungumza katika mkutano na  Kamati ya kitaifa ya kuandaa Mwezi maalumu wa maadhimisho ya Urithi wa Taifa la Tanzania uliofanyika leo kwenye Chuo cha Taifa cha Utalii Posta jijini Dar es salaam leo. 
Na Mwandishi Wetu-Dar es Salaam
................................................................................................
 WAZIRI wa Maliasili na Utalii Dk.Hamisi Kigwangala amezindua kamati ya kitaifa ya kuandaa Mwezi maalumu wa maadhimisho ya Urithi wa Taifa la Tanzania.
 Kamati hiyo inahusisha Wakuu wa Mikoa ambao pia ni wajumbe wateule wa Kamati ya kitaifa ya kuratibu shughuli za maandalizi ya Mwezi Maalum wa Maadhimisho ya urithi wa Tanzania.
 Akizungumza Dar es Salaam leo, wakati wa uzinduzi wa kamati hiyo, Dk.Kigwangala amesema anawapongeza  wajumbe wote wa Kamati ya Maadhimisho wa Mwezi wa Urithi wa Tanzania kwa kuteuliwa kwao kwa ajili ya shughuli hii muhimu katika kuhimiza urithi wa Tanzania kwa maendeleo ya sekta ya utalii katika Taifa letu.
Amesema sekta ya utalii imekuwa mhimili muhimu katika ukuaji wa uchumi  wa Tanzania ambapo kwa mwaka 2017 sekta ya  utalii imechangia dola za kimarekani Bilioni 2.1 takriban asilimia 25  ya  fedha za kigeni.
Amesema takwimu zinaonesha mwaka 2016 idadi ya watalii waliotembelea nchi yetu walifikia 1,284,279. Katika taarifa yake ya 6 ya maendeleo ya uchumi, inayoitwa “Unlocking the Potential of the Tourism Industry for Tanzanians” Benki ya Dunia inaonesha kuwa mapato ya utalii yatakua kila mwaka na kufikia Dola za Marekani 16 bilioni ifikapo 2025. 
“Hata hivyo, mpaka sasa sekta ya utalii Tanzania imekua ikijikita zaidi katika utalii wa wanyamapori ili kuvutia watalii ambapo takriban asilimia zaidi ya 80 ya watalii wa kimataifa wanaotembelea Tanzania bara huja kuona wanyamapori.
“Nchi yetu imejaliwa kwa kuwa na rasilimali mbalimbali za urithi wa Taifa nje ya zile za wanyamapori. Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizojaliwa kuwa na rasilimali za kipekee duniani zinazobainisha harakati za maendeleo ya binadamu kama vile chimbuko lake, teknolojia alizotumia.
”Na namna ambavyo binadamu amekuwa akitumia mazingira yake ili kumwezesha kuishi kwa zaidi ya miaka milioni tatu iliyopita. Mfano wa rasilimali hizo ni masalia ya Binadamu wa Kale (Zamadamu) walioishi Bonde la Olduvai zaidi ya miaka milioni 1.7 iliyopita na nyayo za Zamadamu aitwaye Australopithecus afarensis aliyeishi Laetol miaka milioni 3.6   iliyopita”amesema.
Pia miji ya kihistoria kama vile Bagamoyo na Kilwa, michoro ya miambani, Kondoa na mapango ya Amboni.Aidha Tanzania ikiwa na zaidi ya makabila 120 imejaliwa kuwa na anuaia za mila, desturi, vyakula, misemo, imani, mavazi, nyimbo, ngoma za aina mbali mbali na matumizi ya lugha ya Kiswahili katika kuunganisha Watazania. 
Dk.Kigwangala amesema kutokana na kuona hayo yote wizara yake imeamua kuwepo na mwezi maalumu kwa ajili ya kusheherekea Urithi wa Taifa la Tanzania.
 Amesema Urithi huo wa Taifa ni miongoni mwa vivutio vya utalii kwa kuwa ni  vielelezo vya historia,  utamaduni na ustaarabu wa jamii katika hatua mbalimbali za maisha.
Ameongeza urithi huo huonesha na kuikumbusha jamii husika chimbuko la tabia, mila na desturi ambazo inazitumia katika nyanja za uchumi, siasa, teknolojia na elimu.
“Jamii yoyote ile inatambuliwa, kuthaminiwa na kuheshimiwa kutokana na urithi wake. Kwa sababu hiyo, tuna kila sababu ya kuendeleza urithi huu tuliojaliwa na mwenyezi Mungu.
” Kwa kutambua umuhimu huo,kuuenzi, kuutangaza na kuutumia urithi wa Taifa la Tanzania kama kivutio cha utalii na kumbukumbu za Taifa, Wizara yangu imeona ni vema kukwepo na mwezi maalum wa kusherehekea Urithi wa Taifa la Tanzania (Tanzania National Heritage Month).Tumekubaliana mwezi huo utakuwa ukiadhimishwa kila ifikapo Septemba ya kila mwaka,”amesema.
Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Hamisi Kigwangala akizungumza katika mkutano na  Kamati ya kitaifa ya kuandaa Mwezi maalumu wa maadhimisho ya Urithi wa Taifa la Tanzania uliofanyika leo kwenye Chuo cha Taifa cha Utalii Posta jijini Dar es salaam leo. 
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dk. Aloyce Nzuki akizungumza katika mkutano huo.
Imani Kajula Mjumbe wa Kamati ya kitaifa ya kuandaa Mwezi maalumu wa maadhimisho ya Urithi wa Taifa la Tanzania akizungumza kwenye mkutano uliofanyika leo kwenye chuo cha Utalii cha Taifa Posta jijini Dar es salaam kushoto ni Mjumbe wa kamati hiyo ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mh. Mrisho Gambo na katikati ni Jokate Mwegelo mjumbe pia.
 Kutoka kulia ni Wajumbe wa kamati hiyo WEma Sepetu, Dkt. Sebastian Ndege, Dk. James Wakibara na Dk. Fredy Manongi na Devotha Mdachi
 Mjumbe wa kamati hiyo Ritha Paulsen akichangia mada katika mkutano huo uliofanyika kwenye chuo cha Utalii cha Taifa jijini Dar es salaam.
 Mjumbe wa Kamati hiyo Jokate Mwegelo akitoa mchango wake wa mawazo katika mkutano huo kulia ni Mjumbe Imani Kajula na kushoto ni Mjumbe wa kamati hiyo ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mh. Mrisho Gambo. 
 Picha ya pamoja kati ya Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Dk. Hamisi Kigwangalla (katikati), Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. John Mtaka (wa pili kushoto), Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. Mrisho Gambo (wa pili kulia), Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Amina Masenza (kushoto) na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dk. Aloyce Nzuki (kulia)
 Picha ya pamoja
  Picha ya pamoja kati ya Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Dk. Hamisi Kigwangalla na wajumbe wa kamati hiyo.
Baada ya kuhitimisha uzinduzi na picha ya pamoja.

Tuesday, January 9, 2018

DK. KIGWANGALLA ATEUA KAMATI YA UCHUNGUZI WA CHANGAMOTO ZA BONDE LA MTO KILOMBERO


Na Mwandishi Maalum
...........................................................................

Waziri wa Maliasili na Utalii Dk. Hamisi Kigwangalla (MB) ameteua Kamati maalum ya kuishauri Serikali hatua za kuchukua katika kutatua changamoto zinazolikabili bonde la mto Kilombero lililopo Mkoani Morogoro.

Waziri Kigwangalla amesema, Kamati hiyo aliyoiteua,  ndio itakayomshauri juu ya usimamizi wa bonde hilo ikiwemo hatua za kuchukua ili kulinda bonde hilo ambalo lina umuhimu mkubwa ikiwemo chanzo kikubwa  cha maji yanayotengeneza Stiegler’s Gorge ambako Serikali imeamua kuweka mikakati ya utekelezaji wa mradi wa kuzalisha umeme wa megawatts 2100 huku pia bonde hilo likiwa na utajiri wa kuwepo na aina zaidi ya 400 ya ndege pamoja na mnyama aina ya Puku ama Sheshe ambaye hapatiani kwengineko duniani zaidi ya Tanzania pekee.

"Hii ndio Kamati yangu, itakayonishahuri juu ya bonde ili litasimamiwa vipi. Hii ndio Kamati ambayo itanishahuri mimi na kwamaana hiyo Serikali kwa ujumla wake juu ya namna bora ya uhifadhi hususani katika eneo lile la Pori tengefu.

Hapa kuna vitu viwili vya kuzingatia: Ardhi Oevu (Ramsar site) ambalo lina eneo lake huku pia eneo la pori tengefu nalo kichukua nafasi kubwa zaidi" Amesem Waziri Dk Kigwangalla wakati wa kuteua Kamati hiyo.

Kamati hiyo inaundwa na  wajumbe mbalimbali ambao wataongozwa na Mwenyekiti wa Kamati Ndugu Andrew Napacho, Pia wajumbe ni  Brig. Gen. (Mst.) Edmund Mndolwa, Aliyekuwa Kamanda wa Polisi katika Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Kamishna Mstaafu, Suleiman Kova, Mwenyekiti Taifa wa Chama Cha wafugaji Bwana  Semkae Kilonzo (Policy Forum).

Wengine ni  Dk. Simon Mduma, Prof. Jaffar Kideghesho, Ruzika Muheto, Mkuu wa Wilaya ya Ulanga, MKuu wa Wilaya ya Kilombero na Mkuu wa Wilaya ya Malinyi.

Wengine ni Mwenyekiti Halmashauri Ulanga, M/Halmashauri Kilombero, M/Halmashauri Malinyi  na M/Halmashauri Ifakara.
Pia yupo  Mtendaji Mkuu wa KPL, Mtendaji MKuu wa Illovo, Mkuu Kikosi JKT Chita. Wengine ni  Dk. Aggrey Mlimuka, Mwakilishi kutoka mamlaka ya maji Bonde la Kilombero, Mwakilishi kutoka Wizara ya ardhi.

Wajumbe wengine ni Ndugu Innocent Kylogeris, Dk. James Wakibara, Mkurugenzi Mkuu TAWA ambaye atakuwa Katibu wa Kamati hiyo.

Hatua hiyo inafuatia Waziri Dk Kigwangalla kufanya ziara maalum kwenye bonde hilo la kilombero ambapo ameweza kushuhudia athari kubwa zaidi zilizofanywa na wavamizi wakiwemo wakulima na wafugaji ambao wameonekana kuvamia maeneo makubwa  ndani ya pori tengefu la bonde pamoja na Kwenye eneo ohevu ndani ya bonde hilo.

Friday, January 5, 2018

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII, DK. HAMISI KIGWANGALLA ATOA MAAGIZO MAZITO KWA TFS

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla (wa pilia kulia) akisalimiana na viongozi na watumishi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania TAWA, muda mfupi baada ya kuwasili makao makuu ya mamlaka hiyo mkoani Morogoro jana.

...................................................
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla ameugiza uongozi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kukabidhi eneo la Kilomita za mraba 25 kutoka kwenye Hifadhi ya Msitu wa Morogoro unaosimamiwa na wakala huyo kwa ajili ya ujenzi wa ofisi za Makao Makuu ya Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA).

Ametoa agizo hilo jana akiwa kwenye ziara ya siku mbili mkoani Morogoro ambapo alimuagiza Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Mej. Jen. Gaudence Milanzi kuzikutanisha taasisi hizo ndani ya siku saba zijazo ili kukamilisha mchakato wa kumega eneo hilo na kukabidhiwa kwa Mamlaka hiyo ili taratibu za ujenzi ziweze kuanza.

Aidha, ameuagiza uongozi huo wa TFS kuweka vigingi vya mpaka katika eneo la hifadhi hiyo ya msitu ndani ya siku 30 zijazo huku akitoa muda huo huo kwa wananchi wote waliovamia eneo hilo kuondoka mara moja kwa hiari yao wenyewe kabla ya kuondolewa kwa nguvu.

Katika hatua nyingine, Dk. Kigwangalla amemuagiza Mtendaji Mkuu wa Wakala hiyo, Prof. Dos Santos Silayo kukabidhi mbao zaidi ya 400 zilizokamatwa hivi karibuni mkoani Morogoro baada kuvunwa kinyume cha Sheria kwa uongozi wa Mkoa huo ili zisaidie kutengeneza madawati ya shule za msingi.

Pamoja na mbao hizo amemuagiza pia mtendaji huyo kukabidhi kwa uongozi wa mkoa huo magunia 350 ya mkaa yaliyokamatwa katika kituo cha Tazara yakiwa yanasafirishwa kinyume cha Sheria ili yasambazwe kwenye shule za Sekondari mkoani humo.

Dk. Kigwangalla alitoa maagizo hayo jana wakati akizungumza na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Morogoro inayoongozwa na Mkuu wa Mkoa huo, Dk. Steven Kebwe, ambapo alimuomba kusimamia zoezi hilo la ugawaji kikamilifu ili walengwa waweze kufikiwa.

Katika ziara hiyo ametembelea pia bonde la Kilombero ambalo ni chanzo kikubwa cha maji yanayotengeneza Stieglers Gorge ambapo Serikali ya awamu ya nne itajenga mradi mkubwa wa kuzalisha umeme wa megawatts 2100.
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla (wa pilia kulia) akisalimiana na viongozi na watumishi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania TAWA, muda mfupi baada ya kuwasili makao makuu ya mamlaka hiyo mkoani Morogoro jana.
Dk. Kigwangalla akizungumza na watumishi wa TAWA wakati wa ziara hiyo.

Tuesday, January 2, 2018

DK. KIGWANGALLA NA MKURUGENZI MKAZI WA UNDP KUANZISHA KIKOSI KAZI CHA KUCHUNGUZA TUHUMA ZA UJANGILI WA TEMBO KATIKA HIFADHI YA RUAHA

Na Mwandishi Wetu - Dar es Salaam
.....................................................................
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla na Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), Bi. Natalie BOUCLY wamekubaliana kuanzisha kikosi kazi cha pamoja cha kuchunguza tuhuma zilizotolewa hivi karibuni na kituo cha habari cha ITV LONDON kuhusu ujangili wa Tembo katika Hifadhi ya Taifa ya Ruaha iliyopo Mkoani Iringa.

Dk. Kigwangalla na Mkurugenzi huyo, wamefikia makubaliano hayo leo Januari 2, 2018 wakati wa mazungumzo yaliyofanyika katika ofisi ndogo ya Wizara ya Maliasili na Utalii, Mpingo House Jijini Dar es Salaam.

Aidha, Waziri Kigwangalla amemueleza Mkurugenzi huyo kuwa Wizara yake inaandaa mikakati mbalimbali ya kuongeza idadi ya watalii nchini na mapato ikiwemo kuwashirikisha wananchi kuandaa mwezi maalum wa Urithi wa Tanzania pamoja na kuimarisha mifumo ya ukusanyaji wa mapato kwa njia za kielektroniki katika vituo mbalimbali ya Utalii.

Kwa upande wake, Mkurugenzi huyo amemuahidi Waziri Kigwangalla kuendelea kumpa ushirikiano katika nyanja mbalimbali za kuendeleza Utalii nchini na uhifadhi wa misitu na wanyamapori kwa ujumla.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla (kulia) akizungumza na Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa hapa nchini (UNDP), Bi. Natalie BOUCLY katika ofisi ndogo ya Wizara hiyo, Mpingo House Jijini Dar es Salaam leo.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla (kulia) akimsikiliza Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa hapa nchini (UNDP), Bi. Natalie BOUCLY wakati wa mazungumzo yaliyofanyika leo katika ofisi ndogo ya Wizara hiyo, Mpingo House Jijini Dar es Salaam. 
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla (kulia) akiagana  na Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa hapa nchini (UNDP), Bi. Natalie BOUCLY baada ya mazungumzo yaliyofanyika katika ofisi ndogo ya Wizara hiyo, Mpingo House Jijini Dar es Salaam leo.

Taarifa kwa vyombo vya habari kuhusu ugawaji wa vitalu vya uwindaji wa kitalii kwa njia ya mnada