slider gif

slider gif

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

Monday, January 25, 2016

KATIBU MKUU WIZARA YA MALIASILI NA UTALII MAJ. GEN. GAUDENCE MILANZI AONGOZA KIKAO CHA KAMATI YA UWEZESHAJI UTALII NCHINI TFC

Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Meja Generali Gaudence Milanzi (kulia) akizungumza kwenye Mkutano wa Kamati ya Uwezeshaji Utalii (Tourism Facilitation Committee- TFC) uliofanyika hivi karibuni Mpingo House Jijini Dar es Salaam. Wapili kulia ni Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Utalii Leseni na ubora wa huduma Bw. Deogratius Mdamu.
Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Utalii, Bi. Uzeeli Kiangi (kulia) akizungumza kwenye kikao hicho.
Baadhi ya Wajumbe wa kamati ya Uwezeshaji Utalii (Tourism Facilitation Committee- TFC) ambao walikutana kujadili changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta ya Utalii nchini kwa kutoa maoni, ushauri na ufumbuzi wa changamoto ikiwa na kuchangia mikakati mbalimbali itakayowezesha kusaidia kuhamasisha Utalii wa ndani.

.....................................................................................................

Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kushirikiana na wadau wa utalii nchini, imejipanga kuhakikisha inaendelea kukuza utalii wa ndani ambao utakua na uhakika zaidi wa kuliingizia taifa mapato tofauti na hivi sasa ambapo utegemezi upo kwa watalii kutoka nje ya nchi ambapo wakati mwingine hupelekea uhaba kutokana na athari za majanga ya kimataifa.

Baadhi ya Majanga hayo yaliyoathiri Sekta ya Utalii katika kipindi cha hivi karibuni ni milipuko ya magonjwa kama Ebola, matukio ya Ugaidi nchini Kenya na kushuka kwa thamani ya Euro ya Ulaya dhidi ya Dola ya Marekani.

Akizungumza kwenye Mkutano wa Kamati ya Uwezeshaji Utalii ijulikanayo kama Tourism Facilitation Committee (TFC) uliofanyika hivi karibuni Mpingo House jijini Dar esSalaam, Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Meja. Generali. Gaudence Milanzi amesema maendeleo ya Utalii yanahitaji sana Utalii wa ndani kuimarika badala ya kudhani kuwa vivutio vya utalii vilivyopo ni kwa ajili ya wageni kutoka nchi za nje.

Meja Generali Milanzi amesema Utalii ni sekta nyeti sana katika kuliingiza Taifa pesa za kigeni lakini hata hivyo ni sekta ambayo imekuwa inaathirika kwa haraka sana pindi majanga yanapotokea nchi jirani hivyo ni lazima jamii ijengewe utamaduni wa kutembelea vivutio vya Utalii ili kuweza kujihakikishia Watalii wa ndani wanakuwa wengi.

Baadhi ya mikakati iliyopendekezwa na Wajumbe wa kamati ya Uwezeshaji Utalii (TFC) ni kuwawezesha maafisa Utalii wa Halmashauri wanatengewa bajeti ya kutosha, wanajengewa uwezo kuhusu ya vivutio vya utalii vilivyopo kwenye maeneo yao pamoja na Idara ya Utalii kufungua ofisi kila kanda ili kuweza kutimiza majukumu yake ipasavyo.

Mkakati mwingine uliopendekezwa ni kwa viwanja vya ndege vilivyopo nchini kuimarishwa ikiwa ni pamoja na nchi kuwa na ndege zake kama ilivyo kwa nchi jirani ya Kenya na Rwanda.

Awali, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Utalii, Bi. Uzeeli Kiangi alisema Mkutano wa TFC hutoa fursa ya kuibua na kujadili changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta ya Utalii hivyo Sekta Binafsi zinawajibu mkubwa wa kuhakikisha changamoto zinazoikabili sekta zinatafutiwa ufumbuzi

Aliongeza kuwa Idara ya Utalii imekuwa ikishiriki katika maonesho mbalimbali ya kitaifa lengo likiwa ni kutoa elimu kwa jamii kuhusu umuhimu wa kutembelea vivutio vya Utalii nchini.

Mdau wa Utalii, Prof Wineastor Anderson amesema sekta ya Utalii imekuwa ikikua lakini si kwa kiwango cha kuridhisha hivyo jitihada za kutangaza utalii ndani na nje nchi upewe uzito unaostahili kwa kuiwezesha Bodi ya Taifa ya Utalii kuwa na bajeti ya kutosha kujitangaza ndani na nje ya nchi.

Wakati huo huo, Mwenyekiti wa Shirikisho la vyama vya Utalii Tanzania (TCT) Bw. Richard Rugimbana, amesema Utalii wa ndani ili uweze kukua suala la elimu linahitajika kutolewa ili kuweza kuibadilisha jamii ipende kutembelea vivutio vya Utalii vya ndani ya nchi.


Kwa upande wake Kamanda wa Polisi (ACP) Ndaki anayeshughulikia dawati la Utalii (Tourism Police Unit) amewahakikishia usalama watalii wa ndani na nje ya nchi kutembelea vivutio vya Utalii bila kuwa na hofu yoyote kwa kuwa Jeshi la Polisi nchini lipo macho muda wote.

No comments:

Post a Comment