slider gif

slider gif

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

Sunday, November 26, 2017

CHUO CHA USIMAMIZI WA WANYAMAPORI-MWEKA KUANZA KUTOA MAFUNZO MAALUM KWA WAONGOZA WATALII NCHINI KUANZIA KESHO

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Japhet Hasunga (wa tatu kulia) akipata maelezo kutoka kwa Mwanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori-Mweka, Brightone Mbilinyi kuhusu mafunzo ya silaha yanavyotolewa chuoni hapo katika mahafali ya 53 ya chuo hicho yaliyofanyika jana katika wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjaro. Zaidi ya asilimia 60 ya mafunzo chuoni hapo hutolewa kwa vitendo. Wengine Pichani ni Balozi wa Nigeria nchini, Mhe. Sahabi Dada (wa pili kushoto) na Mkuu wa Chuo hicho, Prof. Jafari Kideghesho (wa nne kulia).

 Na Hamza Temba-WMU
..................................................

Katika kutimiza azma ya Serikali kuboresha huduma za ukarimu kwenye sekta ya utalii nchini, Wizara ya Maliasili na Utalii imekichagua Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori Mweka kilichopo mkoani Kilimanjaro kwa ajili kutoa mafunzo maalum kwa waongoza watalii nchini. 

Mafunzo hayo ambayo yanatarajiwa kuanza kesho (Jumatatu) chuoni hapo yatakuwa kwenye mfumo wa kujiendeleza na yamelenga kuwawezesha watoa huduma katika sekta hiyo kupata sifa za kusajiliwa na kupewa leseni ya kuendelea kutoa huduma hiyo kwa mujibu ya sheria ya utalii Na. 11 ya mwaka 2008 kifungu cha 48.

Hayo yamesemwa jana na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Japhet Hasunga katika mahafali ya 53 ya kuwatunuku vyeti wahitimu 224 wa chuo hicho katika kozi mbalimbali ikiwemo Shahada, Stashahada na Astashada kwenye Usimamizi wa Wanyamapori na Utalii.

"Katika kutambua utaalamu na uzoefu wa chuo chenu, Wizara yangu imeichagua Mweka kutoa mafunzo yatakayowawezesha waongoza watalii nchini kupata sifa ya kusajiliwa (cheti) na kupewa leseni," alisema Naibu Waziri Hasunga.

"Nimefurahi kusikia kuwa  mmeshajipanga tayari kuanza kutoa mafunzo hayo baada ya kufanya tathmini ya mahitaji ya mafunzo na kuainisha mapungufu kwenye taaluma, ujuzi na mitazamo pamoja na kuandaa mtaala wa mafunzo hayo.

"Nitoe wito kwa waongoza watalii  nchini wajisaji ili wapate mafunzo haya muhimu kwakua katika miaka michache ijayo hawataruhusiwa kutoa huduma hiyo bila kutimiza masharti haya ya kisheria,” alisema Hasunga.

Alisema tafiti mbalimbali zinaonyesha kuwa watalii wengi wanaokuja nchini hupata taarifa kutoka kwa wenzao waliotembelea Tanzania ambao muda wao mwingi wanakuwa na waongoza watalii kwenye maeneo ya vivutio.

"Hivyo ni muhimu wapewe mafunzo  maalum waweze kutoa huduma bora zaidi zitakazowafanya watalii wafurahie ukarimu wao waweze kuwa mabalozi wazuri wa kuutangaza utalii wetu watakaporudi nchini kwao" alisema  Hasunga. 

Alisema licha ya Sekta ya utalii nchini kuchangia asilimia 17 ya pato la taifa na asilimia 25 ya fedha za kigeni (watalii milioni 1.28 na bilioni 2 mwaka 2016), mchango wake unaweza kukua zaidi kupitia mikakati mbalimbali inayowekwa  na wizara yake ikiwemo hiyo ya mafunzo ambayo imelenga kuongeza idadi ya watalii kufikia milioni mbili mwaka 2020 na watalii milioni 8 mwaka 2025 pamoja na mapato ya dola za kimarekani bilioni 20 mwaka 2025.

Akizungumzia kuhusu mafunzo ya jeshi usu chuoni hapo, Naibu Waziri Hasunga aliuagiza uongozi wa chuo hicho kuendesha mafunzo hayo muda wote wa masomo tofauti na ilivyo hivi sasa ambapo hutolewa kwa wiki mbili katika kila 'semister'.

"Mafunzo haya yasiishie tu kwa muda wa wiki mbili, ni matarajio yangu kuona yanaendeshwa katika kipindi chote cha mafunzo ikiwemo wanafunzi kuvaa sare za heshima za jeshi usu, kuwa na nidhamu ya kijeshi na muhimu zaidi kuonyesha utayari na uwezo wa kukabiliana na wahalifu ikiwemo majangili," alisema Hasunga.

Aidha, alizitaka taasisi zilizopo chini ya Wizara yake kuajiri wananfunzi wanaomaliza chuoni hapo ikiwa ni pamoja na kutumia fursa ya chuo hicho mahiri kuwaongezea ujuzi wafanyakazi waliopo makazini.

Kwa upande wake Mkuu wa Chuo hicho, Prof. Jafari Kideghesho alimueleza Naibu Waziri Hasunga kuwa Chuo chake kimeshafanya maandalizi yote ya kuanza kutoa mafunzo kwa waongoza watalii nchini kama ilivyoagizwa na wizara yake ambapo tathmini ya mahitaji ya mafunzo hayo imeshafanywa kwa kuainishwa mapungu katika taaluma, ujuzi na mitazamo. 

"Tumeshaandaa pia mitaala ya mafunzo ambayo imezingatia kuondoa mapungufu tuliyoyabaini, na tunatarajia kuanza mafunzo yetu ya kwanza kwa wapagazi 100 kwa muda wiki tatu kuanzia jumatatu ijayo (leo)," alisema Prof. Kideghesho.

Alisema ili kufanikisha mafunzo hayo chuo chake kimepokea msaada wa Shilingi milioni 110 kutoka Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) kwa ajili ya kutoa mafunzo kwa wapagazi wanaotoa huduma katika mlima Kilimanjaro, fedha ambazo zitatumika kwa ajili ya mafunzo na tafiti mbalimbali.

Mahafali hayo ya 53 yalihudhuriwa pia na Balozi wa Nigeria nchini,  Balozi Sahabi Dada, Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Chuo hicho, Prof. Faustin Bee, Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Kippi Warioba, Mkuu wa Wilaya ya Same, Harun Mbogo, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori, Nebo Mwina, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania, Prof. Dos Santos Silayo na baadhi ya wawakilishi wa Mamlaka ya Wanyamapori ya Uganda.

Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka kilianzishwa mwaka 1963 baada ya azimio la Arusha mwaka 1961 ambalo lilitaka uwepo wa watu waliopewa mafunzo kwa ajili ya kulinda na kusimamia urithi wa rasilimali za Afrika. 

Chuo hicho ambacho huendesha mafunzo yake kwa vitendo kwa zaidi ya asilimia 60 kimepata ongezeko la wanafunzi kutoka 25 mwaka 1963/1964 hadi zaidi ya wanafunzi 550 mwaka 2016/2017 kutoka nchi za Tanzania, Kenya, Uganda, Malawi na Cameroon.

Aidha, katika kipindi cha miaka 54 iliyopita chuo hicho kimeweza kufundisha zaidi ya mameneja wa wanyamapori 8,000 kutoka nchi zaidi ya 50 duniani.

Chuo hicho pia kimepewa tuzo na Jumuiya ya Afrika ya Mashariki kama Kituo cha Ubora wa Taaluma ya Usimamizi wa Wanyamapori (Centre of Excellence).
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Japhet Hasunga (wa pili kushoto) akipata maelezo kutoka kwa mmoja ya Mwanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka, Leonard Mgamba kuhusu mafunzo ya taaluma ya wanyamapori yanavyofanywa kwa vitendo chuoni hapo. Wengine pichani ni Balozi wa Nigeria nchini, Sahabi Dada (wa tatu kushoto), Mkuu wa Wilaya ya Same, Mhe. Harun Mbogo (kushoto) na Mtenaji Mkuu wa Wakala wa Huduma za Misitu, Prof. Dos Santos Silayo.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Japhet Hasunga (kulia) akiwa ndani ya handaki linalotumika kwa ajili ya mafunzo kwa vitendo katika Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori-Mweka muda mfupi kabla ya kuwatunuku vyeti wahitimu 224 wa kozi mbalimbali chuoni hapo.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Japhet Hasunga (kulia) akikagua gwaride la wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori-Mweka muda mfupi kabla ya kuwatunuku vyeti wahitimu 224 wa kozi mbalimbali ikiwemo Shahada, Astashahada na Stashada katika taaluma za usimamizi wa wanyamapori na utalii katika mahafali ya 53 yaliyofanyika chuoni hapo jana katika Wilaya ya Moshi Mkoani Kilimanjaro. Zaidi ya asilimia 60 ya mafunzo chuoni hapo hutolewa kwa vitendo na wahitimu 224 wa kozi mbalimbali walitunukiwa vyeti.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Japhet Hasunga (kulia) akisalimiana na baadhi ya viongozi wa Mamlaka ya Wanyamapori ya Uganda ambao walishiriki kwenye mahafali ya 53 ya Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori-Mweka jana.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori Mweka, Prof. Faustin Bee (kulia), Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Mhe. Kippi Warioba (katikati) na Mkuu wa Wilaya ya Same, Mhe. Harun Mbogo (kushoto) wakiteta jambo wakati wa mahafali ya 53 ya chuo hichao ambayo yalifanyika jana mkoani Kilimanjaro.
Mkuu wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori Mweka, Prof. Jafari Kideghesho (kulia) akiwasilisha taarifa fupi kuhusu chuo hicho kwa Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Japhet Hasunga (kushoto) wakati wa mahafali ya 53 ya chuo hicho ambayo yamefanyika jana mkoani Kiliamanjaro. Wengine ni Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Chuo hicho, Prof. Faustin Bee (wa pili kushoto) na Balozi wa Nigeria nchini, Mhe. Sahabi Dada.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Japhet Hasunga (kushoto) akizungumza na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori-Mweka, Prof. Faustin Bee (kulia), Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Mhe. Kippi Warioba (wa pili kulia) na Mkuu wa Wilaya ya Same, Mhe. Harun Mgogo wakati wa mahafali ya 53 ya chuo hicho ambayo yamefanyika jana mkoani Kilimanjaro. 
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Japhet Hasunga (kulia) na Balozi wa Nigeria nchini, Mhe. Sahabi Dada.
Mkuu wa Chuo chaUsimamizi wa Wanyamapori Mweka, Prof. Jafari Kideghesho (kulia) akiteta jambo na Balozi wa Nigeria nchini, Mhe. Sahabi Dada.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Japhet Hasunga (kushoto) akipata maelezo kutoka kwa Mwanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka, Ebenezer Mollel kuhusu mafunzo ya taaluma ya wanyamapori yanavyofanywa kwa vitendo chuoni hapo. Wengine pichani ni Mkuu wa Chuo hicho, Prof. Jafari Kideghesho (wa pili kushoto) na Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Mhe. Kippi Warioba.
Sehemu ya taswira ya Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori Mweka.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Japhet Hasunga akipanda mti wa kumbukumbu chuoni hao.
Baadhi ya wanafunzi wa chuo cha Usimamizi ya Wanyamapori Mweka, pembeni yao ni mifupa ya miguu ya tembo katika chumba maalum cha mafunzo ya wanyamapori.
Sehemu ya wananfunzi 224 waliopewa vyeti vya kuhitimu mafunzo mbalimbali katika Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori-Mweka wakiwasili katika viwanja kwa ajili ya mahafali ya 53 yachuo hicho yaliyofanyika jana katika viwanja vya chuo hicho wilayani Moshi Mkoa wa Kiliamanjaro. Vyeti hivyo vilitpolewa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga. 
Gwaride la wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori Mweka wakitoa heshma mbele ya mgeni rasmi, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Japhet Hasunga (hayuko pichani)

Naibu Waziri wa Maliasi na Utalii, Mhe. Japhet Hasunga (wa pili kulia) akimtunuku cheti Mhitimu wa Shahada ya Usimamizi wa Wanyamapori, katika Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori-Mweka, Valentina Fiasco ambaye ni raia wa Italia katika mahafali ya 53 yaliyofanyika jana chuoni hapo katika wilaya ya Moshi mkoani Kiliamanjaro. Kulia ni Mkuu wa Chuo hicho, Prof. Jafari Kideghesho. Jumla ya wahitimu 224 wa kozi mbalimbali walitunukiwa vyeti.
Naibu Waziri wa Maliasi na Utalii, Mhe. Japhet Hasunga (wa pili kulia) akimtunuku cheti mmoja ya wahitimu wa Shahada ya Usimamizi wa Wanyamapori, katika Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori-Mweka wakati wa mahafali ya 53 yaliyofanyika jana chuoni hapo katika Wilaya ya Moshi Mkoani Kiliamanjaro. Kulia ni Mkuu wa Chuo hicho, Prof. Jafari Kideghesho. Jumla ya wahitimu 224 wa kozi mbalimbali walitunukiwa vyeti. 
 Naibu Waziri wa Maliasi na Utalii, Mhe. Japhet Hasunga (wa pili kulia) akitoa tamko la kuwatunuku kozi mbalimbali wananfunzi 224 wa chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori Mweka katika mahafali ya 53 ya chuo hicho ambacho yamefanyika jana mkoani Kilimanjaro. Kulia ni Mkuu wa chuo hicho, Prof. Jafari Kideghesho, Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo hicho, Prof. Faustin Bee (wa tatu kulia) na Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Mhe. Kippi Warioba.
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania, Prof. Dos Santos Silayo (mwenye tai) na washiriki wengine katika mahafali hayo.

No comments:

Post a Comment