slider gif

slider gif

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

Saturday, May 6, 2017

WANAHABARI WA ISRAEL WATEMBELEA HIFADHI YA TAIFA YA GOMBE, WAAHIDI KUTANGAZA VIVUTIO VYA TANZANIA NCHINI HUMO


Kundi la waandishi wa habari kumi kutoka nchini Israel wakiwa katika hifadhi ya Taifa ya Gombe kwa ajili ya kurekodi vivutio mbalimbali vya utalii vinavyopatikana katika hifadhi hiyo kwa ajili ya kuvitangaza nchini kwao ikiwa ni mkakati wa Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Bodi ya Utalii Tanzania kwa kushirikiana na Hifadhi za Taifa (TANAPA). Kwa sasa soko la utalii la mashariki ya kati limeanza kufunguka kwa kasi ambapo hivi karibuni Waziri Mkuu Mstaafu wa Israel Ehud Barak ametembelea hifadhi za Ngorongoro na Serengeti.

HAMZA TEMBA - WMU
.......................................................................

Kundi la wanahabari kumi akiwemo muigizaji mmoja na maofisa wa kampuni ya utalii ya Safari kutoka nchini Israel limetembelea hifadhi ya Taifa ya Gombe iliyopo mkoani Kigoma na kufurahia vivutio lukuki vya utalii vinavyopatikana katika hifadhi hiyo na kuahidi kuvitangaza watakaporudi nchini kwao ikiwa ni mkakati wa Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia TANAPA na Bodi ya Utalii kutangaza vivutio hivyo nchini humo.

Akizungumza hivi karibuni mara baada ya kukamilika kwa ziara hiyo ya siku mbili, Kiongozi wa kundi hilo, Ronit Hershkovitz alisema ziara hiyo imekuwa na mafanikio makubwa ambapo wamefurahia kuona vivutio vya kipekee katika hifadhi hiyo na kuahidi kuwa mabalozi wazuri wa vivutio hivyo nchini Israel. 

“Ni furaha kubwa kuwa hapa Gombe, tumeona makundi ya Sokwe na fukwe nzuri za Ziwa Tanganyika, tuko hapa kwa ajili ya kwenda kueleza kivutio hiki na vivutio vingine vya Tanzania nchini Israel, Waisrael wanaipenda Tanzania na wanapenda kutembelea Tanzania, tumeona ongezeko kubwa la watalii katika miaka ya hivi karibuni kutoka Israel baada ya kazi ngumu ya muda mrefu, sasa tuna furaha kuona watalii wengi wanaongezeka na tungependa kuona pia Watanzania wengi wakitembelea Israel,” Alisema Ronit.

Aliongeza kuwa, “Tunaenda kueleza taarifa hizi kwenye mitandao ya kijamii, magazeti, televisheni na popote tutakapoweza, lakini kubwa zaidi ni kuwaeleza marafiki zetu ana kwa ana uzuri wa Tanzania kwasababu tunaipenda Tanzania, nakupenda sana”.

Walfson Noa, ambaye ni Mwandishi wa Mitandao ya Kijamii na Meneja Masoko wa Kampuni ya Utalii ya Safari ya Israel alisema, “Tulifanya matembezi kuwaona Sokwe wanaovutia sana huku wakiishi katika mazingira yao ya asili, hili ziwa ni la maajabu sana (Ziwa Tanganyika), hata nyani nao walikuwa wakijaribu kuingia kwenye mahema yetu ni jambo la kuvutia, katika mtizamo wa kimasoko hili ni eneo ambalo nitawashauri wateja wangu watembelee, ni kitu ambacho watu wanatakiwa kukifahamu, kugundua siri ya uzuri wa hifadhi ya Taifa ya Gombe” 

Kwa upande wake Meneja wa Mawasiliano wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania, Paschal Shelutete ambaye alikuwa kiongozi wa msafara huo akishirikiana na Meneja Mawasiliano TTB, Geofrey Tengeneza, Meneja Mawasiliano wa TFS, Glory Mziray na Afisa Mawasiliano wa Wizara ya Maliasili, Hamza Temba alisema ujio wa wanahabari hao utaleta chachu ya kuongezeka kwa watalii wengi kutoka Israel pamoja na kupanua soko la utalii kwa hifadhi za mikoa ya magharibi mwa Tanzania ikiwemo hifadhi ya Gombe.

“Tumekuja na kundi hili la wanahabari ambao wameamua kama mlivowasikia kwa dhati kabisa kwamba watakaporudi nyumbani watatumia mitandao ya kijamii, radio mbalimbali, Televisheni lakini kubwa zaidi magazeti, wataandaa makala na vipindi mbalimbali hivyo tunaamini kwa dhati kabisa watakaporudi nyumbani na kuzifanyia kazi taarifa zote walizozipata katika hifadhi ya Taifa ya Gombe ama kwa hakika tutashuhudia ongezeko kubwa la watalii kutoka nchini Israel katika siku chache zijazo,” Alisema Shelutete.

Aliongeza kuwa, “Ni wajibu wa kila Mtanzania kuhakikisha rasilimali hizi za hifadhi zinazopatikana katika hifadhi za taifa zinaendelea kutunzwa kwa ajili ya kizazi hiki na vizazi vijavyo, watalii hawaji kuangalia ng’ombe kwenye hifadhi zetu, nasisitiza kuwa mifugo haikubaliki kwenye hifadhi zetu”.

Msafara huo ulikuwa na wanahabari kutoka vyombo maarufu nchini humo ikiwemo kituo cha Televisheni cha Channel 2, Jarida la Atmosphere, Jarida la National Geographic, Jaria la wiki la Yediot Acharanot -7 Yamim na waandishi wawili wa mitandao ya kijamii. Wengine ni maofisa wawili wa kampuni ya Utalii ya Safari ya nchini humo.

Hifadhi ya Taifa ya Gombe ilianzishwa mwaka 1968 kwa ajili ya tafiti za kisayansi, hususani katika kuwalinda na kuwahifadhi wanyamapori adimu wa jamii ya Sokwe Mtu (chimpanzees) ambao wapo hatarini kutoweka. Hifadhi hii inaelezwa kuwa na Sokwe wasiopungua mia moja ambao huishi kwa makundi na kuwa kivutio kikubwa na adimu katika hifadhi hiyo ambayo ina ukubwa wa kilomita za mraba 52.
Timu maalum ya wanahabari kutoka nchini Israel ikiwa na wajumbe kumi ilipowasili katika uwanja wa ndege wa Kigoma tayari kwa ajili ya ziara ya kitalii ya siku mbili katika hifadhi ya Taifa ya Gombe. Ziaza hiyo iliandaliwa na Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) kwa kushirikiana na Shirika ya Hifadhi za Taifa Tanzani (TANAPA) kwa ajili ya kutangaza vivutio vya utalii vya Tanzania nchini Israel ikiwa ni mkakati maamlum wa kukamata soko la Mashariki ya Kati. Kutoka kulia wanaongoza msafara huo ni Meneja Mawasiliano TANAPA, Paschal Shelutete na Meneja Mahusiano wa TTB, Geofrey Tengeneza.
Wanahabari kutoka Israel wakipanda kwenye boti kwa ajili kunza safari kuelekea hifadhi ya Taifa ya Gombe. Msafara huo ulikuwa na wanahabari kutoka vyombo maarufu nchini humo ikiwemo kituo cha Televisheni cha Channel 2, Jarida la Atmosphere, Jarida la National Geographic, Jaria la wiki la Yediot Acharanot -7 Yamim na waandishi wawili wa mitandao ya kijamii. Wengine ni maofisa wawili wa kampuni ya Utalii ya Safari  ya nchini humo.
Msafara wa Wanahabari wa Israel wakiwa kwenye boti tayari kwa safari ya kuelekea hifadhi ya Taifa ya Gombe ambapo kutoka Kigoma mjini hadi kwenye hifadhi hiyo ni mwendo wa saa moja na nusu hadi masaa mawili.
Mhifadhi wa hifadhi ya Taifa ya Gombe, Elihuruma Wilson (kushoto) akitoa maelezo mafupi kwa wanahabari kutoka nchini Israel kuhusu hifadhi hiyo kabla ya kuanza ziara ya kutembelea vivutio vilivyopo. Alieleza kuwa hifadhi hiyo ina vivutio vingi wakiwemo  Sokwe zaidi 100, Nyani, Kima, maporomoko ya maji, ndege aina mbalimbali na fukwe nzuri za kuogelea za ziwa Tanganyika. 
Meneja Mawasiliano wa Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Paschal Shelutete (kulia), Meneja Mahusiano wa Bodi ya Utalii Tanzania (Geofrey Tengeneza) na Meneja Mawasiliano wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (Glory Mziray) wakiongoza msafara wa wanahabari wa Israel kutembelea Hifadhi ya Taifa ya Gombe.
Timu ya wanahabari wa Israel wakianza safari ya kuingia ndani ya msitu wa hifadhi ya Taifa ya Gombe kwa ajili ya kuona makundi mbalimbali ya Sokwe. Lengo kuu la ziara hiyo iliyoandaliwa na Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Bodi ya Utalii na TANAPA ni kutangaza vivutio vya utalii vya Tanzania nchini Israel.
Wanahabari kutoka Israel wakipata maelezo kutoka kwa mhifadhi wa hifadhi ya Taifa ya Gombe kuhusu utarartibu wa kuzingatia wawapo ndani ya hifadhi hiyo ikiwemo kutokupiga kelele na kuepuka matumizi ya mwanga wa kamera (Flash Lights).
Mmoja ya wanahabari wa Israel, Gerald Eddie wa Jarida la National Geographic akiwa katika harakati za kupata taswira mwanana ya picha za Sokwe ndani hifadhi ya Taifa ya Gombe.
Wanahabari wa Israel wakiwa ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Gombe.
Sokwe akirukia matawi ya miti akiwa na mtoto wake ndani ya hifadhi ya Taifa ya Gombe wakati wa ziara ya wanahabari wa Israel kwenye hifadhi hiyo.
Taswira mwanana ya Sokwe Mtu ndani ya hifadhi ya Taifa ya Gombe wakati wa ziara hiyo.
Mtoto wa Sokwe akila matunda yanayopatikana katika hifadhi ya Taifa ya Gombe wakati wa ziara ya wanahabari wa Israel katika hifadhi hiyo. Lengo kuu la ziara hiyo iliyoandaliwa na Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Bodi ya Utalii na TANAPA ni kutangaza vivutio vilivyopo Tanzania nchini Israel.
Sokwe akiwa kapumzika kwenye maeneo yake ya kujidai ndani ya hifadhi ya Taifa ya Gombe wakati wa zaira ya wanahabari wa Israel katika hifadhi hiyo. Wanahabari hao walifurahia kuwaona sokwe hao wanaoelezewa na wanasayansi kuwa wanakaribiana na binaadamu kwa takribani asilimia 80.
Meneja Mawasiliano wa Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Paschal Shelutete (wa pili kulia) akionesha kifaa maalum cha kupigia picha za angani (drone) kilichorushwa na mmoja wa mwanahabari ambaye ni mpigapicha kutoka Israel katika fukwe za Ziwa Tanganyika pembezoni mwa hifadhi ya Taifa ya Gombe wakati wa zaiara ya wanahabari hao hifadhini hapo.   
Kifaa hicho maalum cha kupiga picha za angani kijulikancho kama 'drone' kikiwa angani kupata taswira pana ya hifadhi ya Taifa ya Gombe.
Wanahabari hao wakipiga picha za mwanahabari mwenzao na nyani wanaopatikana katika hifadhi ya Taifa ya Gombe katika fukwe za Ziwa Tanganyika.
Mwanahabari maarufu nchini Israel, Dana Spector, wa Jarida la Yediot  Acharonot (kushoto) akiigiliza mkao wa nyani katika hifadhi ya Taifa ya Gombe wakati wa ziara hiyo. Matukio hayo yataonekana katika jarida hilo nchini Israel kwa ajili kutangaza vivutio vya Tanzania. Anayepiga picha ni Meneja Mawasiliano wa Shirika la Hifadhi za Taifa, Paschal Shelutete.
Mpiga picha wa Jarida la National Geographic la nchini Israel, Gerald Eddie akipiga picha nyani wanaopatikana katika hifadhi ya Taifa ya Gombe ambao pia ni kivutio cha utalii katika hifadhi hiyo kwa ajili ya kuvitangaza katika jarida hilo.
Nyani akiwa kambeba mtoto wake katika  hifadhi ya Taifa ya Gombe tukio ambalo pia sehemu ya vivutio vinavyopatikana katika hifadhi hiyo.
Wanahabari hao hawakutaka kupitwa na tukio lolote katika ziara yao hiyo, hapo wakipiga picha boti ambayo hufanya safari za kawaida kwa wananchi wa vijiji vya mwambao wa ziwa Tanganyika na Manispaa ya Kigoma.
Mwanahabari maarufu nchini Israel, Dana Spector, wa Jarida la Yediot  Acharonot (wa pili kushoto) na Mtangazaji maarufu wa Radio na Televisheni nchini humo, Ran Sarig wakiigiliza mkao wa nyani dume na jike katika fukwe za ziwa Tanganyika kwenye hifadhi ya Taifa ya Gombe.
Mwanahabari maarufu nchini Israel, Dana Spector, wa Jarida la Yediot  Acharonot (wa pili kushoto) na Mtangazaji maarufu wa Radio na Televisheni nchini humo, Ran Sarig wakifurahia matukio mbali mbali yaliyokuwa yakifanywa na nyani wa hifadhi ya Taifa ya Gombe.
Wanahabari hao pia walipata fursa ya kuogolea katika fukwe za kitalii za ziwa Tanganyika pembezoni mwa Hifadhi hiyo ya Taifa ya Gombe, Fukwe hiyo ni kivutio kikubwa cha utalii katika hifadhi ya Taifa ya Gombe. 
Wanahabari hao wakiwa wanaogelea katika fukwe za kuvutia za ziwa Tanganyika kwenye hifadhi ya Taifa ya Gombe huku wakipiga picha za tukio hilo kwa ajili kutangaza kivutio hicho nchini Israel.
Wanahabari hao pia walipata fursa kutembelea jamii ya kijiji cha Mwamgongo ambacho kinapakana na hifadhi ya Taifa ya Gombe, hapo wakimpiga picha mtoto aliyekuwa na mpira wa makaratasi ambao ni sehemu ya utalii wa kiutamaduni.
Mwandishi wa habari kutoka Israel ambaye ni mpiga picha wa kituo cha Televisheni cha Chanel 2, Roni Dahabari Kuban akiwapiga picha watoto katika kijiji cha Mwamgongo jirani na hifadhi ya Taifa ya Gombe.
Mtangazaji maarufu wa Radio na Televisheni nchini Israel, Ran Sarig akifungwa shuka aliyoinunua na wananchi wa Kigoma katika ziara hiyo. Shuka hizo zinazofumwa kwa mikono ni maarufu Mkoani Kigoma na sehemu ya utalii wa Kiutamaduni unaopatikana katika Mkoa huo. 
Mtangazaji maarufu wa Radio na Televisheni nchini Israel, Ran Sarig akipiga picha ya "Selfie" na baadhi ya watoto wa kijiji cha Mwamgongo kilichopo jirani na hifadhi ya Taifa ya Gombe wakati wa ziara hiyo.
Wanahabari hao walipotembelea kijiji cha Mwamgongo kilichopo jirani na hifadhi hiyo ya Taifa ya Gombe walipata kujionea na kushiriki katika ngoma za asili ambazo pia ni sehemu ya utalii wa kiutamaduni.
Mwanahabari maarufu nchini Israel, Dana Spector, wa Jarida la Yediot  Acharonot  akijaribu kuwasiliana na wanakikundi cha ngoma za asili wa kijiji cha Mwamgongo kinachopakana na hifadhi ya Taifa ya Gombe na kushudia kazi zao za mikono na ngoma ambazo ni sehemu ya utalii wa kiutamaduni.
Mwandishi wa habari wa mitandao ya kijamii nchini Israel, Walfson Noa akifurahia michezo na jamii ya watoto wa kijiji cha Mwamgongo wakati wa ziara hiyo.
Watalii wa ndani nao pia walikuwemo kufurahia vivutio vya utalii vinavyopatikana katika hifadhi hiyo na kutoa wito kwa watanzania wengi zaidi kuvitembelea. Meneja wa Shirika la Hifadhi za Taifa, Paschal Shelutete (wa pili kushoto waliosimama) akiongoza mahojiano na watalii hao wa ndani.
Picha ya pamoja ya wanahabari wa Israel, wahifadhi wa hifadhi ya Taifa ya Gombe na waongoza msafara huo ambao ni Meneja Mawasiliano wa TANAPA, Paschal Shelutete (wa pili kulia), Meneja Mahusiano wa TTB, Geofrey Tengeneza (katikati waliosimama), Meneja Mawasiliano TFS, Glory Mziray (wa tatu kulia) na Afisa Mawasiliano wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Hamza Temba (wa nne kulia).
Baada ya kutembelea hifadhi ya Taifa ya Gombe msafara wa wanahabari hao ulipanda boti kwa ajili ya safari ya kurudi Kigoma Mjini.

No comments:

Post a Comment