slider gif

slider gif

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

Sunday, July 9, 2017

TANZANIA YABADILI MSIMAMO WA UNESCO WA KUITAKA KUSITISHA UJENZI WA MRADI WA STIEGLER'S GORGE KATIKA PORI LA AKIBA LA SELOUS


HAMZA TEMBA - WMU
..............................................................

Tanzania imesisitiza uamuzi wake wa kuendelea na mpango wa kujenga mradi mkubwa wa kuzalisha umeme katika maporomoko ya mto Rufiji (Stiegler's Gorge Hydro Power Project) yaliyopo ndani ya Pori la Akiba la Selous mbele ya wajumbe wa Kamati ya Urithi wa Dunia kutokana na umuhimu wake kwa maendeleo ya Watanzania.

Akizungumza mwishoni mwa wiki katika mkutano wa 41 wa wajumbe wa Kamati ya Urithi wa Dunia unaoendeshwa na Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni la Umoja wa Mataifa (UNESCO) ambao unaendelea katika Jiji la Krakov nchini Poland, Kiongozi wa msafara huo ambaye ni Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Meja Jenerali Gaudence Milanzi aliwaeleza wajumbe wa mkutano huo kuwa mpango huo ulikuwepo katika ajenda ya Serikali ya Tanzania tangu miaka ya 1960's na kwamba ukubwa wa eneo litakalotumika kutekeleza mradi huo ni asilimia tatu tu ya eneo lote la pori hilo ambalo lina ukubwa wa kilometa za mraba 50,000.

Aliongeza kuwa, “Itakumbukwa kuwa mnamo mwaka 1982 wakati pori hili (Selous) limewekwa katika orodha ya maeneo ya urithi wa dunia, Shirika la Umoja wa Mataifa la Uhifadhi wa Asili (IUCN) liliutambua mradi huo wa Stiegler's Gorge kutokuwa na madhara makubwa katika uharibifu wa mazingira ukizingatia ukubwa wa pori hilo na eneo litakalotumika kujenga mradi huo”.

Aliwaeleza wajumbe hao kuwa, Serikali ya Tanzania inatekeleza sera ya kujenga uchumi wa viwanda hali inayopelekea kuwa na mahitaji makubwa ya nishati ya umeme hivyo kwa kuzingatia vyanzo vilivyopo imekuwa ni muhimu sasa kufikiria tena ujenzi wa mradi huo kama chanzo kingine muhimu cha nishati kuwezesha kufikia azma hiyo.

Alisema mradi huo utaongeza uzalishaji wa umeme nchini kufikia asilimia 144.8 hivyo kuondoa upungufu wa nishati uliopo kwa sasa na pindi utakapokamilika utawanufaisha watanzania wengi wanaoishi bila umeme ikiwa ni pamoja na kukidhi mahitaji yake ya kuendesha viwanda.


Meja Jenerali Milanzi alilazimika kutoa maelezo hayo kwa kamati hiyo ili kuweka bayana dhamira ya dhati Serikali ya Tanzania ya kuendelea na ujenzi wa mradi huo kwa ajili ya maendeleo endelevu huku akitoa rai kwao kuwa Serikali bado ipo tayari kwa mazungumzo ya namna bora ya kutekeleza mradi huo kwa faida ya jamii, uchumi na mustakbali bora wa mazingira ya hifadhi ya Selous na taifa kwa ujumla.


“Kwa kutumia teknolojia bora zilizopo, mipango imara na usimamizi thabiti, mradi huu utakua na faida kubwa kwa taifa ikiwa na pamoja na kuboresha maisha ya watu maskini na jamii kwa ujumla bila kuathiri mazingira yanayotoa faida hizo”, alisema Milanzi.


Hapo awali, kabla ya mkutano huo, ujumbe wa Tanzania ukiongozwa na Katibu Mkuu huyo ulifanya mazungumzo na Maafisa Waandamizi wa Kituo cha Urithi wa Dunia na Bodi za Ushauri ya kituo hicho na kuwasilisha kwa maandishi msimamo wa Tanzania kuhusu ujenzi wa mradi huo.


Tanzania ilipinga vikali rasimu ya azimio No. 41 COM 7 A.17 aya ya 7 ambalo liliitaka kusitisha kabisa (to permanently abandon) ujenzi wa mradi wa kuzalisha umeme katika maporomoko ya mto Rufiji (Stiegler's Gorge Hydro Power Project). Baada ya tamko la Tanzania kupinga azimio hilo kipengele hicho kilifanyiwa marekebisho ipasavyo na neno “to permanently abandon” (kusitisha kabisa) liliondolewa katika azimio hilo kupisha majadiliano zaidi.


Tanzania ni miongoni mwa nchi wanachama zilizosaini mkataba wa urithi wa Dunia wa mwaka 1972 huku ikiwa na maeneo sita yaliyorodheshwa katika urithi huo ikiwepo Pori la Akiba la Selous, Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro, Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, Mji Mkongwe (Zanzibar), Hifadhi ya Ngorongoro na Michoro ya kondoa, Kilwa Kisiwani na Songo Mnara. Aidha, ni mwanachama wa Kamati ya Urithi wa Dunia kwa kipindi cha miaka minne hadi mwaka 2019.


Tokea ijiunge na kamati hiyo mwaka 2015, Tanzania imekua na msimamo wa kuwa na maendeleo endelevu katika ajenda za mikutano yake pamoja na miongozo yake ili kuruhusu kuendeleza maeneo ya urithi wa dunia kuweza kufikia maendeleo ya kijamii na kiuchumi bila kuwepo kwa athari kubwa katika mazingira.


Mkutano huo wa 41 wa wajumbe wa Kamati ya Urithi wa Dunia unaoendelea katika jiji la Krakov nchini Poland umehudhuriwa na nchi wanachama 193 na unajadili mambo mbalimbali muhimu kuhusu uhifadhi na ulinzi maeneo ya urithi wa dunia pamoja na kutangaza maeneo mengine mapya ya urithi wa dunia yaliyowasilishwa na nchi nyingine wanachama katika mkutano huo.

Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo ulijumuisha pia Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa ambaye pia ni mjumbe wa kudumu wa UNESCO, Samwel W. Shulukindo na Maafisa Waandamizi kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii.  Mkutano huo ulianza tarehe 2 Julai na unategemewa kumalizika tarehe 12 Julai, 2017.

Muonekano wa mto Rufiji kutokea angani ambao maporomoko yake yatatumika kuzalisha umeme katika mradi unaotarajiwa kujengwa na Serikali wa Stiegler's Gorge.
Sehemu ya mto Rufiji unakatiza katika Pori la Akiba la Selous.

Pori la akiba la Selous lina vivutio vingi vya utalii ikiwemo wanyamapori mbalimbali wakubwa kama Tembo, Simba, Nyati, Chui, Twiga na Viboko.


No comments:

Post a Comment