slider gif

slider gif

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

kilimanjaro CAN ONLY B CLIMBED FROM TZ

Thursday, November 24, 2016

WAZIRI MKUU KASSIM MAJALIWA AZUGUMZA NA VIONGOZI NA WATENDAJI WAKUU WA WIZARA YA MALIASILI NA UTALII

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza katika kikao alichokiitisha kati yake na  Watendaji Wakuu wa  Wizara ya Maliasili na Utalii na Wakuu wa Mapori  ya Hifadhi za Mistitu, Ofisini kwake mjini Dodoma Novemba 21, 2016.  Kulia kwake ni Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhandisi Ramo Makani (kushoto kwake) na Katibu Mkuu, Wizara ya Maliasili na Utalii, Maj. Gen. Gaudence Milanzi.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe akizungumza katika Mkutano ulioitishwa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  Ofisini kwake mjiniDodoma Novemba 21, 2016.
  Baadhi ya Watendaji Wakuu  wa Wizara ya Maliasili na Utalii  wakimsikiliza Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa wakati alipozungumza nao Ofisini kwake mjini Dodoma, Novemba 21, 2016.
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiagana na Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe (kulia) na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhandisi Ramo Makani (katikati) baada ya kuongoza kikao kati yake na Viongozi na Watendaji Wakuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Ofisini kwake mjini Dodoma Novemba 21, 2016.
____________________________

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ametoa miezi na siku tisa kwa Wakuu wa Mapori ya Hifadhi za Misitu kuhakikisha wanaweka mawe ya alama (beacons) kwenye mipaka yao ili kuepusha migogoro na wanavijiji wanaowazunguka.

Ametoa agizo hilo leo jioni (Jumatatu, Novemba 21, 2016) wakati akizungumza na Watendaji Wakuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii na Wakuu wa Mapori ya Hifadhi za Misitu nchini katika kikao alichokiitisha kwenye ukumbi wa Ofisi ya Waziri Mkuu mjini Dodoma.

“Tatizo la migogoro baina ya wafugaji, wakulima na kamati za ulinzi na usalama za mikoa na wilaya ni lazima lifanyiwe kazi. Mkitoka hapa rudini katika maeneo yenu mkawaambie wananchi mipaka yenu iko wapi. Ninyi mnatambua mipaka yenu iko wapi kwa hiyo waelewesheni wananchi kwa kuweka alama,” amesema.

“Wakati Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli akizindua bunge tarehe 20 Novemba, 2015 aliwapa maeneo makuu matatu ambayo ni kuanisha mipaka, kupambana na ujangili na kukusanya mapato. Alizungumzia suala la mipaka kwa sababu iliyopo haieleweki, mkiulizwa mnajibu kuna buffer zone. Hivi mwananchi wa kawaida anajua buffer zone ni nini?,” alihoji.

“Sasa ninawapa muda hadi Januari 31, 2017 kazi ya kuweka beacons kwenye hifadhi zote za misitu iwe imekamilika. Kila pori nenda mkatengeneze alama zenu kama TANROADS walivyofanya. Kaeni mpige hesabu ni kiasi gani cha saruji na kokoto kinahitajika. Tutarudi hapa Dodoma kupeana taarifa ya utekelezaji. Katibu Mkuu niletee taarifa ya kila mkoa na wilaya kuna mapori mangapi tutakutana hapahapa kupeana mrejesho,” alisisitiza.

Alisema kama TANROADS waliweza kuweka alama za barabarani kwa nchi nzima ni kwa nini Wizara ya Maliasili na Utalii imeshindwa kuchukua hatua kama hizo. “Ni lazima tuweke hizo alama kila katika pori lake, tusipofanya hivyo, migogoro hii itaendelea,” alisema.

“Nendeni mkaweke alama za mipaka mkishamaliza sasa muwaeleze wananchi ni umbali wanapaswa waache kutoka kwenye hizo alama zenu na muwaelimishe kwamba hiyo ndiyo buffer zone. Suala la beacons ni serious na ninatarajia nikute hizo beacons kwenye maeneo yenu”

“Kila mmoja anayo fursa ya kuitisha mkutano na wananchi na kuwaelimisha kuhusu umuhimu wa kuwa na mapori ya akiba. Pandeni kwenye majukwaa, muelezee mipaka hiyo mipya na wananchi watawaelewa kwa sababu mwenye dhamana ya kwanza katika kutoa elimu hii ni wewe Mkuu wa Pori,” alisistiza.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema kuanzia leo Ofisi ya Rais TAMISEMI haina budi kusitisha usajili wa vijiji hadi zoezi la kuweka alama kwenye mipaka mapori ya hifadhi za misitu litakapokalimika.

“Kuanzia leo ninasimamisha zoezi la usajili wa vijiji unaofanywa na TAMISEMI hadi wizara ya Maliasili na Utalii ikamilikshe zoezi la kuainisha na kuweka alama kwenye mipaka mapori ya hifadhi za misitu. Tusipofanya hivyo tutaendelea kuwa na Taifa la walalamikaji,” alisema huku akishangiliwa na watendaji hao.

“Wakuu wa mapori tambueni ni vijiji vingapi ambavyo Serikali ilifanya makosa na kuvisajili wakati viko ndani ya hifadhi na vijiji vingapi bado havijasajiliwa. Pia onyesheni ni vijiji vingapi ambavyo ni hatarishi,” alisema.

Wakati huo huo, Waziri Mkuu amemtaka Mkurugenzi wa Idara ya Utalii katika wizara hiyo, Bw. Zahoro Kimwaga pamoja na Bodi ya Utalii nchini wabadilike na kuanza kufanya kazi kibiashara zaidi.

“Mkurugenzi wa Utalii na Bodi yako ya Utalii bado hamjajitangaza vya kutosha. Promosheni ya utalii hapa nchini bado haitoshi na mgeweza kuoata mapato makubwa zaidi kwa kujitangaza. Mabango ya barabarani yamejaa matangazo ya Vodacom na Airtel badala ya kuwa na picha za wanyama ili kila mtu akiona atamani kwenda mbugani,” alisema.

“Tumieni mabango ya kieletroniki (electronic screens) kurusha picha za wanyama. Mfano pale nje ya uwanja wa Taifa, au uwanja wa ndege hata kwenye njia kuu  za mikoani wekeni mabango ya iana hiyo. Ombeni vipindi kwenye televisheni nyingine, kile cha TBC1 peke yake hakitoshi,” alisisitiza.

KUKUZA UCHUMI KUPITIA SEKTA YA UTALII KUNAHITAJI WAFANYAKAZI WENYE SIFA - MAGHEMBE

Waziri wa Maliasili na utalii, Prof. Jumanne Maghembe (wa pili kulia) akisikiliza maelezo ya mmoja wa wahitimu wa mafuzo ya upishi katika hoteli za kitalii wakati wa mahafali ya sita ya Chuo cha Hoteli na Utalii Njuweni kilichopo Kibaha, mkoani Pwani hivi karibuni. 
_______________________________

Waziri wa Maliasili na utalii, Prof. Jumanne Maghembe amesema  ili Tanzania iendelelee kukuza uchumi kupitia sekta ya utalii inahitaji wafanyakazi wa kada hiyo  wawe na sifa zinazostahili ikiwemo nidhamu na uaminifu.


Ameyasema hayo hivi karibuni alipokuwa mgeni rasmi kwenye mahafali ya  6 ya Chuo cha Hotel na Utalii  cha Njuweni kilichoko  Kibaha mkoani Pwani ambayo yalifanyika kwenye viwanja vya Chuo hicho.

Alisema kuwa  pamoja na vyanzo mbalimbali vya mapato vinavyokuza uchumi wa taifa taifa,  Wizara ya Maliasili na Utalii ina mchango mkubwa katika kukuza uchumi huo hivyo kinachotakiwa ni kuhakikisha watu wanaopewa dhamana ya kufanyakazi kwenye Wizara hiyo wanafanya kazi kwa weledi.

"Napenda kuwakumbusha kuwa nidhamu na uaminifu ndiyo siri itakayowawezesha ninyi kufika mbali katika utendaji wenu wa kazi, lakini mkiingiza tamaa na udokozi hamtafika mbali na badala yake mtalitia taifa kwenye sifa mbaya" alisema

Alisema kuwa Serikali imekuwa ikikuza uchumi wa nchi kila mwaka kupitia Sekta ya utalii ambapo idadi ya  watalii  imekuwa ikiongezeka kwa asilimia 23.7 kutoka watalii 867,994 mwaka 2011 hadi kufikia watalii 1,137,182 mwaka 2015. Aidha sekta hiyo inachangia asilimia 17 ya pato la taifa.

"Mapato yatokanayo na  shughuli za utalii yaliongezeka  kwa asilimia 28.8 kutoka dola za Marekani mil. 1,353.29 mwaka 2011 hadi kufikia dola za Marekani mil. 1,901.1 mwaka 2015" alisema

kwa upande wake Mkuu wa Chuo hicho, Nditi Rashid alisema kuwa pamoja na mafanikio yaliyopatikana kwa miaka kadhaa tangu kuanzishwa kwa chuo hicho lakini bado kuna changamoto kadhaa zinazowakabili ikiwemo upungufu wa vifaa vya kisasa vya kuendeshea masomo ya TEHAMA

"kutokana na ufinyu wa bajeti tulionao tunakuomba mheshimiwa mgeni rasmi utusaidie kupata msaada wa vifaa vipya vitakavyotusaidia kuendesha masomo ya TEHAMA kwa ufanisi zaidi" alisema

Mahafari hayo ambayo ni ya sita tangu kuanzishwa kwa chuo hicho mwaka 200o  yalihusisha jumla ya wanafunzi 350 waliohitimu kwa ngazi ya stashahada ambao walipata vyeti na zawadi mbalimbali .

Wednesday, November 23, 2016

HAKUNA KIONGOZI WA JUU WA SERIKALI ANAYEPINGA ZOEZI LA UHIFADHI NCHINI – MAJALIWA



NA HAMZA TEMBA - WMU
......................................................................

Kufuatia malalamiko ya wahifadhi juu ya kauli na vitendo mbalimbali za baadhi ya wananchi na viongozi wa kisiasa vyenye lengo la kukwamisha shughuli za uhifadhi nchini kwa maslahi yao binafsi kwa visingizio kuwa ni maagizo kutoka juu, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ametoa tamko na kusema kuwa hakuna kiongozi wa juu wa Serikali anayepinga zoezi la uhifadhi wa maliasili nchini.
Majaliwa ameyasema hayo juzi wakati akizungumza na viongozi na watendaji wakuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, wakuu wa taasisi za uhifadhi zilizopo chini ya wizara hiyo na wakuu wa hifadhi za taifa pamoja na mapori ya akiba katika kikao alichokiitisha kwenye ukumbi wa ofisi ya Waziri Mkuu mjini Dodoma.
“Wapo watu wanaotumia majina ya viongozi wakuu kukwamisha mazoezi yanayoendeshwa na wahifadhi nchini. Hakuna kiongozi wa juu anaeweza kuzuia zoezi muhimu kama hili. Na Kama kuna mtu anakuja kukuambia wewe fulani kasema, mwambie niunganishe na yeye mwenyewe.  Tumeona maeneo mengi sana, watu wanafanya madudu wanasema huyu kaagizwa kutoka juu, juu ni wapi, kwa Mkurugenzi wako? kwa Katibu Mkuu?  Naibu Waziri au Waziri? Au huku kwa Waziri mkuu? Makamu wa Rais au Rais?,” alihoji.
“Fanyeni, bora ukosee halafu tuseme hapo umekosea utarekebisha, kuliko kuogopa kufanya kwa sababu mtu kakukwamisha, kwani ulivokuwa unaimplement (unafanya) alikuambia nani? si kutokana na na sheria na taratibu, muhimu zaidi ni kuzingatia sheria na taratibu, usije ukafanya mambo ya ajabu,” aliongeza.
Ili kufanikisha zoezi hilo aliwaagiza pia kuhakikisha wanaweka alama za mipaka (beacons) katika hifadhi zao hadi kufikia januari 31, 2017 ili kuepusha migogoro na wananchi wanaovamia maeneo hayo kwa makusudi au kwa kutokujua maeneo ya mipaka husika.
“Nendeni mkawaambie mwisho ni hapa weka na beacon kabisa, na sheria zitachukua mkondo wake kwa yeyote ambaye hatafata maelekezo yenu. Tatizo la migogo iliyozungumzwa kati wa wafugaji na wahifadhi au wafugaji na kamati za ulinzi na usalama za wilaya na mikoa ni lazma likafanyiwe kazi, lazima tuendelee kudhibiti kuingia mifugo ndani ya mapori,” alisisitiza.
Aliwaagiza pia kusimama kwenye majukwaa na kutoa elimu ya uhifadhi kwa wananchi wanaozunguka maeneo yao ya hifadhi. “Namba moja wa utoaji elimu ni wewe mkuu wa pori, ni lazma utoe maelezo ya pori lako ni wapi linakoishia, kama mpaka huo ni wa kisheria muwaambie, nini umuhimu wa kutoingia, wananchi wapate elimu namna ya kuhifadhi pori na faida zake,” alisema.
Akizungumzia changamoto iliyoibuliwa katika kikao hicho kuhusu mgongano uliopo katika usimamizi wa misitu baina Wakala wa Huduma za misitu Tanzania na Serikali za Mitaa alisema Serikali inaenda kuliangalia upya suala hilo ili ione namna bora ya kutoa majukumu ya kusimamia rasilimali zote za misitu kwa chombo kimoja tofauti na ilivyo hivi sasa, hatua ambayo inaelezwa kuwa itasaidia kwa kiasi kikubwa kuondoa changamoto za uharibifu wa misitu nchini.
“Kama ilivyoelezwa kuwa kuna mgongano wa majukumu kwenye kitengo cha misitu, baina ya TFS na DFO (Ofisa misitu wa Wilaya), DFO anauza bila hata kumconsult (kumtaarifu) TFS na anagonga na nyundo…, kwa hiyo tutaliangalia tuone majukumu yale na namna ambavyo tunaweza tukayapa chombo kimoja ili kisimamie lakini TFS mmeperform (mmefanya) vizuri endeleeni kufanya hivyo vizuri kwa sasa,” alisema huku akipigiwa makofi na watendaji hao.
Changamoto nyingine iliyoibuliwa katika kikao hicho ni matukio ya kuingizwa kwa mifugo katika maeneo ya hifadhi yaliyoko mpakani huku asilimia kubwa ya mifugo hiyo ikielezwa kutoka nje ya nchi, Waziri Mkuu Majaliwa amekemea kitendo hicho na kuagiza mifugo hiyo iondolewe mara moja. “Hatutaki ng'ombe wa nje ya nchi kuingia ndani ya nchi, mifugo ya ndani imetutosha,” alisema.
Aidha ameutaka uongozi wa Wizara kuimarisha doria za mara kwa mara, kuongeza ajira za makamanda (askari wa wanyamapori) na vitendea kazi muhimu vya kuimarisha doria ikiwemo magari.
Kwa upende wake Waziri wa Maliasili na Utalii, Prof. Jumanne Maghembe alisema ipo changamoto kubwa ya tishio la kutoweka kwa mvua na kukauka kwa vyanzo muhimu vya maji nchini kutokana na uharibifu wa maeneo yaliyohifadhiwa pamoja na mlipuko wa magonjwa mbalimbali yanayosababishwa na muingiliano wa mifugo na wanyamapori kama vile kimeta na homa ya bonde la ufa.
Naye Mkurugenzi wa Idara ya Utalii wa Wizara hiyo, Zahoro Kimwaga alisema, umuhimu wa uhifadhi una faida mtambuka  ambapo sekta ya utalii pekee inachangia asilimia 17 ya pato la taifa huku ikitoa ajira za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja takriban milioni 1.5. Alisema sekta hiyo pia inachangia asilimia 25 ya mapato yote ya fedha za kigeni ikiwa ni sekta kiongozi kwa muda wa miaka mitatu mfululizo.
Aliongeza kuwa hadi kufikia Novemba 20 mwaka huu takwimu zinaonyesha kuwa maendeleo ya sekta ya utalii yameongezeka kwa asilimia 5 licha ya malalamiko mbalimbali kuhusu sekta hiyo baada ya Serikali kuweka kodi ya VAT katika huduma za kitalii nchini.

Tuesday, November 15, 2016

WAZIRI WA MALIASILI, PROF. JUMANNE MAGHEMBE AFUNGUA MKUTANO WA WADAU WA MISITU KUJADILI UHAMASISHAJI NA UENDELEZAJI WA SEKTA HIYO

Waziri wa Maliasili na Utalii, Prof. Jumanne Maghembe akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Kikanda wa Wadau wa Sekta ya Misitu wa nchi ya Finland na Tanzania uliofanyika leo katika hoteli ya Hyatt Regency, Jijini Dar es Salaam. Lengo kuu la mkutano huo likiwa ni kuhamasisha uwekezaji na kukuza ushirikiano baina ya nchi hizo mbili katika uendelezaji wa misitu nchini. Mkutano huo umeandaliwa kwa ushirikiano wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Mambo ya Nje ya Finland, Taasisi ya Uongozi - UONGOZI Institute na Shirika la Maendeleo ya Kifenda la Finland - FINFUND. 
Waziri wa Mambo ya Nje, Biashara na Maendeleo wa Serikali ya Finland, Kai Mykanen akizungumza katika Mkutano huo ambapo ameahidi kuendeleza ushirikiano uliopo baina ya  Finland na Tanzania katika kuendeleza Misitu kwa faida ya kizazi cha sasa na kijacho ikiwa ni pamoja na kukuza teknolojia ya uhifadhi wa mazingira ya kupunguza hewa ukaa. 
 Baadhi ya washiriki wa mkutano huo, kutoka kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Misitu na Nyuki, Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Ezekiel Mwakalukwa, Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili, Eng. Angelina Madete na Kaimu Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania, Prof. Dos Santos Silayo.
Baadhi ya wajumbe katika mkutano huo wakifualia hotuba ya ufunguzi iliyotolewa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Prof. Jumanne Maghembe.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Prof. Jumanne Maghembe (katikati) akizungumza na baadhi ya viongozi wa Serikali ya Finland ikiongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje, Biashara na Maendeleo, Kai Mykanen (wa pili kushoto) muda mfupi kabla ya ufunguzi wa mkutano huo. Wengine kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mehenge, Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Meja Generali, Gaudence Milanzi na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Misitu na Nyuki, Dkt. Ezekiel Mwakalukwa.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Prof. Jumanne Maghembe akizungumza na waandishi wa habari muda mfupi baada ya ufunguzi wa mkutano huo. Alieleza kuwa Tanzania inakabiliwa na changamoto kubwa ya uharibifu wa misitu unaotokana na uvunaji wa mkaa na ukataji wa magogo, uvunaji wa miti usio endelevu jambo lililoisukuma Serikali kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo Serikali ya Finland na wananchi kwa ujumla kwa ajili kuendeleza misitu kwa kupanda miti mingi zaidi iweze kukidhi mahitaji yaliyopo. Aliongeza kuwa ni marufuku kusafirisha magogo na kwamba Serikali ya awamu ya tano imelenga kukuza viwanda kwa ajili ya kuongeza thamani kwenye mazao ya misitu na kuyauza kama bidhaa. Ametoa wito kwa watanzania kujishuulisha na upandaji wa miti kibiashara ili kuinua maisha yao na uchumi wa taifa kwa ujumla. Kushoto kwake ni Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Meja Generali Gaudence Milanzi na kulia kwake ni Mkurugezi Mtendaji wa Taasisi ya Uongozi, Prof. Joseph Semboja.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Prof. Jumanne Maghembe (kushoto) akimkabidhi zawadi ya kinyago, Waziri wa Mambo ya Nje, Biashara na Maendeleo wa Serikali ya Finland, Kai Mykanen katika hafla ya jioni iliyofanyika katika hoteli ya Hyatt Regency, Jijini Dar es Salaam.
_____________________________


Watanzania wametakiwa kutumia fursa ya upandaji wa miti kibiashara kuinua uchumi wa maisha yao na kuacha biashara haramu ya usafirishaji wa magogo nje ya nchi, badala yake watumie fursa hiyo kuzalisha bidhaa za misitu na kuziuza kwa faida zaidi.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe aliyasema hayo jana Dar es Salaam wakati akifungua mkutano wa uwekezaji wa misitu uliowashirikisha wadau wa Mazingira kutoka nchi 16 ulioandaliwa kwa ushirikiano na Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Mambo ya Nje ya Finland, Taasisi ya Uongozi na Shirika la Maendeleo ya Kifenda la Finland - FINFUND.
“Wawekezaji wa misitu wanasema wanataka soko la mazao yao na sisi tunasema soko lipo isipokuwa watengeneze bidhaa kama vitanda, viti na samani za ndani pamoja na makaratasi na vifaa vyote vinavyotokana na miti na hiyo ndiyo itawasaidia ndugu zetu kupata ajira na viwanda vitaongezeka.
“Tukiruhusu magogo kwenda nje itakuwa kama pamba yetu inalimwa hapa na kusafirishwa halafu inatengeneza nguo na tunaletewa, lazima Viwanda vijengwe na hiyo si kazi ngumu.... Tunachotaka hapa teknolojia ya viwanda ije, wasafirishe bidhaa na si magogo,” alisema Profesa Maghembe.
Aliongeza kuwa “Tunataka kufanya uwekezaji katika hewa ukaa, ambayo italeta tija kwa jamii na kutumia zaidi teknolojia katika upandaji wa miti ili kuongeza ubora na soko la mazao hayo”.
Alisema inakaridiwa kwamba hekta 30,000 za misitu zinapotea kila mwaka kutokana na sababu mbalimbali huku zikiwa zinapadwa hekta 80,000 hadi 100,000 kila mwaka.
Alisema kuna changamoto kubwa ya uchomaji mkaa na wengine wanasafirisha nje kupitia kwa bandari bubu na hivyo misitu kupotea kwa sababu pia ya uvunaji wa misitu usio endelevu.
Alisema changamoto nyingine ni uvunaji usio endelevu wa misitu na kupungua kwa vyanzo vya maji kutokana na ukataji wa miti hovyo na uharibifu wa misitu, hivyo Serikali inaongeza juhudi kuhakikisha vyanzo vya maji vinalindwa.
Mkuu wa Taasisi ya Uongozi, Profesa Joseph Semboja alisema jukumu lao ni kuwaweka viongozi na wadau mbalimbali katika kuangalia maendeleo endelevu ambapo kwa sasa wanaangalia namna ya kukabiliana na changamoto kubwa ya mabadiliko ya tabianchi ikiwa ni pamoja na kuboresha na kuendeleza misitu kibiashara.
Mwakilishi wa Benki ya Dunia, Yutaka Yoshino alisema Idara ya Misitu nchini imekuwa ikichangia ukuaji wa uchumi nchini, lakini sekta hiyo imekuwa ikikabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo mabadiliko ya tabianchi.


Thursday, October 27, 2016

TFS YANASA LORI LIKISAFIRISHA MBAO KINYUME CHA SHERIA, DEREVA ATOKOMEA KUSIKOJULIKANA

Kaimu Afisa Habari na Mawasiliano ambaye pia Ofisa Misitu Mkuu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania, Nurdin chamuya (Kushoto) akizungumza na waandishi wa habari (hawako pichani) Jijiji Dar es Salaam jana kuhusiana na kukamatwa kwa lori lenye namba za usajili T676 ANQ lililokuwa linasafirisha mbao kinyume cha sheria kutoka Mkoani Kigoma kuja Jijini Dar es Salaam. Kulia ni Afisa wa Himasheria wa Wakala huyo, Arjason Mloge. 
Kaimu Afisa Habari na Mawasiliano ambaye pia Ofisa Misitu Mkuu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania, Nurdin chamuya (Kushoto) na Afisa wa Himasheria wa Wakala huyo, Arjason Mloge wakionesha sehemu ya mbao zilizokuwa zimefunikwa na katoni za sabuni ndani ya lori lenye namba za usajili T676 ANQ lililokuwa linasafirisha mbao hizo kinyume cha sheria kutoka Mkoani Kigoma kuja Jijini Dar es Salaam.
Muonekano wa sehemu ya mbao hizo zikiwa zimefunikwa na sabuni ndani ya lori hilo.
Maofisa wa kikosi Dhidi ya Ujangili kanda ya Dar es Salaam na kikosi cha Kufuatilia na Kuzuia Uharibifu wa Misitu cha Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania wakitumia mbwa maalum wa kunusa (Sniffer Dog) kwa ajili ya kutambua bidhaa haramu ndani ya lori hilo.
Muonekano wa nje wa Lori hilo.
______________________________

Kikosi cha Kufuatilia na Kuzuia Uharibifu wa Misitu cha Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania kwa kushirikiana na Kikosi Dhidi ya Ujangili kanda ya Dar es Salaam kimefanikiwa kukamata lori lenye namba za usajili T 676 ANQ lililokuwa likisafirisha mbao kinyume cha sheria huku zikiwa zimefichwa kwa kufunikwa na bidhaa mbalimbali ikiwemo sabuni ili zisionekane kiurahisi kwenye vituo vya ukaguzi.

Akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dar es Salaam leo, Kaimu Afisa Habari wa Wakala huyo, Nurdin Chamuya alisema tukio hilo limetokea tarehe 14 Oktoba, 2016 majira ya saa kumi usiku maeneo ya Amana, Ilala Jijini Dar es Salaam baada ya kupata taarifa kutoka kwa raia wema juu ya uwepo lori hilo katika maeneo hayo.

Chamuya alisema baada ya kupata taarifa hizo vikosi hivyo vilifika eneo la tukio na kufanya mahojiano na baadhi ya wananchi waliokuwa karibu na lori hilo ambapo mmoja kati ya wahudumu wa lori hilo alieleza kuwa lori hilo lilitokea Mkoani Kigoma na kwamba lilikuwa limepakia mzigo wa sabuni na chupa za maji zilizotumika. Dereva wa lori hilo hakuweza kupatikana.

“Wahudumu hao walipotakiwa kufungua mlango wa lori hilo kwa ajili ya upekuzi zaidi walisita kwa madai kuwa hawakuwa na funguo za lori hilo, Hatimaye   waliwasiliana na mmlikiwa wa eneo ambaye alikuwa amekabidhiwa funguo kwa ajili ya ulinzi” alisema Chamuya.

Alieleza kuwa mmiliki huyo alipofika alisema, anamfahamu mwenye gari ambaye ndiye mpangaji wa eneo lilipokutwa gari na kwamba anazo taarifa za  gari hilo,  na ameombwa apokee mzigo na kuutunza hadi atakaporudi kutoka safari ya  Mwanza kwa tatizo la msiba wa Baba yake.

Baada ya mmiliki wa eneo hilo kufanya mawasiliano na mwenye gari kuhusu mzigo uliokuwa kwenye gari hilo, mwenye gari alieleza kuwa kwa taarifa za dereva wake na ajenti aliyepakia mzigo Kigoma, gari lake lilikuwa na chupa chakavu na sabuni kutoka Kigoma na hakuna aina nyingine ya mzigo kwa ufahamu wake na akaruhusu gari hilo kufunguliwa mbele ya mwenye eneo.

“Baada ya gari hilo kufunguliwa, kilichoonekana kwa urahisi ni sabuni na mifuko michache inayosomeka kwa nje kuwa ni dawa ya kuku. Baada ya upekuzi ndipo zilionekana mbao zilizokuwa zimefichwa chini ya katoni za sabuni. Tumeshikilia Lori hilo kwa hatua zaidi za kisheria.

“Kufuatia tukio hili, Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia kwa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania tunatoa onyo kali kwa wale wote wanaojihusisha na vitendo vya uvunaji na usafirishaji wa mazao ya misitu kinyume cha sheria ya misitu namba 14 ya mwaka 2002 pamoja na kanuni zake za mwaka 2004 na kwamba watakaobainika watachukuliwa hatua kali kwa mujibu wa sheria za nchi” alisema Chamuya.

Akizungumzia athari mbalimbali za vitendo hivyo vya uvunaji holela wa mazao ya misitu bila ya kufuata taratibu za kisheria za uvunaji endelevu alisema vitendo hivyo vinatishia nchi kuwa jangwa ambapo takwimu zinaonyesha jumla ya hekta 372,000 za misitu nchini hupotea kila mwaka kutokana na matumizi makubwa ya rasilimali hizo ambayo yanazidi uzalishaji wake kwa ujazo wa mita 19.5 milioni kwa mwaka.

Chamuya ametoa wito kwa wananchi wote nchini kushirikiana na Serikali katika uhifadhi na ulinzi wa rasilimali za misitu na kuacha fikra potofu kuwa kazi hiyo ni ya Serikali pekee na taasisi zake kwakuwa faida zake hunufaisha jamii yote na vivyo hivyo kama athari zitajitokeza basi zitaikumba jamii yote bila kubagua.

Friday, October 21, 2016

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII, PROF. JUMANNE MAGHEMBE AAHIDI KUFANYA MABADILIKO MAKUBWA CHUO CHA TAIFA CHA UTALII

Waziri wa Maliasili Na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe akizungumza na watumishi wa Chuo cha Taifa cha Utalii Kampasi ya Bustani pamoja na waandishi wa habari alipotembelea chuo hicho juzi.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe (wanne kushoto) akikagua sehemu ya jiko katika chuo hicho.
Picha ya pamoja kati ya Waziri wa Maliasili Na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe na viongozi pamoja na watumishi wa chuo hicho.
________________________________________

Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe, ameahidi kuibadili Bodi ya Ushauri ya Chuo cha Taifa cha Utalii na kuifanya kuwa Bodi ya Utawala.

Alisema lengo la mabadiliko hayo ni kuhakikisha Chuo hicho kinatoa wataalamu wenye sifa na viwango vinavyostahiki kufanya kazi ndani na nje ya nchi.

Waziri Maghembe ametoa kauli hiyo juzi alipotembelea chuo hicho na kuangalia namna ya kukiboresha na kukifanya kiwe cha ushindani.


Aidha, Prof.Maghembe ameutaka uongozi wa chuo hicho kuondoa jina la Wakala ambalo limekuwa likitumika na chuo hicho badala yake kiitwe Chuo cha Taifa cha Utalii ili kionyeshe hadhi yake kitaifa na kimataifa huku akisisitizia suala la ubunifu katika uendeshaji na kuongeza mapato badala ya kulalamika kukabiliwa na changamoto nyingi ambazo chuo kingeweza kuzitatua.


Amekitaka chuo hicho kuwa cha mfano kwa kuwafundisha wanafunzi k maadili mema kwa kuwa wafanyakazi wengi wa mahoteli nchini wamelalamikiwa kuwa na sifa za udokozi hivyo kuwafanya watu wenye mahoteli kuajiri wafanyakazi kutoka nje ili kuepuka fedheha hiyo.


"Baadhi ya wahudumu katika hoteli zetu wamekuwa na tabia ya udokozi, hii ni sifa mbaya kwa wageni kwani huharibu taswira ya hoteli"


Aliutaka uongozi wa chuo hicho kuwa na mitaala yenye kutoa mafunzo ya kupika vyakula vya asili ili kuenzi utamaduni wa Mtanzania na kuendeleza utalii wa kiutamaduni.

Thursday, October 20, 2016

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI ENG. RAMO MAKANI ATETA NA WANANCHI WALIOVAMIA HIFADHI ZA MISITU MKOANI GEITA

Naibu Waziri wa Maliasili, Mhandisi Ramo Makani akizungumza na wananchi wa eneo la Mchangani waliovamia Hifadhi ya Msitu wa Biharamulo – Kahama uliopo Wilaya ya Chato Mkoani Geita alipotembelea kuona changamoto za uhifadhi. Asilimia 70 ya hifadhi hiyo kwa upande wa Wilaya ya Chato imeharibiwa kabisa na shughuli za kibinadamu ikiwemo kilimo, ufugaji na makazi ya kudumu, nyumba zinazoonekana pichani na sehemu ya makazi hayo.
Naibu Waziri wa Maliasili, Mhandisi Ramo Makani akionesha moja ya kigingi (beacon) cha mpaka wa Hifadhi ya Msitu wa Biharamulo - Kahama uliopo Wilayani Chato Mkoa wa Geita ambao umevunjwa na wananchi waliovamia msitu huo kwa ajili ya kuendesha shughuli za kilimo, ufugaji na makazi. Wa pili kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Geita, Meja Gen. Mstaafu Ezekiel Kyunga na Mkuu wa Wilaya ya Chato, Shaaban Ntarambe (kulia).
Naibu Waziri wa Maliasili, Mhandisi Ramo Makani akizungumza na wananchi wa eneo la Iponyanzege waliovamia Hifadhi ya Msitu wa Biharamulo – Kahama uliopo Wilaya ya Chato Mkoani Geita alipotembelea kuona changamoto za uhifadhi Mkoani humo. 
Naibu Waziri wa Maliasili, Mhandisi Ramo Makani akizungumza na viongozi wa Mkoa wa Geita na Wilaya ya Chato katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya hiyo alipofanya ziara katika maeneo ya hifadhi yenye changamoto Mkoani humo kwa ajili ya kuyatafutia suluhu ya kudumu.
Hizi ni miongoni mwa athari za uvamizi wa wananchi hao katika Hifadhi ya Misitu wa Biharamulo - Kahama Wilayani Chato Mkoa wa Geita ambapo miti ya asili imekatwa kupisha shughuli za kilimo, ufugaji na makazi bila kujali athari za tabianchi. 

_______________________________________

Wananchi wanaozunguka hifadhi za misitu na wanyamapori nchini wametakiwa kutii sheria za uhifadhi na kujiepusha na vitendo viovu vya uharibifu wa mazingira vinavyopelekea kupotea kwa uoto wa asili na kutishia nchi kuwa jangwa ambapo pamoja na mambo mengine wametakiwa kuondoa mifugo yao katika maeneo yaliyohifadhiwa kisheria. 

Hayo yamesemwa juzi Mkoani Geita na Naibu Waziri, Wizara ya Maliasili na Utalii, Mhandisi Ramo Makani wakati akizungumza na viongozi na watendaji wa Mkoa huo Wilayani Chato kuhusu maelekezo ya kuwaondoa wananchi waliovamia maeneo hifadhi Mkoani humo na taifa kwa ujumla.

Alieleza kuwa vitendo hivyo vya uharibifu wa mazingira ni pamoja na ukataji wa miti hovyo, kilimo kisichoendelevu, uchungaji holela wa mifugo, uanzishaji makazi na shughuli zingine za kibinadamu katika maeneo yaliyohifadhiwa kisheria ikiwemo Hifadhi za Misitu, Mapori ya Akiba, Mapori Tengefu na Hifadhi za Taifa.

"kwa sasa Tanzania inapoteza takriban hekta 372,000 za uoto wa asili kila mwaka na endapo hali hiyo ikiachwa iendelee tishio la kutoweka kwa uoto huo ni kubwa zaidi. Takwimu pia zinaonyesha kuwa Tanzania ina eneo la uoto wa asili lenye ukubwa wa takriban Hekta milioni 48.1 na kwamba kasi hiyo ikiachwa iendelee itaiacha Tanzania bila uoto wa asili baada ya miaka 129" alisema Makani.

Akizungumzia taratibu za kuwaondoa wananchi katika maeneo yaliyohifadhiwa kisheria alisema watumishi na viongozi wote wa Serikali wanaotekeleza zoezi hilo wanatakiwa kufuata sheria na miongozo iliyowekwa ikiwa ni pamoja na kujiepusha na vitendo viovu vinavyoweza kuichafua Serikali ikiwemo rushwa na unyanyasaji wa wananchi, "watakaobainika kwenda kinyume na utaratibu huo watachukuliwa hatua za kisheria" alisema.

Katika utekelezaji na usimamizi wa sheria hizo za uhifadhi, aliwataka watumishi wa Wizara ya Maliasili na Utalii kusimamia sheria hizo kila siku na kuendesha utekelezaji wake kwa kushirikiana na kamati za ulinzi na usalama za Wilaya na Mikoa ili kuimarisha utekelezaji wa sheria hizo na kuweka uwazi katika utendaji.

Kwa upande wa wananchi ambao wapo katika vijiji na vitongoji vilivyosajiliwa kisheria aliwataka kutoanzisha au kuendeleza shughuli mpya za kibinadamu hususani zinazosababisha uharibifu wa mazingira ikiwemo kuathiri mabadiliko ya tabia nchi mpaka pale kikosi kazi cha kitaifa kitakapokamilisha kazi yake na kuishauri Serikali namna bora ya kumaliza migogoro ya ardhi nchini.

Maagizo hayo yamekuja ikiwa ni siku chache kabla ya kikosi kazi hicho ambacho kimeundwa na Serikali kikiwa na wajumbe kutoka Wizara sita zinazohusika moja kwa moja na changamoto mbalimbali za ardhi kwa madhumuni ya kufanya uchunguzi wa kina ikiwemo kupitia sheria zote zinazohusika kabla ya kuishauri serikali namna bora ya kumaliza migogoro ya ardhi ikiwemo kwenye maeneo ya hifadhi.

Makani alizitaja wizara hizo kuwa ni Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Maliasili na Utalii, TAMISEMI na Kilimo, Mifugo na Uvuvi ambazo ndizo zimeanza utekelezaji wa zoezi hilo linalotarajiwa kukamilika mwezi Desemba mwaka huu. Alisema Wizara nyingine mbili zitaungana baadae kukamilisha zoezi hilo ambazo ni Maji na Umwagiliaji na Nishati na Madini.

Hata hivyo alitoa tahadhari kwa wananchi juu ya uelewa wa tamko hilo ambapo alisema "Haitarajiwi kwamba Wananchi wengine watatumia vibaya tamko hili na kuanza kuingia katika maeneo ya hifadhi kwa shughuli zozote zile za kibinaadamu kwa kuwa vitendo hivyo havihusiani na tamko hilo na hatua kali zitachukuliwa mara moja dhidi ya wale watakaodiriki kwenda kinyume".

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Geita, Meja Gen. Mstaafu Ezekiel Kyunga alisema Mkoa wake unakabiliwa na uhaba wa ardhi uliosababishwa na ongezeko kubwa la watu waliovutiwa na shughuli za kiuchumi Mkoani humo ikiwemo uchimbaji wa madini, uvuvi, ufugaji pamoja na kilimo ambazo kwa namna moja ama nyingine imekuwa ni changamoto kubwa katika uhifadhi Mkoani humo. Alieleza changamoto nyingine kuwa ni mitazamo tofauti ya baadhi ya wanasiasa kuhusu uhifadhi.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Chato, Shaaban Ntarambe alisema kumekuwepo na uharibifu mkubwa wa misitu Wilayani humo ambapo Hifadhi ya Msitu wa Biharamulo - Kahama kwa upande wa Wilaya yake umeharibiwa kwa asilimia 70 kutokana na shughuli za kilimo, ufugaji, uchimbaji madini na makazi ya kudumu hali inayohatarisha kutoweka kwa hifadhi hiyo.

Msitu wa Biharamulo - Kahama una ukubwa wa hekta 134,684 na upo katika Wilaya tatu za Chato, Bukombe na Biharamulo. Kwa upande wa Wilaya ya Chato ambapo uharibifu  huo umefanyika kwa asilimia 70 una ukubwa wa hekta 30,000.